Swahili na Waswahili

Swahili na Waswahili
Waswahili na Mswahili Rachel Siwa...Pamoja Daima!!

Wednesday 25 April 2018

Kikombe Cha Asubuhi ; 2 Wafalme 15......




Shalom,Habari za Asubuhi,Hamjambo,Mmeamkaje?

Haleluyah Mungu wetu yu mwema sana...
Tumshukuru Mungu katika yote....

Asante Mungu wetu kwa wema na fadhili zako kwetu
Asante kwa ulinzi wako kwetu wakati wote
Asante kwakutuchagua tena na kutupa kibali cha kuendelea
kuiuona leo hii
Asante kwa pumzi/uzima,afya na kuwa tayari kwa majukumu yetu.....

Utukuzwe ee Mungu wetu,usifiwe Baba wa Mbinguni,
Uhimidiwe ee Jehovah,Uabudiwe Yahweh..!!
Neema yako yatutosha ee Mungu wetu..!!

Mkaribisheni kwenu mtu aliye dhaifu, lakini msibishane naye juu ya mawazo yake binafsi. Watu hutofautiana: Mmoja imani yake inamruhusu kula kila kitu; lakini mwingine ambaye imani yake ni dhaifu, hula tu mboga za majani. Mtu ambaye hula kila kitu asimdharau yule ambaye hawezi kula kila kitu; naye ambaye hula tu mboga za majani asimhukumu anayekula kila kitu, maana Mungu amemkubali. Wewe ni nani hata uthubutu kumhukumu mtumishi wa mwingine? Akisimama au akianguka ni shauri la Bwana wake; naam, atasimama imara, maana Bwana anaweza kumsimamisha.

Mungu wetu tunakuja mnbele zako tukijinyenyekeza,tukijishusha
na kujiachilia mikononi mwako
Baba wa Mbinguni tunaomba utusamehe makosa yetu yote tuliyoyatenda
Kwakuwaza,kwakunena,kwakutenda,kwakujua/kutojua
Yahweh nasi tunaomba utupe neema ya kuweza kuwasamehe 
wale wote waliotukosea
Mungu wetu usitutie majaribuni Baba wa Mbinguni
tunaomba utuokoe na yule mwovu na kazi zake zote
Jehovah tunaomba ututakase miili yetu na akili zetu
Mungu wetu utufunike kwa Damu ya Bwana na Mwokozi wetu
 Yesu Kristo wa Nazareti,yeye aliteseka kwanza ili sisi tupate kupona...

Yahweh tunaomba ukabariki kazi za mikono yetu
Mungu wetu tunaomba ukatupe ubunifu na maarifa katika utendaji
Baba wa Mbinguni nasi tukatende sawasawa na mapenzi yako
Jehovah tunaomba ukabariki ridhiki zetu ziingiazo/zitokazo
Mungu wetu nasi tunaomba ukatupe neema ya kuweza kuwabariki
wenye kuhitaji
Yahweh tusipungukiwe katika mahitaji yetu Mungu wetu ukatupe
kama inavyokupendeza wewe...

Mtu anaweza kufikiria siku fulani kuwa ya maana zaidi kuliko nyingine; mtu mwingine aweza kuzifikiria siku zote kuwa sawa. Kila mmoja na afuate msimamo wa akili yake. Anayeadhimisha siku fulani anaadhimisha siku hiyo kwa ajili ya kumtukuza Mungu; naye anayekula chakula fulani anafanya hivyo kwa kumtukuza Bwana maana anamshukuru Mungu. Kadhalika naye anayeacha kula chakula fulani anafanya hivyo kwa ajili ya kumtukuza Bwana, naye pia anamshukuru Mungu. Maana hakuna mtu yeyote miongoni mwetu aishiye kwa ajili yake mwenyewe, wala hakuna anayekufa kwa ajili yake mwenyewe maana tukiishi twaishi kwa ajili ya Bwana; tukifa, tunakufa kwa ajili ya Bwana. Basi, kama tukiishi au tukifa, sisi ni mali yake Bwana. Maana Kristo alikufa, akafufuka ili apate kuwa Bwana wa walio hai na wafu. Kwa nini basi, wewe wamhukumu ndugu yako? Nawe, kwa nini wamdharau ndugu yako? Sisi sote tutasimama mbele ya kiti cha hukumu cha Mungu. Maana Maandiko yanasema: “Kama niishivyo, asema Bwana, kila mtu atanipigia magoti, na kila mmoja atakiri kwamba mimi ni Mungu.” Kwa hiyo, kila mmoja wetu atatoa hoja juu yake mwenyewe mbele ya Mungu.

Mfalme wa amani tunaomba amani yako ikatawale katika maisha yetu
Mungu wetu tunaomba ukabariki nyumba/ndoa zetu,watoto,wazazi wetu,
familia/ndugu na wote wanaotuzunguka..
Baba wa Mbinguni tunaomba ulinzi wako kwetu na kwa vyote tuvyovimiliki
Jehovah tunaomba ukatubariki tuingiapo/tutokapo 
Yahweh tunaomba ukabariki vyote tunavyoenda kugusa/kutumia
Mungu wetu ukavitakase na kuvifunika kwa Damu ya Bwana wetu Yesu Kristo,Baba wa Mbinguni tunaomba ukatamalaki na kutuatamia 
Yahweh tukawe salama rohoni Jehovah ukatupe macho ya kuona na 
masikio ya kusikia sauti yako na kuitii
Mungu wetu ukatupe neema ya kufuata njia zako Yahweh tukasimamie
Neno lako amri na sheria zako siku zote za maisha yetu
Baba wa Mbinguni ukatupe neema ya kutambua mema na mabaya
Jehovah Nuru yako ikaangaze katika maisha yetu..
Tukawe barua njema Mungu wetu nasi tukasomeke kama 
inavyokupendeza wewe
Roho Mtakatifu akatuongoze katika yote na tukawe na kiasi...


Basi, tuache kuhukumiana, bali tuazimie kutokuwa kamwe kikwazo kwa ndugu au kumsababisha aanguke katika dhambi. Katika kuungana na Bwana Yesu, nina hakika kwamba hakuna kitu chochote kilicho najisi kwa asili yake; lakini, mtu akidhani kwamba kitu fulani ni najisi, basi, kwake huwa najisi. Kama ukimhuzunisha ndugu yako kwa sababu ya chakula unachokula, basi mwenendo wako hauongozwi na upendo. Usikubali hata kidogo chakula chako kiwe sababu ya kupotea kwa mtu mwingine ambaye Kristo alikufa kwa ajili yake! Basi, msikubali kitu mnachokiona kwenu kuwa chema kidharauliwe. Maana ufalme wa Mungu si shauri la kula na kunywa, bali unahusika na kuwa na uadilifu, amani na furaha iletwayo na Roho Mtakatifu. Anayemtumikia Kristo namna hiyo humpendeza Mungu, na kukubaliwa na watu. Kwa hiyo tuyazingatie daima mambo yenye kuleta amani, na yanayotusaidia kujengana. Basi, usiiharibu kazi ya Mungu kwa sababu ya ubishi juu ya chakula. Vyakula vyote ni halali, lakini haifai kula chakula ambacho kitamfanya mtu aanguke katika dhambi. Afadhali kuacha kula nyama, kunywa divai, au kufanya chochote ambacho chaweza kumsababisha ndugu yako aanguke. Basi, shikilia unachoamini kati yako na Mungu wako. Heri mtu yule ambaye, katika kujiamulia la kufanya, haipingi dhamiri yake. Lakini mtu anayeona shaka juu ya chakula anachokula, anahukumiwa kama akila, kwa sababu msimamo wa kitendo chake haumo katika imani. Na, chochote kisicho na msingi wake katika imani ni dhambi.
Mungu wetu tazama  wenye shida/tabu,wagonjwa,wenye njaa,
wanaopitia magumu/majaribu mbalimbali,waliokata
tamaa,waliokataliwa,wenye hofu na mashaka,walio katika vifungo
vya yule mwovu,waliokwama kibiashara,kielimu,wanaotafuta watoto,
na wote wanaokutafuta kwa bidii na imani
Baba wa Mbinguni tunaomba ukawaguse kwa mkono wako wenye nguvu
Yahweh tunaomba ukawaponye kimwili na kiroho pia
Jehovah tunaomba ukawaokoe na kuwavusha salama
Mungu wetu tunaomba ukawatendee kila mmoja na mahitaji yake
Baba wa Mbinguni tunaomba ukaonekane katika maisha yao
Yahweh tunaomba ukawasamehe pale walipokwenda kinyume nawe
Jehovah ukawape neema ya kujiombea na kufuata njia zako
nazo ziwaweke huru
Yahweh nuru yako ikaangaze katika maisha yao,amani ikatawale
Ukawape macho ya rohoni Mungu wetu...
Ee Baba tunaomba ukasikie na ukapokee sala/maombi yetu
Mungu Baba tunaomba ukawatendee sawasawa na mapenzi yako
Kwakuwa Ufalme ni wako Nguvu na Utukufu hata Milele
Amina..!!

Asanteni sana wapendwa katika Kristo Yesu kwakuwa nami/kunisoma
Baba wa Mbinguni aendelee kuwabariki na kuwatendea kama inavyompendeza yeye...
Nawapenda.

Mfalme Azaria wa Yuda

(2Nya 26:1-23)

1Katika mwaka wa ishirini na saba wa utawala wa Yeroboamu mfalme wa Israeli, Azaria mwana wa Amazia mfalme wa Yuda alianza kutawala. 2Alikuwa na umri wa miaka kumi na sita alipoanza kutawala. Alitawala kwa muda wa miaka hamsini na miwili huko Yerusalemu. Mama yake alikuwa Yekolia wa Yerusalemu. 3Alitenda mema mbele ya Mwenyezi-Mungu sawasawa na yote baba yake aliyotenda. 4Hata hivyo, mahali pa ibada milimani hapakuharibiwa, na watu waliendelea kutambika na kufukiza ubani hapo. 5Mwenyezi-Mungu akamwadhibu Azaria, akawa na ukoma mpaka alipokufa. Alikaa katika nyumba ya pekee na shughuli zake zote za utawala ziliendeshwa na mwanawe Yothamu.
6Matendo mengine yote ya Azaria yameandikwa katika Kitabu cha Mambo ya Nyakati za Wafalme wa Yuda. 7Azaria alifariki na kuzikwa katika makaburi ya wafalme katika mji wa Daudi; na mwanawe Yothamu alitawala mahali pake.

Mfalme Zekaria wa Israeli

8Katika mwaka wa thelathini na nane wa enzi ya Azaria mfalme wa Yuda, Zekaria mwana wa Yeroboamu alianza kutawala Israeli, akatawala kwa muda wa miezi sita. 9Naye, kama vile watangulizi wake, alimwasi Mwenyezi-Mungu. Alifuata mfano mbaya wa mfalme Yeroboamu mwana wa Nebati, ambaye aliwapotosha watu wa Israeli wakatenda dhambi. 10Shalumu mwana wa Yabeshi alikula njama dhidi ya mfalme Zekaria, akampiga mbele ya watu na kumwua, kisha akatawala mahali pake.
11Matendo mengine yote ya Zekaria yameandikwa katika Kitabu cha Mambo ya Nyakati za Wafalme wa Israeli.
12Basi tukio hilo lilitokana na ahadi ya Mwenyezi-Mungu kwa mfalme Yehu, kusema, “Wazawa wako watatawala Israeli mpaka kizazi cha nne.”

Mfalme Shalumu wa Israeli

13Katika mwaka wa thelathini na tisa wa enzi ya mfalme Azaria wa Yuda, Shalumu mwana wa Yabeshi alianza kutawala Israeli, akatawala huko Samaria kwa muda wa mwezi mmoja. 14Menahemu mwana wa Gadi aliondoka Tirza kwenda Samaria, na huko akamuua Shalumu mwana wa Yabeshi, kisha akatawala mahali pake. 15Matendo mengine yote ya Shalumu na njama zake zote alizofanya, yameandikwa katika Kitabu cha Mambo ya Nyakati za Wafalme wa Israeli. 16Menahemu alipokuwa njiani kutoka Tirza, aliuharibu kabisa mji wa Tapua na kuangamiza wakazi wake pamoja na nchi yote iliyozunguka kwa sababu hawakujisalimisha kwake. Isitoshe, aliwatumbua wanawake waja wazito wote.

Mfalme Menahemu wa Israeli

17Katika mwaka wa thelathini na tisa wa enzi ya mfalme Azaria wa Yuda, Menahemu mwana wa Gadi alianza kutawala Israeli, akatawala huko Samaria kwa muda wa miaka kumi. 18Alimwasi Mwenyezi-Mungu siku zote za utawala wala hakuacha maovu ya Yeroboamu mwana wa Nebati, ambaye aliwapotosha watu wa Israeli wakatenda dhambi. 19Basi, Pulu15:19 Pulu: Katika 1Nya 5:26: Tiglath-pileseri. mfalme wa Ashuru, aliivamia Israeli, naye Menahemu akampa kilo thelathini na nne za fedha ili amsaidie kuimarisha mamlaka yake juu ya nchi ya Israeli. 20Menahemu alipata fedha hiyo kwa kuwalazimisha matajiri wa Israeli kutoa mchango wa shekeli hamsini za fedha kila mmoja. Halafu Pulu hakukaa Israeli bali alirudi katika nchi yake.
21Matendo mengine yote ya Menahemu yameandikwa katika Kitabu cha Mambo ya Nyakati za Wafalme wa Israeli. 22Menahemu alifariki, naye mwanawe Pekahia alitawala mahali pake.

Mfalme Pekahia wa Israeli

23Katika mwaka wa hamsini wa enzi ya mfalme Azaria wa Yuda, Pekahia mwana wa Menahemu alianza kutawala Israeli, akatawala huko Samaria kwa muda wa miaka miwili. 24Alimwasi Mwenyezi-Mungu na kufuata mfano mbaya wa mfalme Yeroboamu mwana wa Nebati, ambaye aliwafanya watu wa Israeli watende dhambi. 25Peka mwana wa Remalia, ambaye alikuwa ofisa wa jeshi la Pekahia, alishirikiana na watu wengine hamsini kutoka Gileadi, akamuua Pekahia katika ngome ya ndani ya nyumba ya mfalme huko Samaria, na kuwa mfalme mahali pake.
26Matendo mengine ya Pekahia na yote aliyofanya yameandikwa katika Kitabu cha Mambo ya Nyakati za Wafalme wa Israeli.
Mfalme Peka wa Israeli
27Katika mwaka wa hamsini na mbili wa enzi ya mfalme Azaria wa Yuda, Peka mwana wa Remalia alianza kutawala huko Samaria, akatawala kwa muda wa miaka ishirini. 28Alimwasi Mwenyezi-Mungu kwa kufuata mfano mbaya wa mfalme Yeroboamu mwana wa Nebati, aliyewafanya watu wa Israeli watende dhambi.
29Wakati wa enzi ya Peka mfalme wa Israeli, Tiglath-pileseri, mfalme wa Ashuru, aliteka miji ya Iyoni, Abel-beth-maaka, Yanoa, Kadeshi na Hazori, pamoja na nchi za Gileadi, Galilaya na Naftali na kuwachukua mateka wakazi wao.
30Katika mwaka wa ishirini wa utawala wa Yothamu mwana wa Uzia mfalme wa Yuda, Hoshea mwana wa Ela alikula njama dhidi ya Peka, mwana wa Remalia, na akamuua, kisha akatawala mahali pake. 31Matendo mengine ya Peka na yote aliyoyafanya yameandikwa katika Kitabu cha Mambo ya Nyakati za Wafalme wa Israeli.

Mfalme Yothamu wa Yuda

(2Nya 27:1-9)

32Katika mwaka wa pili wa enzi ya Peka mwana wa Remalia huko Israeli, Yothamu mwana wa Uzia mfalme wa Yuda alianza kutawala Yuda. 33Alikuwa na umri wa miaka ishirini na mitano alipoanza kutawala; alitawala huko Yerusalemu kwa muda wa miaka kumi na sita. Mama yake aliitwa Yerusha, binti Sadoki. 34Kama vile Uzia baba yake, Yothamu alitenda mambo yaliyompendeza Mwenyezi-Mungu. 35Hata hivyo, mahali pa kuabudia miungu ya uongo hapakuharibiwa, na watu waliendelea kutoa sadaka na kufukiza ubani kwenye mahali pa juu. Yothamu alijenga lango la kaskazini la nyumba ya Mwenyezi-Mungu.
36Matendo mengine ya Yothamu na yote aliyofanya yameandikwa katika Kitabu cha Mambo ya Nyakati za Wafalme wa Yuda. 37Wakati wa enzi ya Yothamu, Mwenyezi-Mungu alianza kutuma mfalme Resini wa Aramu na mfalme Peka wa Israeli ili kushambulia Yuda. 38Yothamu akafariki na kuzikwa katika makaburi ya kifalme katika mji wa Daudi. Mwanae Ahazi alitawala mahali pake.



2Wafalme15;1-38


Biblia Habari Njema kwa Watu Wote(BHN)

"Swahili Na Waswahili"Mbarikiwe.

No comments: