Swahili na Waswahili

Swahili na Waswahili
Waswahili na Mswahili Rachel Siwa...Pamoja Daima!!

Thursday 25 January 2018

Kikombe Cha Asubuhi ;1Samueli29...



Shalom,Habari za Asubuhi,Hamjambo,Mmeamkaje?

Haleluyah Mungu wetu yu mwema sana..
Tumshukuru Mungu wetu katika yote..

Asante Baba wa Mbinguni kwa wema na fadhili zako kwetu
Asante kwa ulinzi wako kwetu wakati wote
Asante kwakutuchagua tena na kutupa kibali cha kuendelea kuiona leo hii
Asante kwa pumzi/uzima,afya na kuwa tayari kwa majukumu yetu..
Utukuzwe ee Mungu wetu,Unastahili sifa Baba wa Mbinguni,Unastahili kuabudiwa Jehovah,Unastahili kuhimidiwa Yahweh,Utukufu una wewe ee Mungu wetu,Mungu wa Abrahamu,Isaka na Yakobo..
Mungu mwenye nguvu,muweza wa yote,Alpha na Omega...

Baba wa Mbinguni tunakuja mbele zako tujinyenyekeza,tukijishusha na kujiachilia mikononi mwako
Jehovah tunaomba utusamehe dhambi zetu zote tulizo zifanya
kwakuwaza,kwakunena,kwakutenda,kwakujua/kutojua
Yahweh nasi tunaomba utupe neema ya kuweza kuwasamehe wale wote waliotukosea..
Baba wa Mbinguni tunaomba utuepushe katika majaribu Yahweh utuokoe na yule mwovu na kazi zake zote..
Nguvu za giza,nguvu za mapepo,nguvu za mizimu,nguvu za mpinga Kristo na vyote vinavyokwenda kinyume nawe Baba  vikashindwe katika jina la Bwana wetuYesu Kristo ...
Mungu wetu tunaomba ututakase miili yetu na akili zetu Yahweh tunaomba utufunike kwa Damu ya Bwana na Mwokozi wetu Yesu Kristo wa Nazareti yeye aliteseka kwanza ili sisi tupate kupona..


Je, tunaanza tena kujipendekeza? Je, tunahitaji barua ya utambulisho kwenu, au kutoka kwenu, kama watu wengine? Nyinyi wenyewe ni barua yetu; barua iliyoandikwa mioyoni mwetu kila mtu aione na kuisoma. Ni dhahiri kwamba nyinyi ni barua ya Kristo aliyoipeleka kwa mikono yetu. Barua yenyewe imeandikwa si kwa wino, bali kwa Roho wa Mungu aliye hai; imeandikwa si juu ya kipande cha jiwe, bali juu ya mioyo ya watu. Tunaweza kusema hayo kwa sababu ya tumaini letu tulilo nalo kwa Mungu kwa njia ya Kristo. Si kwamba sisi tunaweza kufanya chochote kwa nguvu zetu wenyewe, ila uwezo wetu wote hutoka kwa Mungu: Maana yeye ndiye aliyetuwezesha kulihudumia Agano Jipya ambalo si agano la sheria iliyoandikwa, bali agano la Roho. Maana sheria iliyoandikwa huleta kifo, lakini Roho huleta uhai.

Jehovah tunaomba ukabariki kazi za mikono yetu
Yahweh ukatupe ubunifu na maarifa katika ufanyaji/utendaji nasi tukatende sawasawa na mapenzi yako
Mungu wetu tunaomba ukabariki ridhiki zetu ziingiazo/zitokazo
Baba wa Mbinguni nasi tunaomba utupe neema ya kuweza kuwabariki wenye kuhitaji
Yahweh tusipungukiwe katika mahitaji yetu Mungu wetu tunaomba ukatupe kama inavyokupendeza wewe..

Mungu wetu tunayaweka maisha yetu mikononi mwako
Yahweh tunaomba ukabariki nyumba/ndoa zetu,watoto,wazazi wetu,familia/ndugu na wote wanaotuzunguka
Mungu Baba tunaomba ulinzi wako kwetu na kwa vyote tunavyovimiliki
Yahweh ukatungoze tuingiapo na tutokapo Mungu wetu ukatuponye nafsi zetu Jehovah tukawe salama moyoni Baba wa Mbinguni ukatupe macho ya kuona na masikio ya kusikia sauti yako na kuitii
Mungu wetu ukatupe neema ya kufuata njia zako Jehovah tukasimamie Neno lako amri na sheria zako siku zote za maisha yetu
Mfalme wa amani tunaomba amani yako ikatawale,upendo ukadumu kati yetu,utu wema na kujali wengine,tukatende  yote yanayokupendeza wewe na ukatuokoe na kiburi,majivuno,makwazo na yote yanayokwenda kinyume nawe..
Mungu wetu ukaonekane popote tupitapo Jehovah na ikajulikane kwamba upo Baba wa Mbinguni...
tukawe barua njema Mungu wetu na tukasomeke kama inavyokupendeza wewe..
Roho Mtakatifu akatuongoze katika yote na tukawe na kiasi...


Sheria iliwekwa kwa kuandikwa juu ya vipande vya mawe. Ingawaje mwisho wake umekuwa kifo, utukufu wake ulikuwa mkuu mno hata wana wa Israeli wasiweze kuutazama uso wa Mose kwa sababu ya mngao wake. Tena mngao huo ulikuwa wa muda tu. Basi, ikiwa huduma ya kile ambacho kimesababisha kifo imefanyika kwa utukufu mwingi kiasi hicho, basi, huduma ya Roho ina utukufu mkuu zaidi. Ikiwa basi, kulikuwa na utukufu katika huduma ile iliyoleta hukumu, ni wazi kwamba huduma iletayo uadilifu itakuwa na utukufu mkuu zaidi. Sasa utukufu mkuu zaidi umechukua nafasi ya ule utukufu uliokuja hapo awali, ambao fahari yake imekwisha toweka. Maana ikiwa kile kilichokuwa cha muda tu kilikuwa na utukufu wake, bila shaka kile chenye kudumu milele kitakuwa na utukufu mkuu zaidi. Kwa vile hili ndilo tumaini letu, sisi twasema kwa uhodari mkuu. Sisi hatufanyi kama Mose ambaye alilazimika kuufunika uso wake kwa kitambaa ili watu wa Israeli wasiuone ule mwisho wa mngao ule uliokuwa unafifia. Lakini akili zao zilipumbazwa. Mpaka leo hii lisomwapo Agano la Kale, kifuniko hicho bado kipo. Kifuniko hicho kitaondolewa tu mtu anapoungana na Kristo. Naam, mpaka hivi leo kila isomwapo sheria akili zao huwa zimefunikwa. Lakini, wakati mtu amgeukiapo Bwana, kifuniko hicho huondolewa. Hapa “Bwana” ni Roho; na pale alipo Roho wa Bwana ndipo ulipo uhuru. Basi, sisi sote ambao nyuso zetu hazikufunikwa, tunaona kama katika kioo, utukufu wa Bwana; tunabadilishwa tufanane zaidi na huo mfano wake kwa utukufu mwingi zaidi. Hiyo ni kazi yake Roho wa Bwana.

Yahweh tunaomba ukawaguse kwa mkono wako wenye nguvu wenye shida/tabu,wagonjwa,wenye njaa,walio katika vifungo vya yule mwovu,walio kataliwa,walio kata tamaa,wenye hofu na mashaka,wanaopitia magumu/majaribu mbalimbali,walio anguka/potea Mungu wetu tunaomba ukawaponye kiroho na kimwili pia Yahweh tunaomba ukawaongoze na kuwasiamisha tena Baba wa Mbinguni tunaomba  ukawape neema ya kujiombea,kufuata njia zako,wakapate kutambua/kujitambua,ukawasamehe Mungu wetu na ukasikie kilio chao Yahweh ukawafute machozi ya watoto wako wanaokulilia,kukuomba,kukurudia Baba ukawapokee wote wanaokuomba kwa bidii na imani..
Jehovah tunaomba ukasikie,ukapokee na ukajibu sala/maombi yetu
Yahweh ukawatendee sawasawa na mapenzi..
Kwakuwa Ufalme ni wako Nguvu na Utukufu hata Milele..
Amina..!!

Wapendwa katika Kristo Yesu asanteni sana kwakuwa nami
Mungu aendelee kuwabariki na msipungukiwe katika mahitaji yenu
Baba wa Mbinguni akawape kinachowafaa ..
Nawapenda.

Daudi akataliwa na Wafilisti

1Wafilisti walikusanya majeshi yao yote huko Afeka, na Waisraeli walipiga kambi kwenye chemchemi ya bonde la Yezreeli. 2Wakuu watano wa Wafilisti walipokuwa wakipita na vikosi vyao vya mamia na maelfu, Daudi naye akiwa na watu wake pamoja na Akishi walikuwa wanafuata upande wa nyuma wa jeshi hilo. 3Makamanda wa Wafilisti waliuliza, “Waebrania hawa wanafanya nini hapa?” Akishi akawajibu hao makamanda Wafilisti, “Huyu ni Daudi, mtumishi wa Shauli mfalme wa Israeli; naye amekuwa nami kwa muda mrefu: Miaka kadhaa. Na tangu alipokimbilia kwangu, sijampata na kosa lolote.”
4Lakini makamanda wa Wafilisti walimkasirikia sana Akishi, wakamwambia, “Mrudishe aende mahali ulikompa akae. Kamwe asiende pamoja nasi vitani, la sivyo wakati wa vita atageuka na kuwa adui yetu. Huoni kuwa mtu huyu atapata njia nzuri ya kupatana na bwana wake halafu kuwa adui yetu vitani? 5Je, huyu si Daudi yuleyule ambaye wanawake waliimba habari zake walipokuwa wakicheza,
‘Shauli ameua maelfu,
lakini Daudi ameua maelfu kumi.’”
6Akishi akamwita Daudi na kumwambia, “Naapa kwa Mwenyezi-Mungu aliye hai, kwamba umekuwa mwaminifu kwangu. Lingekuwa jambo jema kwangu twende wote vitani, kwa maana sijaona lolote baya kwako tangu siku ile ulipokuja kwangu hadi leo hii. Hata hivyo, wakuu hawajaridhika nawe. 7Hivyo sasa, rudi nyumbani. Nenda kwa amani ili usiwachukize wakuu wa Wafilisti.”
8Daudi akamwambia Akishi, “Lakini nimefanya nini? Kama unavyosema kuwa, hujaniona na kosa lolote tangu siku ile nilipoanza kukutumikia hadi leo, kwa nini nisiende kupigana na maadui za bwana wangu, mfalme?”
9Akishi akamwambia, “Najua kuwa huna lawama mbele yangu kama malaika wa Mungu. Hata hivyo, makamanda wa Wafilisti wamesema, ‘Kamwe asiende pamoja nasi vitani’. 10Sasa, wewe pamoja na watumishi wa bwana wako Shauli waliokuja pamoja nawe, kesho asubuhi na mapema, amkeni na kuondoka mara kunapopambazuka.”
11Hivyo, kesho yake asubuhi, Daudi pamoja na watu wake waliondoka kurudi katika nchi ya Wafilisti. Lakini hao Wafilisti wakaenda Yezreeli.


1Samweli29;1-11

Biblia Habari Njema kwa Watu Wote(BHN)

"Swahili Na Waswahili"Mbarikiwe.

No comments: