Swahili na Waswahili

Swahili na Waswahili
Waswahili na Mswahili Rachel Siwa...Pamoja Daima!!

Wednesday 23 May 2018

Kikombe Cha Asubuhi ; 1Mambo ya Nyakati 10...



Shalom,Habari za Asubuhi,Hamjambo,Mmeamkaje?

Haleluyah Mungu wetu yu mwema sana..
Tumshukuru Mungu wetu katika yote...

Asante Mungu wetu kwa wema na fadhili zako kwetu
Asante kwa ulinzi wako kwetu wakati wote
Asante kwa kutuchagua tena na kutupa kibali
cha kuendelea kuiona leo hii
Asante kwa pumzi/uzima,afya na kuwa tayari kwa mamjukumu yetu

Utukuzwe ee Mungu wetu,Usifiwe Baba wa Mbinguni
Uhimidiwe Jehovah,Uabudiwe Yahweh
Matendo yako ni makuu mno,Matendo yako ni ya ajabu
Matendo yako yanatisha...!!
Hakuna kama wewe ee Mungu wetu..
Neema yako yatutosha Baba wa Mbinguni...!!


Mtu na atuone sisi kuwa ni watumishi wa Kristo tuliokabidhiwa siri za Mungu. Kinachotakiwa kwa yeyote yule aliyekabidhiwa kazi ni kuwa mwaminifu. Kwangu mimi si kitu nikihukumiwa na nyinyi, au na mahakama ya kibinadamu; wala sijihukumu mimi mwenyewe. Dhamiri yangu hainishtaki kwa jambo lolote, lakini hiyo haionyeshi kwamba sina lawama. Bwana ndiye anayenihukumu. Basi, msihukumu kabla ya wakati wake; acheni mpaka Bwana atakapokuja. Yeye atayafichua mambo ya giza yaliyofichika, na kuonesha wazi nia za mioyo ya watu. Ndipo kila mmoja atapata sifa anayostahili kutoka kwa Mungu. Ndugu, hayo yote niliyosema juu ya Apolo na juu yangu, ni kielelezo kwenu: Kutokana na mfano wangu mimi na Apolo nataka mwelewe maana ya msemo huu: “Zingatieni yaliyoandikwa.” Kati yenu pasiwe na mtu yeyote anayejivunia mtu mmoja na kumdharau mwingine. Nani amekupendelea wewe? Una kitu gani wewe ambacho hukupewa? Na ikiwa umepewa, ya nini kujivunia kana kwamba hukukipewa? Haya! Mmekwisha shiba! Mmekwisha kuwa matajiri! Mmekuwa wafalme bila ya sisi! Naam, laiti mngekuwa kweli watawala, ili nasi pia tutawale pamoja nanyi. Nafikiri Mungu ametufanya sisi mitume tuwe watu wa mwisho kabisa, kama watu waliohukumiwa kuuawa, maana tumekuwa tamasha mbele ya ulimwengu wote, mbele ya malaika na watu.

Yahweh tunakuja mbele zako tukijinyenyekeza,tukijishusha
na kujiachilia mikononi mwako
Mungu wetu tunaomba utusamehe makosa yetu yote tuliyoyafanya
Kwakuwaza,kwakunena,kwakutenda,kwakujua/kutojua
Baba wa Mbinguni nasi tunaomba utupe neema ya kuweza
kuwasamehe wale wote waliotukosea
Jehovah usitutie majaribuni Mungu wetu utuokoe na yule
mwovu na kazi zake zote
Ututakase miili yetu na akili zetu Baba wa Mbinguni
tunaomba utufunike kwa Damu ya Bwana na Mwokozi
wetu Yesu Kristo wa Nazareti yeye aliteseka kwanza ili
sisi tupate kupona...


Sisi ni wapumbavu kwa ajili ya Kristo, lakini nyinyi ni wenye busara katika kuungana na Kristo! Sisi ni dhaifu, nyinyi ni wenye nguvu. Nyinyi mnaheshimika, sisi tunadharauliwa. Mpaka dakika hii, sisi tuna njaa na kiu, hatuna nguo, twapigwa makofi, hatuna malazi. Tena twataabika na kufanya kazi kwa mikono yetu wenyewe. Tukitukanwa, tunawatakia baraka; tukidhulumiwa, tunavumilia; tukisingiziwa, tunajibu kwa adabu. Mpaka sasa tumetendewa kama uchafu wa dunia; na kwa kila mtu sisi ni takataka!

Mungu wetu tunaomba ukabariki kazi za mikono yetu
Baba wa Mbinguni tunaomba ukatupe maarifa na ubunifu katika utendaji
Yahweh nasi tukatende sawasawa na mapenzi yako
Jehovah tunaomba ukabariki ridhiki zetu ziingiazo/zitokazo
Mungu wetu nasi tunaomba ukatupe neema ya kuweza 
kuwabariki wenye kuhitaji
Baba wa Mbinguni tusipungukiwe katika mahitaji yetu
Mungu wetu ukatupe kama inavyokupendeza wewe

Mungu wetu tunayaweka maisha yetu mikononi mwako
Baba wa Mbinguni tunaomba ukabariki nyumba/ndoa zetu,
watoto,wazazi wetu,familia/ndugu na wote wanaotuzunguka
Jehovah tunaomba ulinzi wako kwetu na kwa vyote tunavyo vimiliki
Yahweh tunaomba utubariki tuingiapo/tutokapo
Mungu wetu tunaomba ukavibariki vyote tunavyoenda kugusa/kutumia
Baba wa Mbinguni ukavitakase na kuvifunika kwa Damu
 ya Bwana wetu Yesu Kristo
Mungu wetu ukatamalaki na kutuatamia
Baba wa Mbinguni tukawe salama rohoni
Jehovah ukatupe macho ya kuona na masikio ya kusikia
 sauti yako na kuitii
Mungu wetu tunaomba ukatupe neema ya kufuta njia zako
Baba wa Mbinguni tukasimamie Neno lako amri na sheria zako
siku zote za maisha yetu
Mkono wako wenye nguvu ukatuguse
Mungu wetu ukaonekane katika maisha yetu
Mfalme wa amani amani yako ikatawale katika maisha yetu
Baba wa Mbinguni ukatupe hekima,busara,uvumilivu,utuwema,fadhili
na upendo ukadumu kati yetu
Tuka nene yaliyoyako ee Mungu wetu
Neema zako zikawe nasi Nuru yako ikaangaze katika maisha yetu
Ukatufanye chombo chema Mungu wetu nasi tukatumike 
kama inavyokupendeza wewe
Roho matakatifu akatuongoze katika yote na tukawe na kiasi....


Siandiki mambo haya kwa ajili ya kuwaaibisha nyinyi, bali kwa ajili ya kuwafundisheni watoto wangu wapenzi. Maana hata kama mnao maelfu ya walezi katika maisha yenu ya Kikristo, baba yenu ni mmoja tu, kwani katika kuungana na Kristo mimi ndiye niliyewazaeni kwa kuihubiri Habari Njema. Kwa hiyo, nawasihi: Fuateni mfano wangu. Ndiyo maana nimemtuma Timotheo kwenu. Yeye ni mtoto wangu mpenzi na mwaminifu katika kuungana na Bwana. Atawakumbusheni njia ninayofuata katika kuungana na Kristo; njia ninayofundisha kila mahali katika makanisa yote. Baadhi yenu wameanza kuwa na majivuno wakidhani kwamba sitakuja tena kwenu. Lakini, Bwana akipenda, nitakuja kwenu upesi; na hapo ndipo nitakapojionea mwenyewe, sio tu kile wanachoweza kusema hao wenye majivuno, bali pia kile wanachoweza kufanya. Maana ufalme wa Mungu si shauri la maneno matupu, bali ni nguvu. Mnapendelea lipi? Nije kwenu na fimbo, ama nije na moyo wa upendo na upole?


Mungu wetu tunawaweka mikonioni mwako watoto wetu
Baba wa Mbinguni tunaomba ukawaongoze katika hatua zao
Jehovah tunaomba ukawape ufahamu,akili,maarifa,
wakatambue mema na mabaya
Ukafungue masikio yao ee Mungu wetu na wakapate kusikia
sauti yako na wakawe watiifu kwako Mungu,wazazi/walezi,
walimu,wakubwa/wadogo
Mungu wetu wasipate kusikia yanayokwenda kinyume nawe
wasisikilize taarifa potofu zinazo jenga hofu
na zisizokupendeza Mungu wetu
Baba wa Mbinguni tunaomba ukawape macho ya rohoni
Mungu wetu ukayatawale macho yao wakapate kuangalia
yaliyo mema na sikuona yasioyo faa..
Baba wa Mbinguni tunaomba ukalinde vinywa vyao
Mungu wetu wakanene yaliyo yako,ukawaokoe na
Uongo,matusi na yote yasiyokupendeza Mungu
Maneno yao yakapate kibali  mbele zako Mungu na yakawanufaishe
wale wote watakao yasikiliza na kuwajengea kiimani na utii..
Ukawape Moyo wa furaha,amani,uchangamfu na kukujua wewe Mungu mapema katika makuzi yao  ee Baba wa Mbinguni ukatawale maisha yao
Ubariki mikono yao Mungu wetu wakafanye kazi zilizo zao kwa bidii
na imani na ukazibariki kazi za mikono yao
Mungu wetu tunaomba ukabariki miguu yao watembeapo
wakatembee njia zilizo zako,wasiambatane na walio waovu,wakaambatane na wenye hekima  na njia zao zikawe salama
Mungu wetu ukawalinde katika ujana wao na ukawaokoe na hatari
zote katika ujana wao wakawe watoto wema,wawe kaka/dada
wema na ili  waje  kuwa mama/baba wazuri mbele zako Mungu
na mbele  ya jamii yote...
Ee Mungu wetu tunaomba ukasikie kuomba kwetu
Baba wa Mbinguni tunaomba ukapokee sala/maombi yetu
Jehovah ukatende sawasawa na mapenzi yako
kwakuwa Ufalme ni wako Nguvu na Utukufu hata Milele
Amina...!!

Asanteni sana wapendwa/waungwana kwakuwa nami
Mungu Baba aendelee kuwabariki  na kwatendea kama
inavyompendeza yeye
Amani ya Bwana wetu Yesu Kristo na Upendo wa Mungu Baba
ukae nanyi daima.
Nawapenda.



Kifo cha mfalme Shauli

(1Sam 31:1-13)

1Basi, Wafilisti walipigana vita dhidi ya Waisraeli; nao Waisraeli walikimbia mbele ya Wafilisti na kuuawa katika mlima wa Gilboa. 2Lakini Wafilisti wakamzingira Shauli na wanawe, kisha wakawaua Yonathani, Abinadabu na Malki-shua wana wa Shauli. 3Vita vilikuwa vikali sana dhidi ya Shauli. Wapiga mishale walipomwona walimjeruhi.
4Ndipo Shauli alipomwambia mtu aliyembebea silaha, “Chomoa upanga wako unichome nife, ili watu hawa wasiotahiriwa wasije wakanidhihaki.” Lakini huyo aliyembebea silaha hakuthubutu; kwa sababu aliogopa sana. Hivyo, Shauli alichukua upanga wake mwenyewe akauangukia. 5Halafu yule aliyembebea silaha alipoona kuwa Shauli amekufa, naye pia akauangukia upanga wake, akafa. 6Hivyo ndivyo Shauli alivyokufa, yeye na wanawe watatu, na jamaa yake yote. 7Nao watu wa Israeli walioishi bondeni walipoona jeshi limewakimbia maadui, na ya kuwa Shauli na wanawe wamekufa, waliihama miji yao wakakimbia. Wafilisti wakaenda na kukaa katika miji hiyo.
8Kesho yake, Wafilisti walipokwenda kuwateka nyara hao waliouawa, waliikuta maiti ya Shauli na wanawe mlimani Gilboa. 9Walimvua mavazi, wakachukua kichwa chake pamoja na silaha zake, halafu walituma wajumbe katika nchi yote ya Filistia kutangaza habari njema kwa sanamu zao na watu. 10Waliziweka silaha za Shauli katika hekalu la miungu yao; kisha wakakitundika kichwa chake katika hekalu la Dagoni. 11Lakini watu wa Yabesh-gileadi waliposikia yote Wafilisti waliyomtendea Shauli, 12mashujaa wote waliondoka na kuuchukua mwili wa Shauli na miili ya wanawe, wakaileta mpaka Yabeshi. Wakaizika mifupa yao chini ya mwaloni huko Yabeshi, nao wakafunga kwa muda wa siku saba.
13Shauli alikufa kwa sababu ya kutokuwa mwaminifu; hakuwa mwaminifu kwani hakutii neno la Mwenyezi-Mungu na alikwenda kwa mwaguzi kumtaka shauri, 14badala ya kumwendea Mwenyezi-Mungu ili kumtaka shauri. Kwa sababu hiyo Mwenyezi-Mungu akamuua, na ufalme wake akampa Daudi mwana wa Yese.


1Mambo ya Nyakati10;1-14


Biblia Habari Njema kwa Watu Wote(BHN)

"Swahili Na Waswahili"Mbarikiwe.

No comments: