Swahili na Waswahili

Swahili na Waswahili
Waswahili na Mswahili Rachel Siwa...Pamoja Daima!!

Monday 11 September 2017

Kikombe Cha Asubuhi Kumbukumbu la Sheria 14 (Kumbukumbu la Torati katika tafsiri nyingine)



Shalom,Habari za Asubuhi,Hamjambo,Mmeamkaje?

Ni siku nyingine tena Mungu wetu ametuchagua na 
ametupa kibali cha kuendelea kuiona leo hii..
Si kwamba sisi tumetenda mema sana,
si kwa nguvu zetu au akili zetu..
Hapana ni kwa neema na rehema zake Mungu wetu sisi kuwa hivi tulivyo...


Hapo mwanzo, Neno alikuwako; naye alikuwa na Mungu, naye alikuwa Mungu. Tangu mwanzo Neno alikuwa na Mungu. Kwa njia yake vitu vyote viliumbwa; hakuna hata kiumbe kimoja kilichoumbwa pasipo yeye. Yeye alikuwa chanzo cha uhai na uhai huo ulikuwa mwanga wa watu. Na mwanga huo huangaza gizani, nalo giza halikuweza kuushinda. Mungu alimtuma mtu mmoja jina lake Yohane, ambaye alikuja kuwaambia watu juu ya huo mwanga. Alikuja ili kwa ujumbe wake watu wote wapate kuamini. Yeye hakuwa huo mwanga, ila alikuja tu kuwaambia watu juu ya huo mwanga. Huu ndio mwanga halisi, mwanga unaokuja ulimwenguni, na kuwaangazia watu wote. Basi, Neno alikuwako ulimwenguni, na kwa njia yake ulimwengu uliumbwa, lakini ulimwengu haukumtambua. Alikuja katika nchi yake mwenyewe, nao walio wake hawakumpokea. Lakini wale waliompokea, wale waliomwamini, aliwapa uwezo wa kuwa watoto wa Mungu, ambao walizaliwa si kwa maumbile ya kibinadamu, wala kwa nguvu za kimwili, wala mapenzi ya mtu, bali kutokana na Mungu mwenyewe. Naye Neno akawa mwanadamu, akakaa kwetu. Nasi tumeuona utukufu wake, utukufu wake yeye aliye Mwana wa pekee wa Baba; amejaa neema na ukweli. Yohane aliwaambia watu habari zake, akasema kwa sauti, “Huyu ndiye niliyemtaja wakati niliposema: ‘Anakuja mtu mmoja baada yangu ambaye ni mkuu kuliko mimi, maana alikuwako kabla mimi sijazaliwa.’” Kutokana na ukamilifu wake sisi sote tumepokea neema kupita neema. Maana Mungu alitoa sheria kwa njia ya Mose, nayo neema na kweli vimetujia kwa njia ya Yesu Kristo. Hakuna mtu aliyemwona Mungu kamwe. Mwana wa pekee aliye sawa na Mungu ambaye ameungana na Baba, ndiye aliyetujulisha habari za Mungu.

Asante Mungu wetu,Baba yetu,Muumba wetu..
Asante kwa wema na fadhili zako kwetu..
Asante kwa ulinzi wako wakati wote..
Unastahili sifa Baba wa Mbinguni,Unastahili kuabudiwa Jehovah..
Unastahili kutukuzwa Yahweh,Unastahili kuheshimiwa Mungu wetu..
Matendo yako ni ya Ajabu,Wema na fadhili zako  zatutosha..

Huu ndio ushahidi Yohane alioutoa wakati viongozi wa Wayahudi kule Yerusalemu walipowatuma makuhani na Walawi, wamwulize: “Wewe u nani?” Yohane hakukataa kujibu swali hilo, bali alisema waziwazi, “Mimi siye Kristo.” Hapo wakamwuliza, “Basi, wewe ni nani? Je, wewe ni Elia?” Yohane akajibu, “La, mimi siye.” Wakamwuliza, “Je, wewe ni yule nabii?” Yohane akawajibu, “La!” Nao wakamwuliza, “Basi, wewe ni nani? Wasema nini juu yako mwenyewe? Tuambie, ili tuwapelekee jibu wale waliotutuma.” Yohane akawajibu, “Mimi ndiye yule ambaye nabii Isaya alisema habari zake: ‘Sauti ya mtu anaita jangwani: Nyosheni njia ya Bwana.’” Hao watu walikuwa wametumwa na Mafarisayo. Basi, wakamwuliza Yohane, “Kama wewe si Masiha, wala Elia, wala yule nabii, mbona wabatiza?” Yohane akawajibu, “Mimi nabatiza kwa maji, lakini yuko mmoja kati yenu, msiyemjua bado. Huyo anakuja baada yangu, lakini mimi sistahili hata kumfungua kamba za viatu vyake.” Mambo haya yalifanyika huko Bethania, ngambo ya mto Yordani ambako Yohane alikuwa anabatiza.


Sifa na Utukufu ni kwako Mungu wetu..
Tunakuja Mbele zako Mungu wetu,Tukijinyenyekeza,tukijishusha na kujiachilia mikononi mwako..
Tunaomba utusamehe dhambi zetu zote tulizozifanya..
Kwakuwaza,kwakunena,kwakutenda,kwakujua/kutojua..
Baba wa Upendo nasi tunaomba utupe neema ya kuweza kuwasamehe wale wote waliotukosea..

Kesho yake, Yohane alimwona Yesu akimjia, akasema, “Huyu ndiye Mwanakondoo wa Mungu aondoaye dhambi ya ulimwengu! Huyu ndiye niliyeongea juu yake niliposema: ‘Baada yangu anakuja mtu mmoja aliye mkuu zaidi kuliko mimi, maana alikuwako kabla mimi sijazaliwa!’ Mimi mwenyewe sikumfahamu, lakini nimekuja kubatiza kwa maji ili watu wa Israeli wapate kumjua.” Yohane alishuhudia hivi: “Nilimwona Roho akishuka kama njiwa kutoka mbinguni na kutua juu yake. Mimi sikumjua, lakini yule aliyenituma kubatiza watu kwa maji alikuwa ameniambia: ‘Mtu yule utakayemwona Roho akimshukia kutoka mbinguni na kukaa juu yake, huyo ndiye anayebatiza kwa Roho Mtakatifu.’ Mimi nimeona na nimeshuhudia kwamba huyu ndiye Mwana wa Mungu.”

Yahweh utuepushe katika majaribu na utuokoe na yule mwovu na kazi zake zote..
Ututakase miili yetu na akili zetu na utufunike kwa Damu ya Bwana wetu Yesu Kristo wa Nazareti..

Hii ni mara yangu ya tatu kuja kwenu. “Kila tatizo litatatuliwa kwa ushahidi wa watu wawili au watatu,” yasema Maandiko. Nilikwisha sema, na kama ilivyokuwa safari ya pili, sasa nasema tena nikiwa mbali: Wale wote waliotenda uovu bila kutubu, na pia wale wengine, nitakapokuja, sitakuwa na huruma. Mtajionea wenyewe kwamba Kristo anasema ndani yangu. Kwenu Kristo si dhaifu; bali nguvu yake yafanya kazi miongoni mwenu. Maana hata kama alisulubiwa kwa sababu ya udhaifu, lakini sasa anaishi kwa uwezo wa Mungu. Sisi pia tu dhaifu kwa kuungana naye lakini tutaishi naye kwa uwezo wa Mungu kwa ajili yenu. Jichunguzeni nyinyi wenyewe mpate kujua kama kweli mnayo imani. Jichunguzeni nyinyi wenyewe. Je, hamjui kwamba Kristo Yesu yumo ndani yenu? Kama sivyo, basi nyinyi mmeshindwa. Lakini natumaini kwamba nyinyi mnajua kuwa sisi hatukushindwa. Tunamwomba Mungu msifanye uovu wowote, lakini si kusudi tuonekane kama watu waliokwisha faulu, bali mpate kutenda mema, hata kama sisi tunaonekana kuwa tumeshindwa. Maana hatuwezi kuupinga ukweli; uwezo tulio nao ni wa kuuendeleza ukweli. Tunafurahi kwamba sisi tu dhaifu, lakini nyinyi mna nguvu; kwa hiyo tunaomba mpate kuwa wakamilifu. Basi, ninaandika barua hii nikiwa mbali, ili nitakapofika kwenu nisilazimike kuwa mkali kwenu kwa kutumia ule uwezo alionipa Bwana; naam, uwezo wa kujenga na si wa kubomoa. Kwa sasa, ndugu, kwaherini! Muwe na ukamilifu, shikeni mashauri yangu, muwe na nia moja; kaeni kwa amani. Naye Mungu wa upendo na amani atakuwa pamoja nanyi. Salimianeni kwa ishara ya upendo. Watu wote wa Mungu huku wanawasalimuni. Neema ya Bwana Yesu Kristo na upendo wa Mungu na umoja wa Roho Mtakatifu, viwe nanyi nyote.

Mungu Baba tunaomba utubariki na ukabariki kazi za mikono yetu..
Ukabariki ridhiki zetu ziingiazo/zitokazo..
Jehovah nasi ukatupe neema ya kuweza kuwabariki wenye kuhitaji..
Yahweh tusipungukiwe katika mahitaji yetu Baba  ukatupe sawasawa na mapenzi yako..
Baba wa Mbinguni tunayaweka maisha yetu mikononi mwako..
Ukatuongoze katika yote tunayoenda kufanya/kutenda
 na tukatende kamainavyokupendeza wewe..
Ukatupe neema ya kusimamia Neno lako,Amri na Sheria zako..
Ukatufanye chombo chema nasi tukatumike sawasawa na mapenzi yako..
Roho Mtakatifu akatuongoze katika yote na tukawe na kiasi..
Asante Mungu wetu na yote tunayaweka mikononi mwako..
Tuliyoyanena na tusiyo yanena Mungu wetu unayajua na kutujua sisi zaidi ya tunavyojijua..
Kwakuwa Ufalme ni wako Nguvu na Utukufu hata Milele..
Amina..!
Asanteni sana wapendwa/waungwana kwa kuwa nami..
Mungu aendelee kuwalinda na kuwatendea kama inavyompendeza yeye..
Nawapenda.



Desturi za maombolezo zilizokatazwa

1“Nyinyi ni watoto wa Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu; msijichanje wala kunyoa upara kwa ajili ya mtu aliyefariki. 2Nyinyi ni watu watakatifu kwa Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu; Mwenyezi-Mungu amewachagua muwe watu wake hasa, kati ya watu wote waishio duniani.

Wanyama safi na najisi

(Lawi 11:1-47)
3“Msile kitu kilicho chukizo kwa Mungu. 4Mnaweza kula wanyama wafuatao: Ng'ombe, kondoo, mbuzi, 5kulungu, paa, kongoni, mbuzimwitu, paa mweupe, pofu na mbuzi wa mlimani; 6na kila mnyama mwenye kwato zilizogawanyika sehemu mbili na mwenye kucheua, huyo mnaweza kula. 7Lakini msile mnyama yeyote ambaye kwato zake hazikugawanyika sehemu mbili na hacheui; msile ngamia, sungura na pelele, ingawa hucheua lakini kwato zao hazikugawanyika sehemu mbili; hao ni najisi kwenu. 8Pia msile nguruwe, maana ijapokuwa kwato zake zimegawanyika sehemu mbili, yeye hacheui; hao ni najisi kwenu, msile nyama zao wala msiguse mizoga yao.
9“Mnaweza kula kila aina ya samaki wenye mapezi na magamba. 10Lakini kiumbe chochote kinachoishi majini kisicho na mapezi wala magamba msile; hivyo ni najisi kwenu.
11“Mnaweza kula ndege wote walio safi. 12Lakini msile ndege wafuatao: Furukombe, kipungu, 13kengewa, kozi, mwewe kwa aina zake, 14kunguru kwa aina zake, 15mbuni, kirukanjia, dudumizi, kipanga kwa aina zake, 16bundi, mumbi, bundi mkubwa, 17mwari, nderi, mnandi, 18membe, koikoi kwa aina zake, hudihudi na popo. 19Na wadudu wote wenye mabawa ni najisi kwenu; msiwale. 20Mnaweza kula viumbe vyote vyenye mabawa vilivyo safi. 21Msile nyamafu yoyote; mnaweza kumpa mgeni anayeishi katika miji yenu, ale, au mnaweza kumwuzia mtu wa taifa lingine, kwa sababu nyinyi ni watakatifu na Mwenyezi-Mungu ni Mungu wenu. Msimchemshe mwanambuzi katika maziwa ya mama yake.

Sheria kuhusu zaka

22“Toeni sehemu moja ya kumi ya mazao yenu yote ya shambani kila mwaka. 23Halafu nendeni mahali ambapo Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu amepachagua kuweka jina lake, na mkiwa mbele yake mtaila zaka ya nafaka yenu, ya divai yenu na ya mafuta, na ya wazaliwa wa kwanza wa ng'ombe na kondoo wenu; fanyeni hivi ili mjifunze kumcha Mwenyezi-Mungu Mungu wenu daima. 24Ikiwa safari ni ndefu kwa kuwa Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu, amechagua mahali pa kuweka jina lake ambapo ni mbali mno na nyumbani, nanyi hamwezi kubeba zaka za mazao yenu ambayo Mwenyezi-Mungu amewajalia kupata, basi, fanyeni hivi:
25“Uzeni mazao yenu na kuchukua fedha hiyo mpaka mahali Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu, alipopachagua, 26mzitumie hizo fedha kwa chochote kile mtakachopenda – nyama ya ng'ombe, nyama ya kondoo, divai au kinywaji kikali; mtavila na kufurahi hapo mbele ya Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu, pamoja na jamaa zenu. 27Msiwasahau Walawi wanaoishi miongoni mwenu; wao hawana fungu wala urithi wao kati yenu. 28Na kila mwisho wa mwaka wa tatu toeni zaka ya mazao yenu yote na kuyaweka akiba katika miji yenu. 29Hiyo itakuwa kwa ajili ya Walawi, kwa kuwa hawana fungu wala urithi wao kati yenu, nao wageni, yatima na wajane ambao wanaishi katika miji yenu, watakuja kula na kushiba. Fanyeni hivi naye Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu, awabariki katika kazi zenu zote mfanyazo kwa mikono yenu.



Kumbukumbu la Sheria 14:1-29

Biblia Habari Njema kwa Watu Wote(BHN)

"Swahili Na Waswahili"Mbarikiwe.

No comments: