Swahili na Waswahili

Swahili na Waswahili
Waswahili na Mswahili Rachel Siwa...Pamoja Daima!!

Tuesday 12 December 2017

Kikombe Cha Asubuhi ;Tumemaliza kitabu cha Waamuzi-Tunaanza Kitabu cha Ruthu Mungu yu mwema...



Shalom,Habari za Asubuhi,Hamjambo,Mmeamkaje?

Mungu wetu yu mwema sana,Tunamshukuru Mungu kwakumaliza
kitabu cha "Waamuzi"na Leo tunaanza Kitabu cha "Ruthu"
Mungu akatupe kibali cha kusoma na kuelewa,akatupe macho
ya rohoni,tusomapo tukapate kuelewa na kujifunza zaidi,ikawe
faida kwetu na kwa wengine,Tukawe na kiu,shahuku ya kujifunza
zaidi..Ee Mungu wetu utusaidie...!!

Yesu alianza kufundisha tena akiwa kando ya ziwa. Umati mkubwa wa watu ulimzunguka hata ikambidi aingie katika mashua na kuketi. Watu wote wakawa wamekaa katika nchi kavu, kando ya ziwa. Aliwafundisha mambo mengi kwa mifano, na katika mafundisho yake aliwaambia, “Sikilizeni! Mpanzi alikwenda kupanda mbegu. Alipokuwa akipanda mbegu, nyingine zilianguka njiani, ndege wakaja wakazila. Nyingine zilianguka penye mawe pasipokuwa na udongo mwingi, zikaota mara kwa kuwa udongo haukuwa na kina. Jua lilipochomoza, zikateketea; na kwa kuwa mizizi yake haikuwa na nguvu, zikanyauka. Nyingine zilianguka kwenye miti ya miiba, nayo ikakua na kuzisonga, nazo hazikuzaa nafaka. Nyingine zilianguka katika udongo mzuri, zikamea, zikakua na kuzaa: Moja punje thelathini, moja sitini na nyingine mia.”
Asante Baba wa Mbinguni kwa wema na fadhili zako kwetu..
Asante kwa ulinzi wako kwetu wakati wote..
Asante kwa uzima/pumzi,afya na kuwa tayari kwa majukumu yetu..
Asante kwakutuchagua tena na kutupa kibali cha kuendelea kuiona Leo hii
Utukuzwe Ee-Mwenyezi Mungu..!Unifundishe masharti yako..
Utukuzwe Ee Mwenyezi-Mungu..!kwa sababu ya nguvu yako tutaimba
na kuusifu uwezo wako..
Utukuzwe Ee Mwenyezi-Mungu..!juu ya Mbingu  Utukufu wako uenee duniani kote..
Utukuzwe Ee Mwenyezi-Mungu...!Milele na Milele..!
Mungu wetu Baba yetu,Mungu wa Abrahamu,Isaka na Yakobo..!
Unatosha Baba wa Mbinguni,Hakuna kama wewe..!


Watu wa Israeli walipotoka Misri, wazawa wa Yakobo walipotoka ugenini, Yuda ikawa maskani ya Mungu, Israeli ikawa milki yake. Bahari iliona hayo ikakimbia; mto Yordani ukaacha kutiririka! Milima ilirukaruka kama kondoo dume; vilima vikaruka kama wanakondoo! Ee bahari, imekuwaje hata ukakimbia? Nawe Yordani, kwa nini ukaacha kutiririka? Enyi milima, mbona mliruka kama kondoo dume? Nanyi vilima, mmerukaje kama wanakondoo? Tetemeka, ee dunia mbele yake Mwenyezi-Mungu; tetemeka mbele ya Mungu wa Yakobo, anayeugusa mwamba ukawa bwawa la maji, nayo majabali yakawa chemchemi za maji!
Baba wa Mbinguni tunakuja mbele zako tukijinyenyekeza,tukijishusha
na kujiachilia mikononi mwako ...
Mungu wetu tunaomba utusamehe Dhambi zetu zote tulizozifanya kwakuwaza,kwakunena,kwakutenda,kwakujua/kutojua..
Jehovah nasi tunaomba utupe neema ya kuweza kuwasamehe wale wote waliotukosea..
Mungu wetu tunaomba utuepushe katika majaribu Yahweh tunaomba utuokoe na yule mwovu na kazi zake zote..
Baba wa Mbinguni tunaomba ututakase miili yetu na akili zetu Jehovah
tunaomba utufunike kwa Damu ya Bwana na Mwokozi wetu Yesu Kristo
wa Nazareti yeye aliteseka kwanza ili sisi tupate kupona..

“Kama Mwenyezi-Mungu asingalikuwa upande wetu Semeni nyote mlio katika Israeli: “Kama Mwenyezi-Mungu asingalikuwa upande wetu, wakati ule tuliposhambuliwa na maadui, hakika tungalimezwa tukiwa hai, wakati hasira zao zilipotuwakia. Tungalikumbwa na gharika, tungalifunikwa na mto wa maji, mkondo wa maji ungalituchukua!” Atukuzwe Mwenyezi-Mungu, ambaye hakutuacha makuchani mwao. Tumeponyoka kama ndege mtegoni; mtego umeteguliwa, nasi tukaokoka. Msaada wetu watoka kwa Mwenyezi-Mungu, aliyeumba mbingu na dunia.
Mungu wetu tunaomba ukabariki kazi za mikono yetu Jehovah tunaomba
ukatupe ubunifu na maarifa katika ufanyaji/utendaji Baba tukatende
sawasawa na mapenzi yako..
Yahweh tunaomba ukabariki ridhiki zetu ziingiazo/zitokazo Mungu wetu
nasi tunaomba utupe neema ya kuweza kuwabariki wenye kuhitaji..
Baba wa Mbinguni tusipungukiwe katika mahitaji yetu Yahweh ukatupe
kama inavyokupendeza wewe..

Mafalme wa Amani tunayaweka maisha yetu mikononi mwako Jehovah
tunaomba ukabariki nyumba/ndoa zetu,watoto,wazazi wetu,familia/ndugu na wote wanaotuzunguka..
Mungu wetu tunaomba ulinzi wako kwetu na kwa vyote tunavyovimiliki
Yahweh ukatamalaki na kutuatamia,Mungu wetu ukatuguse kwa mkono
wako wenye nguvu Baba wa Mbinguni tukapate kutambua/kujitambua
Yahweh ukatupe neema ya kufuata njia zako,Kusimamia Neno lako
amri na sheria zako siku zote za maisha yetu..
Baba wa Mbinguni ukatupe macho ya kuona, masikio ya kusikia
sauti yako na kuitii,Yahweh ukatubariki tuingiapo/tutokapo..
Mungu wetu ukaonekane katika maisha yetu,popote tupitapo
na ijulikane kwamba upo Baba wa Mbinguni..
Ukatufanye chombo chema Baba wa mbinguni nasi tukatumike kama
inavyokupendeza wewe..
Roho Mtakatifu akatuongoze katika yote na tukawe na kiasi..



Nilifurahi waliponiambia: “Twende nyumbani kwa Mwenyezi-Mungu.” Sasa tuko tumesimama, kwenye malango yako, ee Yerusalemu! Yerusalemu, mji uliojengwa, ili jumuiya ikutane humo. Humo ndimo makabila yanamofika, naam, makabila ya Israeli, kumshukuru Mwenyezi-Mungu kama alivyoagiza. Humo mmewekwa mahakama ya hukumu ya haki, mahakama ya ukoo wa kifalme wa Daudi. Uombeeni Yerusalemu amani: “Wote wakupendao na wafanikiwe! Ndani ya kuta zako kuwe na amani, majumbani mwako kuweko usalama!” Kwa ajili ya jamaa na ndugu zangu, ee Yerusalemu, nakutakia amani! Kwa ajili ya nyumba ya Mwenyezi-Mungu, Mungu wetu, ninakuombea upate fanaka!

Mungu wetu tunaomba ukawaguse kwa mkono wako wenye nguvu wote wasumbakao na kuelemewa na mizigo,Mungu wetu tunaomba uponyaji kwa wagonjwa Yahweh ukawape nguvuna uvumilivu wanaowauguza...
Yahweh tunaomba ukabariki mashamba/kazi Mungu wetu ukawape chakula cha kutosha na kuweka akiba  wenye njaa..
Baba wa mbinguni utaomba ukawaweke huru wale walio katika vifungo
vya yule mwovu,Mungu wetu haki ikatendeke kwa wote waliovifungoni
pasipo na hatia,Baba wa Mbinguni ukawasimamishe na kuwarudisha
wale wote walioanguka/potea Baba ukawasamehe wale wote waliokwenda
kinyume nawe,Mungu wetu ukawafariji wafiwa,Mfalme wa amani
ukatawale,ukabariki,ukasikie,ukapokee,ukajibu sala/maombi yetu
Mungu wetu ukawatendee sawasawa na mapenzi yako..
Sifa na Utukufu tunakurudishia Mungu Baba..
Kwakuwa Ufalme ni wako Nguvu na Utukiufu hata Milele....
Amina..!

Asanteni sana wapendwa katika Bwana kwakuwa nami..
Pendo lenu likadumu,Amani ikatawale maishani mwenu,Nuru ikaangaaze
katika nyumba zetu,Damu ya Bwana wetu Yesu Kristo ikawafunike..
Nawapenda.

Elimeleki na jamaa yake wanakwenda Moabu

1Hapo zamani, wakati waamuzi walipokuwa wanatawala Israeli, palitokea njaa nchini humo. Mtu mmoja kutoka Bethlehemu katika Yuda pamoja na mkewe na watoto wao wa kiume wawili walikwenda kuishi kwa muda nchini Moabu ili kuishi kama wageni. 2Mtu huyo aliitwa Elimeleki na mkewe aliitwa Naomi. Watoto wao wawili wa kiume, mmoja aliitwa Mahloni na mwingine Kilioni. Mtu huyo na jamaa yake walikuwa Waefrathi wa huko Bethlehemu katika Yuda. Walikwenda nchini Moabu, wakakaa huko. 3Lakini Elimeleki, mumewe Naomi, alifariki na Naomi akaachwa na wanawe wawili. 4Vijana hao walioa wasichana wa Kimoabu, Orpa na Ruthu. Baada ya miaka kumi hivi, 5Mahloni na Kilioni nao pia walifariki.

Naomi na Ruthu wanarudi Bethlehemu

6Baadaye, Naomi alipata habari kwamba Mwenyezi-Mungu alikuwa amewabariki watu wake kwa kuwapa chakula. Basi, akaondoka kutoka Moabu kurudi kwao pamoja na wakwe zake. 7Akaondoka mahali pale alipoishi pamoja na wakwe zake, wakashika njia ya kurudi Yuda. 8Naye Naomi akawaambia hao wakwe zake wawili, “Rudini kila mmoja nyumbani kwa mama yake. Naomba Mwenyezi-Mungu awe mwema kwenu kama mlivyokuwa wema kwangu na kwa wale watu wangu waliofariki. 9Mwenyezi-Mungu awajalie, kila mmoja wenu apate mume na nyumba yake.” Kisha Naomi akawaaga kwa kuwabusu. Lakini wao walianza kulia kwa sauti 10na kumwambia, “La hasha! Tutakwenda pamoja nawe kwa watu wako.”
11Naye Naomi akawasihi, “Rudini, binti zangu. Kwa nini kunifuata? Je, mnafikiri naweza kupata tena watoto watakaokuwa waume zenu? 12Rudini nyumbani kwenu binti zangu, kwa maana mimi ni mzee mno, siwezi kuolewa tena. Hata kama ningesema ninalo tumaini, na hata kama ningepata mume usiku huu na kupata watoto, 13je, mngeweza kungoja mpaka wakue? Je, mngeweza kujizuia msiolewe na waume wengine? Sivyo, binti zangu! Mambo yangu ni magumu mno kwa ajili yenu, maana Mwenyezi-Mungu amenipiga kipigo.”
14Hapo walipaza sauti wakaanza kulia tena. Ndipo Orpa akamkumbatia mkwewe, akamuaga na kurudi nyumbani; lakini Ruthu, akaandamana naye. 15Basi Naomi akamwambia, “Ruthu, tazama dada yako amerudi nyumbani kwake na kwa mungu wake; basi, nawe pia urudi, umfuate dada yako.”
16Lakini Ruthu akamjibu,
“Usinisihi nikuache wewe,
wala usinizuie kufuatana nawe.
Kokote utakakokwenda ndiko nami nitakakokwenda,
na ukaapo nitakaa,
watu wako watakuwa watu wangu,
na Mungu wako atakuwa Mungu wangu.
17Pale utakapofia hapo nitakufa nami,
na papo hapo nitazikwa;
Mwenyezi-Mungu anipe adhabu kali kama nikitenganishwa nawe
isipokuwa tu kwa kifo.”
18Naomi alipoona kuwa Ruthu ameamua kwenda pamoja naye, aliacha kumshawishi. 19Ndipo wote wawili wakaendelea na safari hadi Bethlehemu. Walipofika huko, watu wote walishangaa, hata wanawake wakaulizana, “Je, huyu ni Naomi?”
20Naomi akasema, “Msiniite tena Naomi1:20 Naomi: Maana yake: Mwema. niiteni Mara,1:20 Mara: Maana yake: Mwenye uchungu. kwa maana Mungu mwenye nguvu ameyafanya maisha yangu yawe machungu mno. 21Nilipoondoka hapa, nilikuwa na vitu vingi, lakini sasa Mwenyezi-Mungu amenirudisha mikono mitupu. Mbona mwaniita Naomi na hali Mwenyezi-Mungu ameniadhibu, naye Mungu Mwenye Nguvu amenitesa.”
22Hivyo ndivyo Naomi pamoja na Ruthu Mmoabu, mkwewe, walivyorejea kutoka Moabu, na kuwasili Bethlehemu wakati uvunaji wa shayiri ulipokuwa unaanza.


Ruthu1;1-22

Biblia Habari Njema kwa Watu Wote(BHN)

"Swahili Na Waswahili"Mbarikiwe.

No comments: