Swahili na Waswahili

Swahili na Waswahili
Waswahili na Mswahili Rachel Siwa...Pamoja Daima!!

Wednesday 23 August 2017

Kikombe Cha Asubuhi; Leo tunaanza kitabu cha- Kumbukumbu la Sheria 1 (Kumbukumbu la Torati katika tafsiri nyingine)




Shalom,Habari za Asubuhi,Hamjambo,Mmeamkaje?

Haleluyha Mungu wetu yu mwema sana..
Tumshukuru na kumsifu Daima..
Tunamshukuru Mungu wetu kwa kutuongoza na kutupa neema ya kuweza kujifunza katika kitabu cha Hesabu,Nimatumaini yangu wewe unayepitia hapa kuna kitu umejifunza..
Tunamuomba Mungu atupe neema ya kuweza kujifunza kitabu hiki
Kitabu hiki kinaitwa Kumbukumbu la Sheria (Kumbukumbu la Torati katika tafsiri nyingine)

Mungu wetu akatupe macho ya rohoni,Masikio ya kusikia sauti yake..
Tukasome na kumaanisha tukafaidike sisi na kuwafaidisha wengine..
Akatupe Shauku/hamu,kiu ya kupenda kujifunza zaidi..
Tupate kuelewa na kusimamia Neno lake Amri na Sheria zake..
Ee Baba utuongoze..

Basi, kwa vile ahadi ya kuingia mahali pa pumziko bado ipo, na tuogope ili yeyote kati yenu asije akashindwa kupata pumziko hilo. Maana Habari Njema imehubiriwa kwetu kama vile ilivyohubiriwa kwa hao watu wa kale. Lakini ujumbe huo haukuwafaa chochote, maana waliusikia lakini hawakuupokea kwa imani. Basi, sisi tunaoamini tunapata pumziko hilo aliloahidi Mungu. Kama alivyosema: “Nilikasirika, nikaapa: ‘Hawataingia mahali pangu pa pumziko.’” Mungu alisema hayo ingawa kazi yake ilikuwa imekwisha malizika tangu alipoumba ulimwengu. Maana Maandiko yasema mahali fulani kuhusu siku ya saba: “Mungu alipumzika siku ya saba, akaacha kazi zake zote.” Tena jambo hili lasemwa pia: “Hawataingia mahali pangu pa pumziko.” Basi, hiyo ahadi ya kuingia bado ipo, maana wale waliohubiriwa Habari Njema pale awali walishindwa kuingia humo kwa sababu walikosa kutii. Mungu aliweka siku nyingine ambayo inaitwa “Leo,” akasema baadaye kwa njia ya Daudi maneno yaliyokwisha tajwa: “Kama mkisikia sauti ya Mungu leo, msiwe wakaidi.” Kama Yoshua angekuwa amewapa watu hao hilo pumziko, Mungu hangalisema baadaye juu ya siku nyingine. Kwa hiyo, basi, bado kuna kupumzika kwa watu wa Mungu. Maana, kila aingiaye mahali pa pumziko la Mungu atapumzika kutoka katika kazi yake kama vile pia Mungu alivyopumzika kutoka kazi yake. Basi, tujitahidi kuingia katika pumziko hilo, ili asiwepo yeyote miongoni mwetu atakayekataa kutii kama walivyofanya wao. Neno la Mungu ni hai na lina nguvu; ni kali kuliko upanga wenye makali kuwili. Hukata kabisa mpaka mahali ambapo moyo na roho hukutana, mpaka pale vikutanapo viungo vya mwili na uboho. Neno hilo huchambua nia na fikira za mioyo ya watu. Hakuna kiumbe chochote kilichofichika mbele ya Mungu; kila kitu kimefunuliwa wazi mbele ya macho yake yeye ambaye kwake tutapaswa kutoa hoja ya matendo yetu. Basi, tuzingatie kwa makini imani tunayoiungama. Maana tunaye Kuhani Mkuu aliyeingia mpaka mbinguni; Yesu, Mwana wa Mungu. Huyu Kuhani Mkuu wetu anaelewa kabisa unyonge wetu; yeye mwenyewe alijaribiwa kama sisi kwa kila namna lakini hakutenda dhambi. Basi, na tukikaribie bila hofu kiti cha enzi cha Mungu mwenye neema, tupokee huruma na neema ya kutusaidia wakati wa shida.

Tunakushuru Ee Mungu wetu,Baba yetu,Muumba wetu,Muumba wa Mbingu na  Nchi na vyote vilivyomo Baba ni mali yako..
Utukuzwe ee Mungu wetu,Usifiwe,Uabudiwe Milele na Milele..
Tazama jana imepita Mungu wetu Leo ni siku mpya na Kesho ni siku nyingine Baba wa Upendo..
Tunakuja mbele zako Mungu wetu tukijishusha,tukijinyeyekeza na kujiachiliamikononi mwako Jehovah..
Tunaomba utusamehe dhambi zetu zote tulizo zifanya..
Kwakunena,kwakutenda,kwakujua/kutojua..
Mungu wetu tunaomba nasi  utupe neema ya kuweza kuwasamehe wale wote waliotukosea..

Ee Mwenyezi-Mungu, utusikie; utusamehe ee Mwenyezi-Mungu. Ee Mwenyezi-Mungu, kwa hisani yako utusikie na kuchukua hatua, wala usikawie, ee Mungu wangu, kwa ajili ya mji huu na watu hawa wanaoitwa kwa jina lako!
Utuepushe katika majaribu Mungu wetu,Utuokoe na yule mwovu na kazi zake zote..
Nguvu za giza,nguvu za mapepo,nguvu za mizimu na mpinga Kristo zishindwe katika Jina la Bwana wetu Yesu Kristo..

Watoto, mwisho u karibu! Mlikwisha sikia kwamba mpinzani wa Kristo anakuja, na sasa wapinzani wengi wa Kristo wamekwisha fika, na hivyo twajua kwamba mwisho u karibu. Watu hao wametokea kati yetu lakini hawakuwa kweli wa kwetu na ndiyo maana walituacha; kama wangalikuwa wa kwetu, wangalibaki nasi. Lakini waliondoka, wakaenda zao, kusudi ionekane wazi kwamba hawakuwa kamwe wa kwetu. Nyinyi, lakini, mlipata kumiminiwa Roho Mtakatifu na Kristo, na hivyo mnaujua ukweli. Basi, nawaandikieni, si kwa kuwa hamwujui ukweli, bali kwa sababu mnaujua; na pia mnajua kwamba uongo wowote haupatikani katika ukweli. Mwongo ni nani? Ni yule anayekana kwamba Yesu ni Kristo. Mtu wa namna hiyo ni mpinzani wa Kristo – anamkana Baba na Mwana. Maana yeyote anayemkana Mwana, anamkana pia Baba; na yeyote anayemkubali Mwana, anampata Baba pia. Basi, ujumbe ule mliousikia tangu mwanzo na ukae mioyoni mwenu. Kama ujumbe huo mliousikia tangu mwanzo ukikaa ndani yenu, basi, mtaishi daima katika umoja na Mwana na Baba. Na ahadi aliyotuahidia sisi ndiyo hii: Uhai wa milele. Nimewaandikieni mambo haya kuhusu wale wanaotaka kuwapotosha nyinyi. Lakini, kwa upande wenu nyinyi, Kristo aliwatia mafuta kwa Roho wake. Na kama Roho huyo akiendelea kukaa ndani yenu, hamhitaji kufundishwa na mtu yeyote. Maana yeye anawafundisheni kila kitu, na mafundisho yake ni ya kweli, si ya uongo. Basi, shikeni mafundisho ya huyo Roho na kubaki katika muungano na Kristo. Naam, watoto, kaeni ndani yake kusudi wakati atakapotokea tuwe hodari bila kuwa na sababu ya kujificha kwa aibu siku ya kuja kwake. Mnajua kwamba Kristo ni mwadilifu kabisa; basi, mnapaswa kujua pia kwamba kila mtu atendaye mambo adili ni mtoto wa Mungu.

Yahweh tunaomba ututakase Miili yetu na Akili zetu na utufunike kwa Damu ya Mwanao mpendwa Bwana na Mwokozi wetu Yesu Kristo wa Nazareti..

Taabu na mateso
(Marko 13:3-13; Luka 21:7-19)



Yesu alipokuwa ameketi juu ya mlima wa Mizeituni, wanafunzi walimwendea faraghani, wakamwuliza, “Tuambie mambo haya yatatukia lini? Ni ishara gani itakayoonesha kuja kwako na mwisho wa nyakati?” Yesu akawajibu, “Jihadharini msije mkadanganywa na mtu. Maana wengi watatokea wakisema kila mmoja kwamba yeye ndiye Kristo nao watawapotosha watu wengi. Mtasikia juu ya vita na fununu za vita; lakini msifadhaike, maana hayo hayana budi kutokea, lakini mwisho wenyewe ungali bado. Taifa moja litapigana na taifa lingine; ufalme mmoja utapigana na ufalme mwingine. Hapa na pale patakuwa na njaa na mitetemeko ya ardhi. Yote hayo ni kama mwanzo wa maumivu ya kujifungua mtoto. “Kisha watawatoeni ili mteswe na kuuawa. Mataifa yote yatawachukieni kwa sababu ya jina langu. Tena, wengi wataiacha imani yao, watasalitiana na kuchukiana. Watatokea manabii wengi wa uongo watakaowapotosha watu wengi. Kwa sababu ya ongezeko la uhalifu, upendo wa watu wengi utafifia. Lakini atakayevumilia mpaka mwisho ndiye atakayeokolewa. Ila, kabla ya mwisho kufika, hii Habari Njema ya ufalme wa Mungu itahubiriwa ulimwenguni kote kama ushuhuda kwa mataifa yote.

Yeye aliteseka kwanza ili sisi tupatekupona..
Roho Mtakatifu akatuongoze katika yote na tukawe na kiasi..

Jehovah tunaomba ukatubariki na ukabariki kazi za mikono yetu..
ukabariki vyote tunavyoenda kufanya/kutenda Mungu wetu tukatende kama inavyokupendeza wewe..
Yahweh tunaomba ukabariki ridhiki zetu ziingiazo/zitokazo
Mungu wetu tunaomba nasi utupe neema ya kuweza kuwabariki wenyekuhitaji..
Tusipungukiwe katika mahitaji yetu Baba wa Mbinguni ukatupe sawasawa na mapenzi yako..
Mungu wetu tunaweka mikononi mwako Nyumba zetu/Ndoa,watoto/familia ,ndugu na wote wanaotuzunguka..
Baba wa mbinguni ukawatunze na kuwalinda,ukawafunike kwa Damu ya Bwana wetu Yesu Kristo..
Mfalme wa Amani tunaomba ukawaguse na mkono wako wenye nguvu wote wataabikao,wenye shida/tabu ,wanaopitia magumu/majaribu mbalimbali,walio katika vifungo vya yule mwovu...
Mungu wetu ukawaponye kimwili na kiroho pia,ukawaokoe na kuwapa neema ya kukujua wewe,wakasimamie Neno lako wakati wote..


Neema,Baraka,Uponyaji,Upendo,Tumaini,Amani na vyote vinavyoponya mwili na roho vina wewe Mungu wetu..


Asante kwa pendo lako kwetu,Ulinzi wako wakati wote..
Sifa na Utukufu tunakurudishia wewe Mungu wetu..
Kwakuwa Ufalme ni wako Nguvu na Utukufu hata Milele..
Amina..!

Asanteni sana wapendwa kwa kuwa nami..
Baba wa upendo akawe nayi daima..
Nawapenda.


Utangulizi

1Kitabu hiki kina maneno ambayo Mose aliwaambia watu wote wa Israeli wakati walipokuwa nyikani mashariki ya mto Yordani. Walikuwa katika bonde la Yordani karibu na Sufu, kati ya mji wa Parani upande mmoja na mji wa Tofeli, Labani, Hazerothi na Dizahabu, upande mwingine. 2(Ni mwendo wa siku kumi na moja kutoka mlima Horebu hadi Kadesh-barnea kwa njia ya mlima Seiri.) 3Siku ya kwanza ya mwezi wa kumi na moja, mwaka wa arubaini, baada ya kutoka Misri, Mose aliwaambia watu kila kitu ambacho Mwenyezi-Mungu alimwamuru awaambie. 4Taz Hes 2:21-35 Alifanya hivyo baada ya kumshinda mfalme Sihoni wa Waamori ambaye alikuwa anakaa mjini Heshboni, na mfalme Ogu wa Bashani ambaye alikuwa anakaa mjini Ashtarothi na Edrei. 5Mose alichukua jukumu la kuwaelezea watu sheria ya Mungu wakati walipokuwa ngambo ya pili ya mto Yordani.
Aliwaambia hivi: 6“Tulipokuwa mlimani Sinai, Mwenyezi-Mungu, Mungu wetu alituambia hivi: ‘Mmekaa muda wa kutosha kwenye mlima huu; 7sasa vunjeni kambi yenu mwendelee na safari. Nendeni kwenye nchi ya milima ya Waamori na maeneo ya nchi jirani katika Araba, kwenye milima na mabonde, huko Negebu na sehemu za pwani; naam, nendeni mpaka nchi ya Kanaani, na nchi ya Lebanoni, hadi kwenye ule mto mkubwa wa Eufrate. 8Nchi hii yote nimeiweka mbele yenu. Basi, nendeni mkaimiliki nchi hiyo ambayo mimi Mwenyezi-Mungu niliapa kuwapa wazee wenu Abrahamu, Isaka, Yakobo na wazawa wao.’”

Mose ateua waamuzi

(Kut 18:13-27)

9Mose akawaambia watu, “Tulipokuwa bado mlimani Sinai, mimi niliwaambieni hivi: ‘Jukumu la kuwaongozeni ni kubwa mno kwangu mimi peke yangu. 10Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu, amewafanya muwe wengi; leo mmekuwa wengi kama nyota za mbinguni. 11Mwenyezi-Mungu, Mungu wa babu zenu, na awafanye mzidi kuongezeka mara elfu zaidi ya mlivyo sasa na kuwabariki kama alivyoahidi! 12Lakini mimi peke yangu nitawezaje kuchukua jukumu hilo zito la kusuluhisha ugomvi wenu? 13Chagueni kutoka katika kila kabila watu wenye hekima, busara na ujuzi ili niwateue wawe viongozi wenu.’ 14Nyinyi mlikubali, mkanijibu hivi: ‘Jambo ulilosema ni la busara’. 15Hivyo niliwachukua wale viongozi wenye hekima, busara na ujuzi ambao mliwachagua kutoka katika makabila yenu, nikawaweka kuwa viongozi wenu. Niliwaweka wengine kuwa makamanda wa makundi ya watu elfuelfu, ya watu miamia, ya watu hamsinihamsini na ya watu kumikumi. Nilichagua pia maofisa wengine wa kuchunga kila kabila.
16“Wakati huohuo niliwapa waamuzi wenu maagizo yafuatayo: ‘Sikilizeni kesi za watu wenu. Toeni hukumu za haki katika visa vya watu wenu, kadhalika na mizozo ya wageni waishio pamoja nanyi. 17Msimpendelee mtu yeyote katika kutoa hukumu; mtawasikiliza bila upendeleo, wakubwa kwa wadogo. Msitishwe na mtu yeyote, maana hukumu mnayotoa inatoka kwa Mungu. Kesi yoyote ikiwa ngumu zaidi kwenu, ileteni kwangu, nami nitaisikiliza.’ 18Wakati huohuo, niliwaagizeni mambo yote mnayopaswa kufanya.

Uasi wa Israeli kuhusu nchi ya ahadi

(Hes 13:1-33)

19“Basi, kama Mwenyezi-Mungu, Mungu wetu, alivyotuamuru, tulianza safari yetu kutoka mlima Horebu, tukapita katika lile jangwa kubwa la kutisha mnalolijua, kwa kufuata njia inayoelekea nchi ya milima ya Waamori. Tulipofika Kadesh-barnea, 20mimi niliwaambieni: ‘Sasa mmefika katika nchi ya milima ya Waamori ambayo Mwenyezi-Mungu, Mungu wetu, ametupatia. 21Tazameni, Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu, ameiweka nchi hii mbele yenu. Haya! Ingieni, mkaimiliki kama Mwenyezi-Mungu, Mungu wa wazee wenu alivyowaambia. Msiogope wala msifadhaike!’
22“Kisha nyote mlikuja karibu nami mkaniambia, ‘Tutume watu watutangulie, waipeleleze nchi, halafu warudi kutujulisha njia bora ya kufuata na miji ipi tutaikuta huko.’ 23Jambo hilo lilionekana kuwa jema kwangu, nikawateua watu kumi na wawili, mtu mmoja kutoka katika kila kabila. 24Watu hao walikwenda katika nchi ile ya milima, wakafika kwenye bonde la Eshkoli na kulipeleleza. 25Waliporudi, walituletea baadhi ya matunda ya nchi hiyo na wakatuarifu kwamba nchi hiyo anayotupatia Mwenyezi-Mungu, Mungu wetu, ni nzuri.
26“Lakini nyinyi hamkufuata agizo la Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu, kwa kukataa kwenda katika nchi hiyo. 27Mlinungunika ndani ya mahema yenu mkisema, ‘Mwenyezi-Mungu anatuchukia na ndiyo maana alitutoa nchini Misri. Alitaka kututia mikononi mwa Waamori, atuangamize. 28Kwa nini tuende huko hali tumevunjika moyo kwa hofu? Wametuambia kuwa watu wa huko ni wakubwa na warefu kuliko sisi, na kwamba miji yao ni mikubwa na yenye kuta zifikazo mawinguni. Tena wamesema kwamba waliwaona wale wazawa wa Anaki!’1:28 Anaki: Taz Hes 13:22.
29“Lakini mimi niliwaambieni hivi: ‘Msiwe na hofu wala msiwaogope watu hao.’ 30Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu, ambaye huwatangulia, yeye mwenyewe atapigana kwa ajili yenu kama alivyofanya mbele yenu kule Misri na 31kule jangwani ambako mliona jinsi alivyowabeba safari hiyo yote kama vile baba amchukuavyo mwanawe mpaka mkafika hapa. 32Lakini japo nilisema hayo yote, nyinyi hamkumwamini Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu, 33ambaye aliwatangulia njiani na kuwatafutia mahali pa kupiga kambi zenu. Usiku aliwatangulieni kwa moto na mchana kwa wingu, ili kuwaonesha njia.
34“Mwenyezi-Mungu aliyasikia manunguniko yenu, akakasirika, akaapa akisema: 35‘Hakuna hata mmoja wenu katika kizazi hiki kiovu atakayeingia katika nchi ile nzuri niliyoahidi kuwapa wazee wenu. 36Kalebu mwana wa Yefune, ndiye tu atakayeiona; nami nitampatia nchi hiyo aliyoikanyaga iwe yake yeye na wazawa wake kwa kuwa amekuwa mwaminifu kabisa kwangu.’ 37Mwenyezi-Mungu alinikasirikia mimi pia kwa sababu yenu, akasema, ‘Hata wewe Mose hutaingia katika nchi hiyo. 38Lakini msaidizi wako Yoshua mwana wa Nuni, ataingia humo. Basi, mtie moyo kwani yeye atawaongoza watu wa Israeli waimiliki nchi hiyo’. 39Kisha Mwenyezi-Mungu akatuambia sisi sote, ‘Hao watoto wenu mnaoogopa kwamba watakuwa nyara za adui zenu, naam hao walio wadogo ambao hawajui bado kupambanua kati ya mema na mabaya, hao ndio watakaoingia huko, nami nitawapa wao nchi hiyo iwe yao. 40Lakini nyinyi, geukeni na kurudi jangwani kuelekea Bahari ya Shamu.’
41“Kisha mkanijibu, ‘Sisi tumemtendea dhambi Mwenyezi-Mungu, lakini sasa tutakwenda na kupigana kama Mwenyezi-Mungu, Mungu wetu, alivyotuamuru’. Hivyo, kila mmoja wenu akajitayarisha kupigana vita; maana mlifikiri kwamba lingekuwa jambo rahisi kuivamia nchi hiyo ya milima. 42Naye Mwenyezi-Mungu akaniambia, ‘Waambie hao watu wasiende kupigana kwa sababu sipo pamoja nao; wasiende, wasije wakashindwa na adui zao’. 43Basi, mimi niliwaambieni hivyo, lakini nyinyi hamkusikia. Badala yake mlikataa kufuata agizo la Mwenyezi-Mungu, bila kujali mkaingia katika nchi hiyo ya milima. 44Hapo, Waamori waliokuwa wanaishi katika eneo hilo la milimani wakateremka kuwashambulia na kama wafanyavyo nyuki wakawapiga huko Seiri mpaka Horma. 45Ndipo mliporudi, mkamlilia Mwenyezi-Mungu, lakini Mwenyezi-Mungu hakuwasikiliza wala hakuwajali. 46Basi, mkabaki huko Kadeshi kwa muda mrefu ambao mlikaa huko.

Kumbukumbu la Sheria 1:1-46


Biblia Habari Njema kwa Watu Wote(BHN)

"Swahili Na Waswahili"Mbarikiwe.

No comments: