Swahili na Waswahili

Swahili na Waswahili
Waswahili na Mswahili Rachel Siwa...Pamoja Daima!!

Tuesday 12 September 2017

Kikombe Cha Asubuhi Kumbukumbu la Sheria 15 (Kumbukumbu la Torati katika tafsiri nyingine)



Shalom,Habari za Asubuhi,Hamjambo,Mmeamkaje?

Haleluyah..! ni siku nyingine tena Mungu ametuchagua na kutupa kibali cha kuendelea kuiona leo hii..

Asante Mungu wetu kwa wema na fadhili zako kwetu..
Asante kwa ulinzi wako wakati wote..
Asante kwa Neema hii ya pumzi na uzima..

Kisha Yesu akawaambia wanafunzi wake, “Kwa sababu hiyo nawaambieni, msiwe na wasiwasi juu ya chakula mnachohitaji ili kuishi, wala juu ya mavazi mnayohitaji kwa ajili ya miili yenu. Kwa sababu uzima ni bora kuliko chakula, na mwili ni bora kuliko mavazi. Chukueni kwa mfano, kunguru: Hawapandi, hawavuni wala hawana ghala yoyote. Hata hivyo, Mungu huwalisha. Nyinyi mna thamani zaidi kuliko ndege! Ni nani kati yenu kwa kuwa na wasiwasi sana anaweza kuongeza kidogo urefu wa maisha yake? Basi, kama hamwezi kufanya jambo dogo kama hilo, kwa nini kuwa na wasiwasi juu ya yale mengine? Angalieni maua jinsi yanavyomea. Hayafanyi kazi wala hayafumi. Lakini nawaambieni, hata Solomoni mwenyewe na fahari zake zote hakupata kuvikwa vizuri kama ua mojawapo. Ikiwa basi, Mungu hulivika hivyo jani la shambani ambalo leo liko na kesho latupwa motoni, je, si atawafanyia nyinyi zaidi? Enyi watu wenye imani haba! “Basi, msivurugike akili, mkihangaika juu ya mtakachokula au mtakachokunywa. Kwa maana hayo yote yanahangaikiwa na watu wote wasiomjua Mungu. Baba yenu anajua kwamba mnahitaji vitu hivyo. Shughulikeni kwanza juu ya ufalme wa Mungu, na hayo mtapewa kwa ziada.


Utukuzwe Mungu wetu,Uhimidiwe Baba wa Mbinguni..
Unatosha Mungu wetu,Mungu wa Abrahamu,Isaka na Yakobo..
Muweza wa yote,wewe ni mwanzo na mwisho,Alfa na Omega..
Unastahili sifa,Unastahili kuabudiwa,Hakuna kama wewe....

Jehovah tunakuja mbele zako tukinyenyekeza,tukijishusha na kujiachilia mikononi mwako..
Mungu wetu tunaomba utusamehe dhambi zetu zote tulizozifanya..
kwakuwaza,kwakunena,kwakutenda,kwakujua/kutojua..
Baba wa rehema tunaomba nasi utupe neema ya kuweza kuwasamehe wale wote waliotukosea..
Yahweh utuepushe katika majaribu Baba wa Mbinguni utuokoe na yule mwovu na kazi zake zote..
Baba wa Mbinguni tunaomba ututakase miili yetu na akili zetu na utufunike kwa Damu ya Bwana wetu Yesu Kristo wa Nazareti..

Mfalme wa Amani tunaomba utubariki na ukabariki kazi za mikono yetu..
Ukabariki ridhiki zetu ziingiazo/zitokazo nasi ukatupe neema ya kuwabariki wenye kuhitaji..
Tusipungukiwe katika mahitaji yetu Jehovah ukatupe kama inavyokupendeza wewe..


“Msiogope, enyi kundi dogo! Maana Baba yenu amependa kuwapeni ufalme. Uzeni mali yenu mkawape maskini hizo fedha. Jifanyieni mifuko isiyochakaa, na kujiwekea hazina mbinguni ambako haitapungua. Huko wezi hawakaribii, wala nondo hawaharibu. Pale ilipo hazina yako, ndipo pia utakapokuwa moyo wako.



Baba wa Mbninguni tunaomba ukabariki,ukavitakase na kuvifunika kwa Damu ya Bwana wetu Yesu Kristo vyote tunavyoenda kugusa/kutumia na vyote tunavyoenda kufanya/kutenda na tukatende kama ikupasavyo..

Yahweh tunayaweka maisha yetu mikononi mwako..
Nyumba/Ndoa zetu,watoto,wazazi/wazee wetu,familia/ndugu na wote wanaotuzunguka,Mungu wetu ukaonekane na kutubariki..
Ukatupe neema ya kusimamia Neno lako Amri na Sheria zako siku zote za maisha yetu..

“Muwe tayari mmejifunga mkanda kiunoni, na taa zenu ziwe zinawaka; muwe kama watumishi wanaomngojea bwana wao arudi kutoka harusini, ili wamfungulie mara atakapobisha. Heri yao watumishi wale ambao bwana wao atakaporudi atawakuta wanakesha! Nawaambieni hakika, huyo bwana atajifunga mkanda kiunoni, atawaketisha mezani na kuwahudumia. Hata kama atarudi usiku wa manane au alfajiri na kuwakuta wanakesha, heri yao watumishi hao! Jueni kwamba, kama mwenye nyumba angejua saa ambayo mwizi atakuja, angekesha, wala hangeiacha nyumba yake ivunjwe. Nanyi, kadhalika muwe tayari, maana Mwana wa Mtu atakuja saa msiyoitazamia.”

Ukatufanye chombo chema nasi tukatumike kama inavyokupendeza wewe...




Petro akamwambia, “Bwana, mfano huo ni kwa ajili yetu tu, au ni kwa ajili ya watu wote?” Bwana akajibu, “Ni nani, basi, aliye mtumishi mwaminifu na mwenye busara, ambaye bwana wake atamweka juu ya watumishi wake ili awape chakula wakati ufaao? Heri yake mtumishi huyo ikiwa bwana wake atakaporudi atamkuta akifanya hivyo. Hakika atampa madaraka juu ya mali yake yote. Lakini, kama mtumishi huyo akijisemea moyoni: ‘Bwana wangu amekawia sana kurudi;’ kisha akaanza kuwapiga watumishi wenzake, wa kiume au wa kike, na kula, kunywa na kulewa, bwana wake atarudi siku asiyoitazamia na saa asiyoijua; atamwadhibu mtumishi huyo vibaya na kumweka fungu moja na wasioamini. Mtumishi ambaye anajua matakwa ya bwana wake lakini hajiweki tayari kufanya anavyotakiwa, atapigwa sana. Lakini yule afanyaye yanayostahili adhabu bila kujua, atapigwa kidogo. Aliyepewa vingi atadaiwa vingi; aliyepewa vingi zaidi atadaiwa vingi zaidi.


Roho Mtakatifu akatuongoze katika yote na tukawe na kiasi..

Tazama wenye shida/tabu,wagonjwa,waliokata tamaa,waliokataliwa..
wanaopitia magumu/majaribu mbalimbali,waliokatika vifungo vya yule mwovu..
Mungu wetu ukawaguse kwa mkono wako wenye nguvu..
Ukawape uponyaji wa mwili na roho pia..
Ukawape neema ya kutambua/kujitambua na kusimamia Neno lako..
Na waweze kukuomba Mungu na ukuwaokoe katika mitego yote ..
Mungu wetu usikie kuomba kwao na ukawatendee kama inavyokupendeza wewe..
Sifa na Utukufu tunakurudishia Mungu wetu..
Kwakuwa Ufalme ni wako Nguvu na Utukufu hata Milele..
Amina..!
Asanteni sana wapendwa/waungwana kwa kuwa nami..
Mungu mwenye upendo aendelee kudumisha pendo lenu kwa watu wote..
Akawabariki na mkawabariki wengine..
Amani iwe nayi wakati wote..
Nawapenda.




Mwaka wa Sabato

(Lawi 25:1-7)

1“Kila mwisho wa mwaka wa saba mtawasamehe wadeni wenu wote. 2Hivi ndivyo mtakavyofanya: Kila mmoja aliyemkopesha jirani yake, alifute hilo deni, wala asijaribu kumdai kwa sababu Mwenyezi-Mungu mwenyewe ameamua deni hilo lifutwe. 3Mnaweza kuwadai wageni, lakini madeni yote ya ndugu zenu wenyewe mtayafuta.
4“Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu atawabariki katika nchi anayowapa iwe mali yenu. Hakuna hata mmoja atakayekuwa maskini kati yenu, 5mradi tu mumtii Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu, kwa kufuata kwa uangalifu amri ninazowapeni hivi leo. 6Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu, atawabariki kama vile alivyowaahidi. Nanyi mtayakopesha mataifa mengi, lakini nyinyi hamtakopa. Kadhalika mtatawala mataifa mengi, lakini mataifa hayo hayatawatawala nyinyi.
7“Kukiwa na maskini wa jamaa yenu katika miji ya nchi ambayo Mwenyezi-Mungu atawapa, msiwe wachoyo na wagumu kwake. 8Badala yake, fumbueni mikono yenu na kumkopesha kwa hiari kiasi cha kutosha mahitaji yake. 9Angalieni wazo ovu lisiwaingie mioyoni mwenu, mkasema: ‘Mwaka wa saba, mwaka wa kusamehe wadeni, uko karibu’; mkamfikiria ndugu yenu maskini kwa ukali na kukataa kumpa chochote; yeye aweza kumlilia Mwenyezi-Mungu dhidi yenu na hiyo ikawa dhambi kwenu. 10Mpeni ndugu maskini kwa ukarimu bila kunungunika; maana kwa ajili ya hayo, Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu atawabariki katika kazi zenu zote na katika kila mfanyalo. 11Maana maskini hawatakosekana nchini; hivyo nawaamuru, muwe wakarimu kwa ndugu zenu wahitaji na maskini nchini mwenu.

Jinsi ya kuwatendea watumwa

(Kut 2:1-11)
12“Kama nduguyo Mwebrania, mwanamume au mwanamke, akiuzwa kwako, atakutumikia kwa miaka sita, lakini katika mwaka wa saba, utamwacha huru. 13Nawe utakapomwacha huru, usimwache aende mikono mitupu. 14Mpe kwa ukarimu kile ambacho Mwenyezi-Mungu amekubariki: Kondoo, nafaka na divai. 15Kumbukeni kwamba nyinyi mlikuwa watumwa huko Misri na Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu, aliwakomboa; ndiyo maana leo nawaamuru hivyo. 16Lakini akikuambia, ‘Sitaondoka kwako,’ kwa sababu anakupenda wewe na jamaa yako na anaridhika kuishi nawe, 17basi, utachukua shazia na kutoboa sikio lake mpaka hiyo shazia iingie mlangoni naye atakuwa mtumwa wako milele. Kadhalika mtendee vivyo hivyo mtumwa wako wa kike. 18Wala usione ugumu utakapomwacha huru mtumwa wako, maana, amekutumikia kwa muda wa miaka sita kwa nusu ya ujira wa mtumishi wa kuajiri. Fanya hivyo, naye Mwenyezi-Mungu, Mungu wako atakubariki kwa kila utakalofanya.

Wazaliwa wa kwanza wa ng'ombe na kondoo

19“Mtolee Mwenyezi-Mungu, Mungu wako, wazaliwa wote wa kwanza wa kiume wa kundi lako la ng'ombe na kondoo. Usiwafanyize kazi ng'ombe hao na kondoo hao usiwakate manyoya. 20Kila mwaka, wewe na jamaa yako mtakula wanyama hao mbele ya Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu, mahali Mwenyezi-Mungu atakapochagua. 21Lakini mnyama huyo akiwa na dosari yoyote, yaani akiwa kilema au kipofu, au ana kasoro yoyote kubwa, usimtoe kuwa sadaka kwa Mwenyezi-Mungu, Mungu wako. 22Utamla mnyama wa namna hiyo ukiwa katika mji wako; pia wote walio safi na wasio safi wanaweza kumla kama unavyokula paa au kulungu. 23Lakini usile damu yake; bali hiyo utaimwaga chini kama maji.



Kumbukumbu la Sheria 15:1-23

Biblia Habari Njema kwa Watu Wote(BHN)

"Swahili Na Waswahili"Mbarikiwe.

No comments: