Swahili na Waswahili

Swahili na Waswahili
Waswahili na Mswahili Rachel Siwa...Pamoja Daima!!

Thursday 20 July 2017

Kikombe Cha Asubuhi;kitabu cha Hesabu..13

Shalom,Habari za Asubuhi,Hamjambo,Mmeamkaje?

Tumshukuru Mungu wetu kwa mema Mengi aliyotutendea/anayotundea..
Mungu wetu Baba yetu,Muumba wetu,Muumba wa Mbingu na Nchi..
Mungu wa Abrahamu,Isaka na Yakobo..
Asante kwa wema na fadhili zako kwetu..
Asante kwa ulinzi wako wakati wote..
Asante kwakutuchagua tena na kutupa kibali cha kuendelea kuiona leo hii..
Baba wa Mbinguni tunakuja mbele zako tukijinyeyekeza na kujiachilia mikononi mwako..
Tunaomba utusamehe dhambi zetu zote tulizoziwaza,tulizozinena,tulizizitenda,tulizozifanya kwakujua/kutojua..
Mfalme wa amani tunaomba nasi utupe neema ya kuweza kuwasamehe wale waliotukosea..
Utuepushe katika majiribu Mungu wetu utuokoe na yule mwovu na kazi zake zote..

Hatimaye, ndugu, tuombeeni ili ujumbe wa Bwana uzidi kuenea upesi na kupokelewa kwa heshima kama vile ulivyo kati yenu. Ombeni pia ili Mungu atuokoe na watu wapotovu na waovu, maana si wote wanauamini ujumbe huu. Lakini Bwana ni mwaminifu. Yeye atawaimarisheni na kuwalinda salama na yule Mwovu. Naye Bwana anatupatia tumaini kubwa juu yenu, na hatuna shaka kwamba mnafanya na mtaendelea kufanya yale tuliyowaambieni. Bwana aiongoze mioyo yenu katika upendo wa Mungu na katika uvumilivu tunaopewa na Kristo.

Mungu wetu tunaomba ututakase Miili yetu na Akili zetu kwa Damu ya Bwana wetu Yesu Kristo wa Nazareti..
Yeye aliteseka kwanza ili sisi tupate kupona..
Roho Mtakatifu akatuongoze katika yote tupate kutambua/kujitambua  Mfalme wa amani ukatupe neema ya kusimamia Neno lako,Amri na Sheria zako..Tukawe wanyenyekevu na wasikivu,ukatupe macho ya rohoni na tusiwe watu wakujisifu na kufuata tamaa za mwili na tukawe na kiasi..
Jehovah tunayaweka maisha yetu mikononi mwako tunaomba utubariki na ukabariki vyote tunavyoenda kufanya/kutenda na tukatende kama inavyokupendeza wewe..
tusipungukiwe katika mahitaji yetu Baba wa Mbinguni ukatupe sawasawa na mapenzi yako..
Yahweh ukabariki ridhiki zetu ziingiazo na zitokazo nasi ukatupe neema ya kuweza kuwabariki wenye kuhitaji..
Ukatufanye chombo chema na tukatumike sawasawa na mapenzi yako..

Je, maisha yenu katika Kristo yanawapeni nguvu? Je, upendo wake unawafarijini? Je, mnao umoja na Roho Mtakatifu na kuoneana huruma na kusikitikiana nyinyi kwa nyinyi? Basi, ikamilisheni furaha yangu kwa kuwa na fikira moja, upendo mmoja, moyo mmoja na nia moja. Msifanye chochote kwa moyo wa fitina au kwa majivuno ya bure; muwe na unyenyekevu nyinyi kwa nyinyi, na kila mmoja amwone mwenzake kuwa bora kuliko yeye mwenyewe. Pasiwe na mtu anayetafuta faida yake mwenyewe tu bali faida ya mwenzake. Muwe na msimamo uleule aliokuwa nao Kristo Yesu: Yeye, kwa asili alikuwa daima Mungu; lakini hakufikiri kwamba kule kuwa sawa na Mungu ni kitu cha kungangania kwa nguvu. Bali, kwa hiari yake mwenyewe, aliachilia hayo yote, akajitwalia hali ya mtumishi, akawa sawa na wanadamu, akaonekana kama wanadamu. Alijinyenyekesha na kutii mpaka kufa, hata kufa msalabani. Kwa sababu hiyo Mungu alimkweza juu kabisa, akampa jina lililo kuu kuliko majina yote. Ili kwa heshima ya jina la Yesu, viumbe vyote mbinguni, duniani na kuzimu, vipige magoti mbele yake, na kila mtu akiri kwamba Yesu Kristo ni Bwana, kwa utukufu wa Mungu Baba.


Jehovah tazama wenye shida/tabu,wagonjwa,wote wanaopita magumu/majaribu mbalimbali,waliokata tamaa,waliokataliwa,Mungu wetu ukaonekane kwenye mapito yao..ukawaguse na mkono wako wenye nguvu,ukawaokoe na kuwaponya kimwili na kiroho pia..ukawape neema ya kukujua wewe na kufuata sheria zako,wakasimamie Neno lako na nalo likawaweke huru..wafiwa ukawe mfariji wao...


Walipowafikia wale wanafunzi wengine, waliona umati mkubwa wa watu hapo. Na baadhi ya waalimu wa sheria walikuwa wanajadiliana nao. Mara tu ule umati wa watu ulipomwona, wote walishangaa sana, wakamkimbilia wamsalimu. Yesu akawauliza, “Mnajadiliana nini nao?” Hapo mtu mmoja katika ule umati wa watu akamjibu, “Mwalimu, nimemleta mwanangu kwako, ana pepo aliyemfanya kuwa bubu. Kila mara anapomvamia, humwangusha chini na kumfanya atokwe na povu kinywani, akisaga meno na kuwa mkavu mwili wote. Niliwaomba wanafunzi wako wamtoe huyo pepo lakini hawakuweza.” Yesu akawaambia, “Enyi kizazi kisicho na imani! Nitakaa nanyi mpaka lini? Nitawavumilia mpaka lini? Mleteni kwangu.” Wakampeleka. Mara tu huyo pepo alipomwona Yesu, alimtia mtoto kifafa, naye mtoto akaanguka chini, akagaagaa na kutoka povu kinywani. Yesu akamwuliza baba yake huyo mtoto, “Amepatwa na mambo hayo tangu lini?” Naye akamjibu, “Tangu utoto wake. Na mara nyingi pepo huyo amemwangusha motoni na majini, ili amwangamize kabisa. Basi, ikiwa waweza, utuhurumie na kutusaidia!” Yesu akamwambia, “Ati ikiwa waweza! Mambo yote yanawezekana kwa mtu aliye na imani.” Hapo, huyo baba akalia kwa sauti, “Naamini! Lakini imani yangu haitoshi, nisaidie.” Yesu alipouona umati wa watu unaongezeka upesi mbele yake, alimkemea yule pepo mchafu “Pepo unayemfanya huyu mtoto kuwa bubu na kiziwi, nakuamuru, mtoke mtoto huyu wala usimwingie tena!” Hapo huyo pepo alipaza sauti, akamwangusha huyo mtoto chini, kisha akamtoka. Mtoto alionekana kama maiti, hata wengine walisema, “Amekufa!” Lakini Yesu akamshika mkono, akamwinua, naye akasimama. Basi, Yesu alipoingia nyumbani, wanafunzi wake walimwuliza kwa faragha, “Kwa nini sisi hatukuweza kumtoa?” Naye akawaambia, “Pepo wa aina hii hawezi kutoka isipokuwa kwa sala.”
Asante Mungu wetu..tunakushukuru na kukusifu Daima..
Sifa na Utukufu tunakurudishia Mungu wetu..
Kwakuwa Ufalme ni wako Nguvu na Utukufu hata Milele..
Amina..!
Mungu aendelee kuwabariki katika yote.
Asanteni sana kwakuwa nami..
Nawapenda.

Wapelelezi

(Kumb 1:19-33)
1Mwenyezi-Mungu akamwambia Mose, 2“Tuma watu waende wakaipeleleze nchi ya Kanaani ambayo ninawapa wana wa Israeli. Utatuma mtu mmoja kutoka katika kila kabila, na mtu huyo lazima awe kiongozi katika kabila lake.”
3Basi, kwa mujibu wa agizo la Mwenyezi-Mungu, Mose akatuma watu kutoka jangwa la Parani. Watu wote waliotumwa walikuwa viongozi wa makabila mbalimbali ya wana wa Israeli. 4Ifuatayo ndiyo orodha ya majina ya watu hao:
Kabila la Reubeni, Shamua mwana wa Zakuri.
5Kabila la Simeoni, Shafati mwana wa Hori.
6Kabila la Yuda, Kalebu mwana wa Yefune.
7Kabila la Isakari, Igali mwana wa Yosefu.
8Kabila la Efraimu, Hoshea mwana wa Nuni.
9Kabila la Benyamini, Palti mwana wa Rafu.
10Kabila la Zebuluni, Gadieli mwana wa Sodi.
11Kabila la Yosefu (yaani kabila la Manase), Gadi mwana wa Susi.
12Kabila la Dani, Amieli mwana wa Gemali.
13Kabila la Asheri, Sethuri mwana wa Mikaeli.
14Kabila la Naftali, Nabi mwana wa Wofsi.
15Kabila la Gadi, Geueli mwana wa Maki.
16Haya ndiyo majina ya watu ambao Mose aliwatuma kwenda kuipeleleza nchi ya Kanaani. Mose alimpa Hoshea mwana wa Nuni jina jipya, akamwita Yoshua.
17Alipowatuma kwenda kuipeleleza nchi ya Kanaani, Mose aliwaambia: “Nendeni juu kule Negebu, hadi kwenye nchi ya milima, 18mkaipeleleze nchi ilivyo. Chunguzeni pia kama watu wanaoishi humo ni wenye nguvu au dhaifu, wengi au wachache. 19Pelelezeni kama nchi hiyo ni nzuri au mbaya, na kama miji wanamoishi ni kambi au ni nyumba zilizozungukwa na ngome. 20Chunguzeni pia kama nchi yenyewe ni tajiri au maskini, ina miti au haina. Muwe na mioyo ya ujasiri na mnaporudi chukueni baadhi ya matunda ya nchi hiyo.” Hayo yalikuwa majira ya zabibu zianzapo kuiva. 21Basi, watu hao wakaenda na kuipeleleza nchi toka jangwa la Sini hadi Rehobu, karibu na njia ya kuingilia Hamathi. 22Walikwenda hadi Negebu wakapita mpaka mji wa Hebroni. Humo waliwakuta Waahimani, Washeshai na Watalmai, wazawa wa Anaki. (Mji wa Hebroni ulikuwa umejengwa miaka saba kabla ya mji wa Soani ulioko nchini Misri). 23Walipofika katika Bonde la Eshkoli, watu hao walikata shada la mzabibu lililokuwa na matunda mengi nalo lilibebwa na watu wawili juu ya mti. Walichukua pia makomamanga kadhaa na tini. 24Mahali hapo paliitwa Bonde la Eshkoli#13:24 Eshkoli: Kiebrania maana yake “shada”. kwa sababu ya shada ambalo watu hao wa Israeli walikata kutoka mahali hapo.
25Baada ya kuipeleleza nchi kwa muda wa siku arubaini, watu hao walirudi. 26Waliwaendea Mose, Aroni na jumuiya ya Waisraeli huko Kadeshi, katika jangwa la Parani, wakatoa taarifa ya mambo waliyoyaona na kuwaonesha matunda ya nchi. 27Walimwambia Mose, “Tuliifikia nchi uliyotutuma tuipeleleze; hiyo ni nchi inayotiririka maziwa na asali, na hili ni tunda lake. 28Lakini wenyeji wake ni wenye nguvu sana, na miji yao ni imara na mikubwa sana. Zaidi ya hayo, huko tuliona wazawa wa Anaki. 29Waamaleki wanakaa katika eneo la Negebu; Wahiti, Wayebusi na Waamori wanakaa katika eneo la milima, na Wakanaani wanakaa karibu na bahari ya Mediteranea na karibu na kingo za mto Yordani.”
30Lakini Kalebu aliwanyamazisha watu mbele ya Mose, akasema, “Twende mara moja tukaimiliki nchi hiyo. Kwa kuwa tunao uwezo sana wa kushinda.” 31Lakini watu walioandamana naye kuipeleleza nchi wakasema, “Hatutaweza kupigana na watu hao; wao wana nguvu kuliko sisi.” 32Kwa hiyo wakaeneza mambo ya uongo kati ya wana wa Israeli kuhusu nchi waliyoipeleleza, wakisema, “Nchi hiyo inawaua watu wake. Pia watu wote tuliowaona huko ni wakubwa sana. 33Tuliona majitu huko, wazawa wa Anaki. Sisi tulijiona kuwa kama panzi mbele yao, na ndivyo walivyotuona sisi.”

Hesabu13;1-33


Biblia Habari Njema kwa Watu Wote(BHN)

"Swahili Na Waswahili"Mbarikiwe.

No comments: