Swahili na Waswahili

Swahili na Waswahili
Waswahili na Mswahili Rachel Siwa...Pamoja Daima!!

Tuesday 2 January 2018

Kikombe Cha Asubuhi ;1Samueli12...




Shalom,Habari za Asubuhi,Hamjambo,Mmeamkaje?

Tumshukuru Mungu wetu katika yote..

Mungu wetu Baba yetu,Muumba wetu Muumba wa Mbingu na Nchi
Muumba wa vyote vilivyomo vinavyoonekana na visivyo onekana
Mungu wa Abrahamu,Isaka na Yakobo,Mungu mwenye nguvu
Mungu wa walio hai,Mungu mwenye huruma,Muweza wa yote
Hakuna kama wewe,Neema yako yatutosha..!!

Asante Mungu wetu kwa wema na fadhili zako kwetu
Asante kwa ulinzi wako kwetu wakati wote
Asante kwa pumzi/uzima,afya na kwakuwa tayari kwa majukumu yetu
Asante kwa kutuchagua tena na kutupa kibali cha kuendelea kuiona leo hii

Utukuzwe Baba wa Mbinguni,Usifiwe ee  Mungu wetu,Uabudiwe Jehovah
Uhimidiwe Yahweh,Mtendo yako ni makuu mno,Mtendo yako ni ya ajabu..
Sifa na Utukufu tunakurudishia Mungu wetu..!


Ukuu ni wako, ee Mwenyezi-Mungu, una nguvu, utukufu, ushindi na enzi. Vyote vilivyoko mbinguni na duniani ni vyako. Ee Mwenyezi-Mungu, ufalme ni wako, nawe umetukuzwa, u mkuu juu ya vitu vyote. Utajiri na heshima hutoka kwako, vyote wavitawala. Uwezo na nguvu vimo mkononi mwako, nawe wawakuza uwapendao, na huwaimarisha wote. Sasa ee Mungu wetu, tunakushukuru na kulisifu jina lako tukufu. “Lakini, mimi ni nani, na watu wangu ni nani, hata tuweze kukupa kitu? Kwa maana vitu vyote vyatoka kwako, tumekutolea vilivyo vyako wewe mwenyewe.

Baba wa Mbinguni tunakuja mbele zako tukijinyenyekeza,tukijishusha na kujiachilia mikononi mwako
Yahweh tunaomba utusamehe makosa yetu tuliyoyafanya
kwakuwaza,kwakunena,kwakutenda,kwakujua/kutojua
Jehovah nasi tunaomba utupe neema ya kuweza kuwasamehe
wale wote waliotukosea..
Mungu wetu tunaomba utuepushe katika majaribu Baba wa Mbinguni
tunaomba utuokoe na yule mwovu na Kazi zake zote...
Yahweh tunaomba ututakase miili yetu na akili zetu Jehovah
utufunike kwa Damu ya Bwana na Mwokozi wetu Yesu Kristo wa Nazareti
Yeye aliteseka kwanza ili sisi tupate kupona..

Ziko habari za kuaminika kwamba kuna uzinzi miongoni mwenu; tena ni uzinzi mbaya ambao haujapata kuwako hata kati ya watu wasiomjua Mungu. Nimeambiwa eti mmoja wenu anaishi na mke wa baba yake! Mnawezaje kujivuna? Ingekuwa afadhali kwenu kuomboleza, na huyo aliyefanya kitu hicho aondolewe miongoni mwenu. Nami, kwa upande wangu, ingawa kwa mwili niko mbali nanyi, hata hivyo kwa roho niko hapo pamoja nanyi: Na hivyo, kama vile nipo hapo, nimekwisha mhukumu huyo aliyefanya jambo hilo la aibu. Wakati mnapokusanyika pamoja kwa jina la Bwana Yesu, nami nikiwa pamoja nanyi kwa roho, basi, kwa uwezo wa Bwana wetu Yesu, mkabidhini mtu huyo kwa Shetani ili mwili wake uharibiwe na roho yake iweze kuokolewa siku ile ya Bwana. Majivuno yenu hayafai! Je, hamjui kwamba chachu kidogo huchachusha donge lote la unga? Jitakaseni, mkatupe mbali chachu ya kale ili mpate kuwa donge jipya lisilotiwa chachu kama mnavyopaswa kuwa; maana, Kristo, Pasaka yetu, amekwisha tolewa kuwa sadaka. Basi, tufanye karamu hiyo si kwa chachu ile ya kale, chachu ya ubaya na uovu, bali kwa mkate usiotiwa chachu, mkate wa usafi na kweli. Niliwaandikia katika barua yangu msishirikiane na wazinzi. Ukweli ni kwamba sikuwa na maana ya watu wote duniani walio wazinzi, wachoyo, walaghai na wenye kuabudu sanamu. Maana, ili kuwaepa hao wote ingewalazimu nyinyi kuihama dunia hii kabisa! Nilichoandika ni hiki: Msishirikiane na ndugu Mkristo aliye mzinzi, mchoyo, mwenye kuabudu sanamu, mchongezi, mlevi na mlaghai. Mtu wa namna hiyo, hata kula msile naye. Je, ni shauri langu kuwahukumu watu walio nje? Hao Mungu atawahukumu. Je, nyinyi hampaswi kuwahukumu wale walio katika jamii yenu nyinyi wenyewe? Mfukuzeni mbali nanyi huyo mwovu!

Baba wa Mbinguni tunaomba ukabariki kazi za kimono yetu
Mungu wetu tunaomba ukatupe ubunifu na maarifa katika
Ufanyaji/utendaji Jehovah nasi tukatende sawasawa na mapenzi yako
Mungu wetu tunaomba ukabariki ridhiki zetu ziingiazo/zitokazo
Yahweh nasi tunaomba utupe neema ya kuweza kuwabariki wenye kuhitaji
Tusipungukiwe katika mahitaji yetu Yahweh ukatupe sawasawa na mapenzi yako....


Mfalme wa amani tunaomba amani yako ikatawale katika 
Maisha yetu,Baba wa Mbinguni tunaomba ukabariki nyumba/ndoa
zetu,watoto,wazazi/walezi wetu,familia/ndugu na wote wanaotuzunguka
Baba wa Mbinguni tunaomba ulinzi wako kwetu na kwa vyote 
tunavyovimiliki..
Yahweh tunaomba ukatuguse kwa mKono wako Wenye nguvu
Mungu wetu tukawe salama rohoni,Baba wa Mbinguni tunaomba
ukatamalaki na kutuatamia,Mungu wetu tunaomba utupe neema
ya kufuata njia zako Jehovah tukasimamie Neno lako amri na sheria
zako siku zote za maisha yetu..
Mfalme wa amani ukatupe macho ya rohoni Baba wa Mbinguni
ukatupe masikio ya kusikia sauti yako na kuitii..
Yahweh  sema  nasi Baba wa Mbinguni ukaonekane popote tupitapo
na ikajulikane kwamba upo Mungu wetu..
Yahweh Nuru yako ikaangaze Katika Maisha yetu,furaha,amani,
utu wema,fadhili,mafanikio,ushindi na vyote vinavyokupendeza
wewe visipungue..
Baba wa Mbinguni utuepushe na kiburi,majivuno,ubinafsi,choyo,makwazo,
unafiki, masengenyo na yote yanayokwenda kinyume nawe..
Mungu wetu ukatufanye barua njema nasi tukasomeke kama inavyokupendeza wewe..
Roho Mtakatifu akatuongoze katika yote na tukawe na kiasi..


Kisha mfalme Daudi akaingia ndani ya hema na kuketi mbele ya Mwenyezi-Mungu, halafu akaomba, “Mimi ni nani, ee Mwenyezi-Mungu, na nyumba yangu ni nini hata unitukuze hivi? Isitoshe, umenifanyia mengine zaidi: Umenitolea ahadi juu ya vizazi vyangu vijavyo ee Mwenyezi-Mungu! Nikuambie nini zaidi, mimi Daudi mtumishi wako, kwa kunitukuza hivyo? Wewe unanijua mimi mtumishi wako. Ee Mwenyezi-Mungu, kwa ajili ya mtumishi wako na kwa kufuatana na moyo wako mwenyewe, umeyatenda hayo makuu yote, ili yajulikane hayo matendo makuu yote. Hakuna mwingine kama wewe, ee Mwenyezi-Mungu, na yote tunayoyasikia yanathibitisha kwamba hakuna Mungu mwingine ila wewe. Tena ni watu gani duniani ambao wanaweza kulinganishwa na watu wako wa Israeli ambao peke yao Mungu wao alikwenda kuwakomboa ili wawe watu wake? Wewe ulijifanyia jina kwa kutenda mambo makubwa na ya ajabu hapo ulipoyafukuza mataifa mbele ya watu wako ambao uliwakomboa kutoka Misri. Hata umejifanyia watu wako wa Israeli kuwa watu wako milele; nawe ee Mwenyezi-Mungu, umekuwa Mungu wao. “Basi sasa, ewe Mwenyezi-Mungu, liimarishe milele neno lako ulilosema kunihusu mimi mtumishi wako na kuhusu jamaa yangu. Nalo jina lako litatukuzwa milele, nao watu watasema, ‘Mwenyezi-Mungu wa majeshi, Mungu wa Israeli, ndiye Mungu wa Israeli!’ Na jamaa yangu, mimi Daudi mtumishi wako, itaimarika mbele yako. Maana ee Mungu wangu nimepata ujasiri kukuomba kwa sababu wewe, umenifunulia ukisema ya kwamba utanijengea nyumba. Sasa ee Mwenyezi-Mungu, wewe ndiwe Mungu, umeniahidi mimi mtumishi wako jambo hili jema; kwa hiyo nakuomba uibariki nyumba yangu, mimi mtumishi wako, ili idumu milele mbele yako; kwani unachobariki wewe, huwa kimebarikiwa milele.”
Yahweh tunaomba ukawaguse kwa mkono wako wenye nguvu
wenye shida/tabu
Mungu wetu tunaomba uponyaji kwa wagonjwa na ukawape uvumilivu wanaowauguza..
Jehovah tunaomba ukawavushe salama wale wanaopitia magumu/majaribu mbalimbali..
Baba wa Mbinguni tunaomba ukawaweke huru wale walio katika vifungo
vya yule mwovu, Mungu wetu haki ikatendeke kwa walio magerezani
pasipo na hatia..
Yahweh ukawe tumaini kwa waliokata tamaa,walio kataliwa,wenye hofu na mashaka..
Mungu wetu tunaomba ukawe mfariji wa wafiwa na ukawaponye
wote  walio umizwa roho..
Baba wa Mbinguni tunaomba ukawasamehe wale wote waliokwenda
kinyume nawe...
Jehovah ukawe msaada na ukawape chakula wenye njaa..
Baba wa Mbinguni tuyaweka haya mikononi mwako
Tukiamini wewe ni Mungu wetu hakuna lililogumu kwako
Kwakuwa Ufalme ni wako Nguvu na Utukufu hata Milele..
Amina..!!

Asanteni sana wapendwa/waungwana kwakuwa nami
Mungu Baba aendelee kuwabariki na msipungukiwe katika
mahitaji yenu..
Baba wa Mbinguni akawape sawasawa na mapezni yake
Nawapenda.



Samueli anawahutubia Waisraeli

1Samueli akawaambia Waisraeli wote, “Yote mliyoniambia, nimeyasikiliza. Nimemtawaza mfalme juu yenu. 2Sasa, mnaye mfalme wa kuwaongoza. Kwa upande wangu, mimi ni mzee mwenye mvi, na watoto wangu wa kiume wako pamoja nanyi. Nimekuwa kiongozi wenu tangu nilipokuwa kijana mpaka sasa. 3Niko hapa, na kama nimefanya tendo lolote lile baya, basi, toeni ushahidi mbele ya Mwenyezi-Mungu na mbele ya mfalme wake mteule. Je, nimepora fahali au punda wa mtu yeyote? Je, nimempunja mtu yeyote? Je, nimemkandamiza mtu yeyote? Je, nimepokea rushwa kwa mtu yeyote ili kupotosha haki? Nami nitamrudishia chochote kile.” 4Watu wakamjibu, “Kamwe hujatudanganya, hujatukandamiza, wala hujachukua kitu chochote kwa mtu.” 5Samueli akajibu, “Mwenyezi-Mungu ni shahidi juu yenu, na mfalme wake mteule leo ni shahidi kuwa mmeniona sina hatia.” Wao wakajibu: “Yeye ni shahidi.” 6Samueli akawaambia, “Mwenyezi-Mungu ndiye aliyemteua Mose na Aroni na kuwatoa babu zenu nchini Misri. 7Sasa simameni papo hapo mlipo ili mimi na nyinyi tuhukumiwe mbele ya Mwenyezi-Mungu, nami nitawahutubia kuhusu matendo yake ya ajabu ambayo aliyatenda ili kuwaokoa nyinyi na babu zenu.
8“Yakobo na jamaa yake walipokwenda Misri, na Wamisri walipowakandamiza, babu zenu walimlilia Mwenyezi-Mungu; naye akawatuma Mose na Aroni ambao waliwatoa babu zenu nchini Misri na kuwafanya mkae katika nchi hii. 9Lakini wao walimsahau Mwenyezi-Mungu, Mungu wao, naye akawatia mikononi mwa Sisera, kamanda wa jeshi la Hazori, na mikononi mwa Wafilisti na mikononi mwa mfalme wa Moabu. Mataifa hayo yalipigana na babu zenu na kuwashinda. 10Babu zenu wakamlilia Mwenyezi-Mungu, wakisema, ‘Tumefanya dhambi kwa sababu tumekuacha wewe Mwenyezi-Mungu, kwa kutumikia Mabaali na Maashtarothi. Tuokoe kutoka mikononi mwa adui zetu, nasi tutakutumikia’. 11Ndipo Mwenyezi-Mungu alipomtuma Yerubaali, na baadaye akamtuma Bedani,12:11 Bedani: Au Baraka. kisha Yeftha, na mwishowe akanituma mimi Samueli. Kila mmoja wetu aliwaokoa kutoka kwa adui zenu waliowazunguka, nanyi mkaishi kwa amani. 12Lakini mlipomwona mfalme Nahashi wa Waamoni amekuja kuwashambulia, mkamkataa Mwenyezi-Mungu ambaye ndiye Mfalme wenu, mkaniambia, ‘La! Mfalme ndiye atakayetutawala.’ 13Sasa, mfalme mliyejichagulia ndiye huyu hapa. Mlimwomba Mwenyezi-Mungu awape mfalme, naye amewapa. 14Kama mkimcha Mwenyezi-Mungu, na kumtumikia, na kusikiliza sauti yake bila kuiasi amri yake, kama nyinyi wenyewe pamoja na mfalme anayewatawala mkimfuata Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu, basi mtafanikiwa. 15Lakini kama hamtasikiliza sauti ya Mwenyezi-Mungu, mkaasi amri yake, basi yeye atapambana nanyi pamoja na mfalme wenu.12:15 mfalme wenu: Makala ya Kiebrania: Baba zenu. 16Kwa hiyo basi, tulieni na kulitazama jambo hilo kubwa ambalo Mwenyezi-Mungu atatenda mbele yenu. 17Je, sasa si wakati wa kuvuna ngano? Lakini mimi nitamwomba Mwenyezi-Mungu alete radi na mvua, nanyi mtatambua na kuona kuwa uovu wenu mliotenda mbele ya Mwenyezi-Mungu kwa kujitakia mfalme, ni mkubwa.”
18Basi, Samueli akamwomba Mwenyezi-Mungu, naye akatuma radi na mvua katika siku hiyo. Watu wote wakamwogopa sana Mwenyezi-Mungu na Samueli. 19Hivyo wakamwambia Samueli, “Tafadhali utuombee sisi watumishi wako kwa Mwenyezi-Mungu, Mungu wako, ili tusife; kwa sababu tumezidisha dhambi zetu kwa uovu huo wa kujitakia mfalme.”
20Samueli akawajibu, “Msiogope; ingawa mmefanya uovu huu, msiache kumfuata Mwenyezi-Mungu, ila mtumikieni kwa moyo wenu wote. 21Msiifuate miungu ya uongo isiyo na faida wala haiwezi kuwaokoa, maana ni ya uongo. 22Kwa heshima ya jina lake kuu, Mwenyezi-Mungu hatawatupa watu wake kwa sababu amependa kuwafanya nyinyi muwe watu wake. 23Tena kwa upande wangu haitatokea niache kuwaombea kwa Mwenyezi-Mungu; kufanya hivyo itakuwa kumkosea Mwenyezi-Mungu. Nitaendelea kuwafundisha njia njema na ya haki. 24Basi, nyinyi mcheni Mwenyezi-Mungu na kumtumikia kwa uaminifu kwa moyo wenu wote. Kumbukeni yale mambo makuu aliyowatendea. 25Lakini kama mkiendelea kutenda maovu, mtaangamia nyinyi wenyewe pamoja na mfalme wenu.”


1Samweli12;1-25

Biblia Habari Njema kwa Watu Wote(BHN)

"Swahili Na Waswahili"Mbarikiwe.

No comments: