Swahili na Waswahili

Swahili na Waswahili
Waswahili na Mswahili Rachel Siwa...Pamoja Daima!!

Friday 17 November 2017

Kikombe Cha Asubuhi ;Waamuzi 5...



Shalom,Habari za Asubuhi,Hamjambo,Mmeamkaje?

Tumshukuru Mungu wetu katika yote..
Mungu wetu,Baba yetu,Muumba wetu,Muumba wa Nchi na Mbingu,
Muumba wa vyote vinavyoonekana na visivyoonekana,Muweza wa yote
Mungu wa Abrahamu,Isaka na Yakobo,Mungu mwenye nguvu,Mfalme wa amani,Alfa na Omega,wewe ni mwanzo na wewe ni mwisho,Hakuna kama wewe,Unatosha Baba wa Mbinguni...!

Asante Mungu wetu kwa wema na fadhili zako kwetu..
Asante kwa ulinzi wako kwetu wakati wote..
Asante kwa kutuchagua tena na kutupa kibali cha kuendelea kuiona leo hii..

Sifa na utukufu tunakurudishia wewe..!!



Enyi watoto, watiini wazazi wenu Kikristo maana hili ni jambo jema. “Waheshimu Baba na mama yako,” hii ndiyo amri ya kwanza ambayo imeongezewa ahadi, yaani, “Upate fanaka na kuishi miaka mingi duniani.” Nanyi akina baba, msiwachukize watoto wenu ila waleeni katika nidhamu na mafundisho ya Kikristo.
Tunakuja mbele zako Mungu wetu tukijinyenyekeza,tukijishusha na
kujiachilia mikononi mwako Jehovah..
Tunaomba utusamehe dhambi zetu zote tulizo zifanya..
kwakuwaza,kwakunena,kwakutenda,kwakujua/kutojua..
Baba wa Mbinguni nasi tunaomba utupe neema ya kuweza
kuwasamehe wale wote waliotukosea..
Mungu wetu tunaomba utuepushe katika majaribu
Baba utuokoe na yule mwovu na kazi zake zote..
Yahweh tunaomba ututakase miili yetu na akili zetu Jehovah
utufunike kwa Damu ya mwanao mpendwa Bwana na Mwokozi
wetu Yesu Kristo wa Nazareti,yeye aliteseka kwanza ili sisi tupate kupona..




Enyi watumwa, watiini mabwana zenu hapa duniani kwa hofu na kutetemeka; fanyeni hivyo kwa unyofu wa moyo kana kwamba mnamtumikia Kristo. Fanyeni hivyo si tu wakati wanapowatazama ili mjipendekeze kwao, bali tumikieni kwa moyo kama atakavyo Mungu kwa sababu nyinyi ni watumishi wa Kristo. Muwe radhi kutumikia kwa ajili ya Bwana na si kwa ajili ya watu. Kumbukeni kwamba kila mtu mwenye kutenda mema, awe mtumwa au mtu huru, atapokea tuzo lake kutoka kwa Bwana. Nanyi mnaotumikiwa, watendeeni vivyo hivyo watumwa wenu, na acheni kutumia vitisho. Kumbukeni kwamba nyinyi pia kama vile wao, mnaye Bwana yuleyule mbinguni, naye hatendi kwa ubaguzi.
Baba wa Mbinguni tunaomba ukabariki kazi za mikono yetu
Mungu wetu ukatupe ubunifu,maarifa katika ufanyaji/utendaji
Yahweh tukatende sawasawa na mapenzi yako..
Mungu wetu tunaomba ukabariki ridhiki zetu ziingiazo/zitokazo
Jehovah nasi tunaomba utupe neema ya kuweza kuwabariki
wenye kuhitaji,Mungu wetu tusipungukiwe katika mahitaji yetu
Yahweh ukatupe kama inavyokupendeza wewe..


Mungu wetu tunaomba ukabariki Nyumba/ndoa zetu,watoto,wazazi
wetu,familia/ndugu na wote wanaotuzunguka,Mfalme wa amani
tunaomba amani yako itawale katika maisha yetu,Mungu wetu tunaomba
ulinzi wako kwetu na kwa vyote tunavyovimiliki,Yahweh ukatamalaki
na kutuatamia,Baba wa Mbinguni ukatupe neema ya kufuata njia zako,kusimamia Neno lako amri na sheria zako siku zote za maisha yetu
Jehovah ukatufanye chombo chema nasi tukatumike
 kama inavyokupendeza wewe..
Roho Mtakatifu akatuongoze katika yote tupate kutambua/kujitambua
na tukawe na kiasi..



Hatimaye, nawatakeni muwe imara katika kuungana na Bwana na kwa msaada wa nguvu yake kuu. Vaeni silaha anazowapeni Mungu mpate kuzipinga mbinu mbaya za Ibilisi. Maana vita vyetu si vita kati yetu na binadamu, bali ni vita dhidi ya jeshi ovu la ulimwengu wa roho; tunapigana na watawala, wakuu na wenye nguvu, wanaomiliki ulimwengu huu wa giza. Kwa sababu hiyo, vaeni silaha za Mungu ili siku ile itakapofika mweze kuyapinga mashambulio ya adui; na mkisha pigana mpaka mwisho, mtakuwa bado imara. Basi, kaeni tayari. Ukweli na uwe kama mkanda kiunoni mwenu, uadilifu uwe kama vazi la kujikinga kifuani, na hamu ya kutangaza Habari Njema ya amani iwe kama viatu miguuni mwenu. Zaidi ya hayo yote, imani iwe daima kama ngao mikononi mwenu, iwawezeshe kuizima mishale ya moto ya yule Mwovu. Upokeeni wokovu kama kofia yenu ya chuma, na neno la Mungu kama upanga mnaopewa na Roho Mtakatifu. Salini daima, mkiomba msaada wa Mungu. Salini kila wakati kwa nguvu ya Roho. Kesheni bila kuchoka mkisali kwa ajili ya watu wote wa Mungu. Niombeeni nami pia ili niongeapo Mungu anijalie cha kusema, niweze kuwajulisha watu fumbo la Injili kwa uthabiti. Mimi ni balozi kwa ajili ya Injili hiyo ingawa sasa niko kifungoni. Ombeni, basi, ili niweze kuwa hodari katika kuitangaza kama inipasavyo.
Mungu wetu tunaomba ukawaguse kwa mkono wako wenye nguvu
wote wanaopitia magumu/majaribu,wagonjwa,wenye shida/tabu,
waliokatika vifungo vya yule mwovu  Baba ukawape uponyaji wa mwili na
roho,ukawape neema ya kujiombea na kufuata njia zako,wenye njaa
Mungu wetu ukawatendee na kubariki mashamba yao,wafiwa ukawe
mafariji wao,Mungu wetu ukafute machozi ya watoto wako na ukasikie
kuomba kwao,Nuru yako ikaangaze katika maisha yao..
Kwakuwa Ufalme ni wako Nguvu na Utukufu hata Milele..
Amina...!



Tukiko, ndugu yetu mpenzi na mtumishi mwaminifu katika kuungana na Bwana, atawapeni habari zangu zote mpate kujua ninachofanya. Namtuma kwenu awapeni habari zetu mpate kuwa na moyo. Ninawatakieni nyinyi ndugu amani, upendo na imani kutoka kwa Mungu Baba na kutoka kwa Bwana Yesu Kristo. Nawatakia neema ya Mungu wote wanaompenda Bwana wetu Yesu Kristo kwa mapendo yasiyo na mwisho.

Wapendwa katika Bwana asanteni sana kwakuwa nami
Mungu wa rehema/neema aendelee kuwabariki na kuwatendea
sawasawa na mapenzi yake, Amani ya Kristo Yesu iwe nanyi Daima..
Nawapenda.

Wimbo wa Debora

1Siku hiyo, Debora na Baraki, mwana wa Abinoamu, wakaimba wimbo huu:
2“Viongozi walijitokeza kuongoza Israeli,
watu walijitolea kwa hiari yao.
Mshukuruni Mwenyezi-Mungu!
3“Sikilizeni, enyi wafalme!
Tegeni sikio, enyi wakuu!
Nitamwimbia Mwenyezi-Mungu, Mungu wa Israeli.
4“Ee Mwenyezi-Mungu, ulipotoka huko Seiri,
ulipoteremka mlimani Edomu,
nchi ilitetemeka,
mbingu zilidondosha maji,
naam, mawingu yakaiangusha mvua.
5Milima ilitikisika mbele yako Mwenyezi-Mungu,
naam, mlima Sinai mbele yako Mwenyezi-Mungu, Mungu wa Israeli.
6“Katika siku za Shamgari, mwana wa Anathi,
katika wakati wa Yaeli,
misafara ilikoma kupita nchini,
wasafiri walipitia vichochoroni.
7Wakulima walikoma kuwako,
walikoma kuwako katika Israeli,
mpaka nilipotokea mimi Debora,
mimi niliye kama mama wa Israeli.
8Walijichagulia miungu mipya,
kukawa na vita katika nchi.
Lakini hakukupatikana mwenye upanga au ngao
kati ya watu 40,000 wa Israeli.
9Nawapa heshima makamanda wa Israeli
waliojitoa kwa hiari yao kati ya watu.
Mshukuruni Mwenyezi-Mungu!
10“Tangazeni, enyi wapandapunda weupe,
enyi mnaokalia mazulia ya fahari,
nyinyi mnaotembea njiani, tangazeni jambo hilo.
11Imbeni kupita wanamuziki kwenye visima vya maji,
tangazeni ushindi wa Mwenyezi-Mungu,
ushindi kwa wakulima wake katika Israeli.
Ndipo watu wa Mwenyezi-Mungu waliposhuka malangoni.
12“Amka, amka, Debora!
Amka! Amka uimbe wimbo!
Amka, Baraki mwana wa Abinoamu,
uwachukue mateka wako.
13Mashujaa waliobaki waliteremka,
watu wa Mwenyezi-Mungu walikwenda kumpigania
dhidi ya wenye nguvu.
14Kutoka Efraimu waliteremka bondeni,5:14 bondeni: Makala ya Kiebrania; katika Maaleki.
wakafuata ndugu zao watu wa Benyamini;
kutoka Makiri walishuka makamanda,
kutoka Zebuluni maofisa wakuu.
15Wakuu wa Isakari wakafuatana na Debora,
watu wa Isakari waaminifu kwa Baraki;
wakamfuata mbio mpaka bondeni.
Lakini miongoni mwa koo za Reubeni
kulikuwamo kusitasita kwingi.
16Kwa nini walibaki mazizini?
Ili kusikiliza milio ya kondoo?
Miongoni mwa koo za Reubeni
kulikuwamo kusitasita kwingi.
17Kabila la Gileadi lilibaki ngambo ya Yordani.
Kabila la Dani, kwa nini mlibaki merikebuni?
Kabila la Asheri lilitulia huko pwani ya bahari,
lilikaa bandarini mwake.
18Watu wa Zebuluni ni watu
waliohatarisha maisha yao katika kifo.
Hata wa Naftali walikikabili kifo
kwenye miinuko ya mashamba.
19“Huko Taanaki, kando ya chemchemi za Megido,
wafalme walikuja, wakapigana;
wafalme wa Kanaani walipigana,
lakini hawakupata nyara za fedha.
20Nyota kutoka mbinguni zilishiriki vita,
zilifuata njia zao, zilipigana na Sisera.
21Mafuriko ya mto Kishoni yaliwachukua mbali,
naam, mafuriko makali ya mto Kishoni.
Songa mbele kwa nguvu, ee nafsi yangu!
22“Farasi walipita wakipiga shoti;,
walikwenda shoti na kishindo cha kwato zao.
23Malaika wa Mwenyezi-Mungu asema hivi:
‘Uapizeni mji wa Merosi,
waapizeni vikali wakazi wake;
maana hawakuja kumsaidia Mwenyezi-Mungu
hawakumsaidia Mwenyezi-Mungu dhidi ya wenye nguvu’.
24“Abarikiwe kuliko wanawake wote
Yaeli, mke wa Heberi, Mkeni.
Naam, amebarikiwa kuliko wanawake wote
wanaokaa mahemani.
25Sisera alimwomba maji, naye akampa maziwa;
alimletea siagi katika bakuli ya heshima.
26Kwa mkono mmoja alishika kigingi cha hema,
na kwa mkono wake wa kulia nyundo ya fundi;
alimponda Sisera kichwa,
alivunja na kupasuapasua paji lake.
27Sisera aliinama, akaanguka;
alilala kimya miguuni pake.
Hapo alipoinama ndipo alipoanguka, amekufa!
28“Mama yake Sisera alitazama dirishani
alichungulia katika viunzi vyake, akalalamika:
‘Kwa nini gari lake limechelewa?
Mbona vishindo vya magari yake vimechelewa kusikika?’
29Jibu akalipata kwa wanawake wenye hekima:
Akajituliza tena na tena kwa jibu hilo:
30‘Bila shaka wanatafuta na kugawana nyara;
msichana mmoja au wawili kwa kila askari,
vazi la sufu ya rangi kwa ajili ya Sisera.
Vazi la sufu iliyotariziwa,
na mikufu miwili ya nakshi kwa ajili ya shingo yangu!’
31“Ee Mwenyezi-Mungu, waangamie adui zako wote!
Lakini rafiki zako na wawe kama jua,
wakati linapochomoza kwa mwanga mkubwa!”
Nayo nchi ikawa na amani kwa muda wa miaka arubaini.


Waamuzi 5;1-31

Biblia Habari Njema kwa Watu Wote(BHN)

"Swahili Na Waswahili"Mbarikiwe.

Thursday 16 November 2017

Kikombe Cha Asubuhi ;Waamuzi 4...



Shalom,Habari za Asubuhi,Hamjambo,Mmeamkaje?

Tumshukuru Mungu wetu katika yote..
Mtakatifu..!Mtakatifu..!Mtakatifu..!Baba wa Mbinguni..
Mungu wetu,Muumba wetu,Muumba wa Vyote vilivyopo..
Mungu wa Abrahamu,Isaka na Yakobo,Mungu wa wote walio hai..
Baba wa Yatima,Mume wa wajane,Baba wa Upendo,Mungu wa huruma Muweza wa yote,Mponyaji wetu,Jehovah..!Yahweh..!Adonai..!
El Shadai..!Elohim..!El Elyon..!El Olam..!El Qanna..!Emanueli..!Mungu pamoja nasi..!

Utukuzwe ee Mungu wetu,Usifiwe Baba wa Mbinguni,
Unatosha Mungu wetu,Hakuna kama wewe..!




Laiti mngenivumilia kidogo, hata kama mimi ni mjinga kiasi! Naam, nivumilieni kidogo. Ninawaoneeni wivu lakini ni wivu wa Mungu; maana nyinyi ni kama bikira safi niliyemposa kwa mwanamume mmoja tu ambaye ndiye Kristo. Lakini naogopa kwamba, kama vile yule nyoka kwa hila zake za uongo alimdanganya Hawa, fikira zenu zaweza kupotoshwa, mkauacha uaminifu wenu wa kweli kwa Kristo. Maana mtu yeyote ajaye na kumhubiri Yesu aliye tofauti na yule tuliyemhubiri, nyinyi mwampokea kwa mikono miwili; au mnakubali roho au Injili tofauti kabisa na ile mliyopokea kutoka kwetu! Sidhani kwamba mimi ni mdogo kuliko hao “mitume wakuu.” Labda sina ufasaha wa lugha, lakini elimu ninayo; jambo hili tumelionesha wazi kwenu, kila mahali na kila wakati.

Asante kwa wema na fadhili zako kwetu..
Asante kwa ulinzi wako kwetu wakati wote..
Asante kwakutuchagua tena na kutupa kibali cha kuendelea kuiona leo hii
Si kwamba tumetenda mema sana,si kwa nguvu/utashi wetu,si kwa akili zetu sisi kuwa hivi tulivyo leo hii Mungu wetu,Ni kwa Neema/rehema zako
Ni kwa mapenzi yako Mungu wetu kuwa hivi tulivyo..

Tazama jana imepita Mungu wetu Leo ni siku mpya na Kesho ni siku
Nyingine Baba wa Mbinguni..
Yahweh tunakuja mbele zako tukijinyenyekeza,tukijishusha na kujiachilia
mikononi mwako Mungu wetu..
Tunaomba utusamehe dhambi zetu zote tulizozifanya
kwakuwaza,kwakunena,kwakutenda,kwakujua/kutojua Mungu wetu
nasi tunaomba utupe neema ya kuweza kuwasamehe wale wote waliotukosea..
Jehovah tunaomba utuepushe katika majaribu Yahweh utuokoe na yule
mwovu na kazi zake zote..
Baba wa Mbinguni tunaomba ututakase miili yetu na akili zetu
Yahweh utufunike kwa Damu ya Bwana na Mwokozi wetu Yesu Kristo
wa Nazareti yeye aliteseka kwanza ili sisi tupate kupona..





Mimi niliihubiri kwenu Habari Njema ya Mungu bila kudai mshahara; nilijinyenyekesha ili nipate kuwakweza nyinyi. Je, nilifanya vibaya? Nilipofanya kazi kati yenu, mahitaji yangu yaligharimiwa na makanisa mengine. Kwa namna moja au nyingine niliwapokonya wao mali yao nipate kuwatumikia nyinyi. Nilipokuwa nanyi sikumsumbua mtu yeyote nilipohitaji fedha; ndugu waliotoka Makedonia waliniletea kila kitu nilichohitaji. Nilikuwa mwangalifu sana nisiwe mzigo kwa namna yoyote ile, na nitaendelea kufanya hivyo. Naahidi kwa ule ukweli wa Kristo ulio ndani yangu, kwamba hakuna kitakachoweza kunizuia kujivunia jambo hilo popote katika Akaya. Kwa nini nasema hivyo? Kwa sababu eti siwapendi nyinyi? Mungu anajua kwamba nawapenda! Nitaendelea kufanya kama ninavyofanya sasa, ili nisiwape nafasi wale wanaotafuta nafasi, nafasi ya kujivuna kwamba eti wanafanya kazi kama sisi. Maana, hao ni mitume wa uongo, wafanyakazi wadanganyifu wanaojisingizia kuwa mitume wa Kristo. Wala si ajabu, maana hata Shetani mwenyewe hujisingizia kuwa malaika wa mwanga! Kwa hiyo si jambo la kushangaza ikiwa na hao watumishi wake wanajisingizia kuwa watumishi wa haki. Mwisho wao watapata kile wanachostahili kufuatana na matendo yao.


Jehovah tunaomba ukabariki kazi za mikono yetu,Mungu wetu ukatupe
Ubunifu,Maarifa katika ufanyaji/utendaji nasi tukatende
sawasawa na mapenzi yako..
Yahweh tunaomba ukabariki ridhiki zetu ziingiazo/zitokazo Mungu wetu
nasi tunaomba utupe neema ya kuweza kuwabariki wenye kuhitaji..



Baba wa Mbinguni tunayaweka maisha yetu mikononi mwako..
Mfalme wa amani tunaomba amani yako ikatawale katika
nyumba/ndoa zetu,watoto,wazazi wetu,familia/ndugu na wote wanaotuzunguka..Mungu wetu tunaomba ulinzi wako kwetu na
kwa vyote tunavyovimiliki,Baba wa Mbinguni ukatawale,ukatamalaki na
kutuatamia,Mungu wetu ukaonekane katika maisha yetu,Baba ukatuokoe
katika majivuno,masengenyo,ugomvi,makwazo na vyote vinavyokwenda
kinyume nawe,Mungu wetu ukatupe neema ya kusaidiana,kupendana na tukafurahi pamoja na tukalie pamoja inapobidi..
Baba tukafuate njia zako,Tukasimamie Neno lako amri na sheria zako
siku zote za maisha yetu,Ukatufanye chombo chema nasi tukatumike
kama inavyokupendeza wewe..
Roho Mtakatifu akatuongoze katika yote na tukawe na kiasi..
Ee.. Baba ..!tunaomba upokee maombi/sala zetu..





Tena nasema: Mtu asinifikirie kuwa mpumbavu. Lakini kama mkifikiri hivyo, basi, nichukueni kama mpumbavu ili nami nipate kuwa na cha kujivunia angaa kidogo. Ninachosema sasa si kile alichoniagiza Bwana; kuhusu jambo hili la kujivuna, nasema tu kama mtu mpumbavu. Maadamu wengi hujivuna kwa sababu za kidunia, nami pia nitajivuna. Nyinyi ni wenye busara, ndiyo maana hata mnawavumilia wapumbavu! Mnamvumilia hata mtu anayewafanya nyinyi watumwa, mtu mwenye kuwanyonya, mwenye kuwakandamiza, mwenye kuwadharau na kuwapiga usoni! Kwa aibu nakubali kwamba sisi tulikuwa dhaifu. Iwe iwavyo, lakini kama kuna mtu yeyote anayethubutu kujivunia kitu – nasema kama mtu mpumbavu – mimi nathubutu pia. Je, wao ni Waebrania? Hata mimi. Je, wao ni Waisraeli? Hata mimi. Wao ni wazawa wa Abrahamu? Hata mimi. Wao ni watumishi wa Kristo? Hata mimi – nanena hayo kiwazimu – ni mtumishi wa Kristo zaidi kuliko wao. Mimi nimefanya kazi ngumu zaidi, nimekaa gerezani mara nyingi zaidi, nimepigwa mara nyingi zaidi na nimekaribia kifo mara nyingi. Mara tano nilichapwa vile viboko arubaini kasoro kimoja vya Wayahudi. Nilipigwa fimbo mara tatu, nilipigwa mawe mara moja; mara tatu nilivunjikiwa meli baharini, na humo nikakesha usiku kucha na kushinda mchana kutwa. Kila mara safarini nimekabiliwa na hatari za mafuriko ya mito, na hatari za wanyama; hatari kutoka kwa wananchi wenzangu na kutoka kwa watu wa mataifa mengine; hatari za mjini, hatari za porini, hatari za baharini, hatari kutoka kwa ndugu wa uongo. Nimefanya kazi na kutaabika, nimekesha bila usingizi mara nyingi; nimekuwa na njaa na kiu; mara nyingi nimefunga na kukaa katika baridi bila nguo. Na, licha ya mengine mengi, kila siku nakabiliwa na shughuli za makanisa yote. Kama mtu yeyote ni dhaifu, nami pia ni dhaifu; mtu yeyote akikwazwa, nami pia huwa na wasiwasi. Ikinilazimu kujivuna, basi, nitajivunia udhaifu wangu. Mungu na Baba wa Bwana Yesu – jina lake litukuzwe milele – yeye anajua kwamba sisemi uongo. Nilipokuwa Damasko, mkuu wa mkoa, aliyekuwa chini ya mfalme Areta, alikuwa akiulinda mji wa Damasko ili anikamate. Lakini, ndani ya kapu kubwa, niliteremshwa nje kupitia katika nafasi ukutani, nikachopoka mikononi mwake.



Mungu wetu ukawaguse kwa mkono wako wenye nguvu wagonjwa
wakapate uponyaji wako,wenye njaa ukawapatie chakula na ukabariki
mashamba yao wapate mavuno ya kutosha na kuweka akiba,
wanaopitia magumu/majaribu Mungu wetu ukawavushe,walio magerezani pasipo na hatia Baba ukawatete na kuwatendea,waliokatika vifungo vya
yule mwovu Mungu wetu ukawafungue na ukawaweke huru,Baba wa Mbinguni ukawape neema ya kujiombea,kufuata njia zako na Nuru yako
ikaangaze katika maisha yao..
Kwa imani tunayaweka haya yote mikononi mwako,tukiamini
wewe ni Mungu wetu Jana leo kesho na hata Milele..
Sifa na Utukufu ni wako Mungu wetu..
Kwakuwa Ufalme ni wako Nguvu na Utukufu hata Milele..
Amina...!


Asanteni sana wapendwa kwakuwa nami,Baba wa Mbinguni aendelee
kuwa nanyi,Amani,Upendo na Baraka zisipungue katika maisha yenu..
Nawapenda.

Debora na Baraki

1Baada ya kifo cha Ehudi, Waisraeli walitenda tena uovu mbele ya Mwenyezi-Mungu. 2Mwenyezi-Mungu akawatia mikononi mwa Yabini, mfalme wa Kanaani, ambaye aliishi huko Hazori. Kamanda wa jeshi lake alikuwa Sisera, mwenyeji wa Harosheth-hagoimu. 3Mfalme Yabini alikuwa na magari ya vita 900 ya chuma. Aliwakandamiza sana Waisraeli kwa miaka ishirini; nao wakamlilia Mwenyezi-Mungu awasaidie.
4Wakati huo, kulikuwa na nabii mwanamke aliyeitwa Debora, mke wa Lapidothi, aliyekuwa mwamuzi wa Waisraeli wakati huo. 5Debora alikuwa na mazoea ya kuketi chini ya mtende uliokuwa kati ya mji wa Rama na mji wa Betheli katika nchi ya milima ya Efraimu. Watu wa Israeli walimjia ili awaamulie mashauri yao. 6Siku moja alimwita Baraki mwana wa Abinoamu wa Kedeshi katika nchi ya Naftali. Alipokuja alimwambia, “Mwenyezi-Mungu, Mungu wa Israeli, anakuamuru hivi: ‘Nenda ukusanye watu wako mlimani Tabori, uchague watu 10,000 kutoka makabila ya Naftali na Zebuluni. 7Mimi nitamchochea Sisera, jemadari wa jeshi la Yabini, aje na majeshi na magari yake kupigana nawe kwenye mto Kishoni, na kumtia mikononi mwako.’” 8Baraki akamwambia Debora, “Kama utakwenda pamoja nami, nitakwenda. Lakini usipokwenda pamoja nami, sitakwenda.” 9Debora akamjibu, “Sawa. Nitakwenda pamoja nawe; lakini hutapata heshima yoyote ya ushindi, maana Mwenyezi-Mungu, atamtia Sisera mikononi mwa mwanamke.” Basi, Debora akafuatana na Baraki kwenda Kedeshi. 10Baraki akayaita makabila ya Naftali na Zebuluni huko Kedeshi; watu 10,000 wakamfuata. Debora akaenda pamoja naye.
11Wakati huo, Heberi, Mkeni, alikuwa amejitenga na Wakeni wenzake ambao ni wazawa wa Hobabu, baba mkwe wa Mose. Alikuwa amepiga hema lake mbali huko kwenye mwaloni wa Zaananimu, karibu na Kedeshi.
12Sisera alipopata habari kwamba Baraki mwana wa Abinoamu amekwenda mlimani Tabori, 13alikusanya jeshi lake lote na magari yake mia tisa ya chuma, akaondoka Harosheth-hagoimu, akaenda kwenye mto Kishoni. 14Debora akamwambia Baraki, “Inuka! Leo ni siku ambayo Mwenyezi-Mungu atamtia Sisera mikononi mwako. Mwenyezi-Mungu anakwenda mbele yako.” Basi, Baraki akashuka kutoka mlimani Tabori akiwaongoza watu wake 10,000. 15Baraki akafanya mashambulizi, naye Mwenyezi-Mungu akamtimua Sisera na jeshi lake lote mbele ya Baraki kwa upanga. Sisera akatoka katika gari lake, akakimbia kwa miguu. 16Baraki akalifuatia jeshi hilo na magari mpaka Harosheth-hagoimu na kuwaua wanajeshi wote wa Sisera kwa mapanga; hakubaki hata mtu mmoja.
17Lakini Sisera alikimbia kwa miguu mpaka hemani kwa Yaeli, mke wa Heberi, Mkeni. Alifanya hivyo kwa sababu kulikuwa na amani kati ya mfalme Yabini wa Hazori na jamaa ya Heberi. 18Yaeli akatoka kumlaki Sisera, akamwambia, “Bwana wangu, karibu kwangu, wala usiogope.” Akaingia hemani mwake, akamfunika kwa blanketi. 19Sisera akamwambia Yaeli, “Tafadhali, nipe maji kidogo ninywe, maana nina kiu.” Akampa maziwa badala ya maji, kisha akamfunika tena. 20Sisera akamwambia, “Simama mlangoni mwa hema. Mtu yeyote akija kukuuliza kama kuna mtu yeyote hapa, mwambie hakuna.” 21Lakini Yaeli, mke wa Heberi, akachukua kigingi cha hema na nyundo, akamwendea polepole akakipigilia kile kigingi cha hema katika paji la uso wake kikapenya mpaka udongoni, kwa maana alikuwa amelala fofofo kwa uchovu. Basi, Sisera akafa papo hapo. 22Naye Baraki alipokuwa anamfuatilia Sisera, Yaeli akatoka nje kumlaki akamwambia, “Njoo nami nitakuonesha yule unayemtafuta.” Baraki akaingia ndani ya hema la Yaeli na kumkuta Sisera chini, amekufa, na kigingi cha hema pajini mwake.
23Hivyo, siku hiyo Mungu akawapa Waisraeli ushindi juu ya mfalme Yabini wa Kanaani. 24Waisraeli wakaendelea kumwandama Yabini, mfalme wa Kanaani, mpaka walipomwangamiza.


Waamuzi 4;1-24

Biblia Habari Njema kwa Watu Wote(BHN)

"Swahili Na Waswahili"Mbarikiwe.

Wednesday 15 November 2017

Kikombe Cha Asubuhi ;Waamuzi 3...




Shalom,Habari za Asubuhi,Hamjambo,Mmeamkaje?

Haleluyah Mungu wetu yu Mwema sana..
Tumshukuru Mungu wetu kwa wema na fadhili zake kwetu..

Asante Baba wa Mbinguni kwa ulinzi wako kwetu wakati wote..
Asante kwakutuchagua na kutupa kibali cha kuendelea kuiona leo hii
Asante kwa mpumzi/uzima,afya na kuwa tayari kwa majukumu yetu..
Utukuzwe Mungu wetu,Usifiwe Baba wa Mbinguni,Uhihidiwe Jehovah,
Uabudiwe Yahweh,Matendo yako ni makuu sana,Matendo yako ni ya ajabu
Sifa na Utukufu tunakurudishia Mungu wetu..!!


Baba wa Mbinguni tunakuja mbele zako tukijinyenyekeza,tukijishusha
na kujiachilia mikononi mwako Yahweh...
Mungu wetu tunaomba utusamehe makosa yetu yote tuliyoyafanya
kwakuwaza,kwakunena,kwakutenda,kwakujua/kutojua...
Jehovah nasi tunaomba utupe neema ya kuweza kuwasamehe
wale wote waliotukosea....
Mungu wetu tunaomba utuepushe katika majaribu
 Baba  utuokoe na yule mwovu na kazi zake zote..
Yahweh tunaomba ututakase miili yetu na akili zetu Jehovah
utufunike kwa Damu ya Bwana na Mwokozi wetu Yesu Kristo wa Nazareti
Yeye aliteseka kwanza ili sisi tupate kupona..

Wastahili sifa, ee Mungu, huko Siyoni, watu watakutimizia wewe ahadi zao, maana wewe wajibu sala zetu. Binadamu wote watakujia wewe. Tunapolemewa na makosa yetu, wewe mwenyewe watusamehe. Heri wale unaowachagua na kuwaleta karibu, waishi katika maskani yako. Sisi tutatoshelezwa na mema ya nyumba yako; mema ya hekalu lako takatifu. Kwa matendo yako makuu watuitikia na kutuokoa, ewe Mungu wa wokovu wetu; wewe ndiwe tumaini la viumbe vyote, duniani kote na mbali baharini. Kwa nguvu yako uliisimika milima mahali pake. Wewe una nguvu mno! Watuliza mshindo wa bahari na wa mawimbi yake, wakomesha ghasia za watu. Ulimwengu wote washangazwa na matendo yako. Wasababisha furaha kila mahali, toka mashariki hata magharibi. Wewe waitunza nchi kwa kuinyeshea mvua, waijalia rutuba na kuistawisha; mto wako umejaa maji tele, waifanikisha nchi na kuipatia mavuno. Hivi ndivyo uitengenezavyo nchi: Mashamba wayanyeshea mvua kwa wingi, na kuyalowanisha kwa maji; ardhi wailainisha kwa manyunyu, na kuibariki mimea ichipue. Wautunukia mwaka wote mema yako, kila ulipopitia pamejaa fanaka. Mbuga za majani zimejaa mifugo, milima nayo imejaa furaha. Malisho yamejaa kondoo, mabonde yamefunikwa kwa ngano. Kila kitu kinashangilia kwa furaha.




Baba wa Mbinguni tunaomba ukabariki kazi za mikono yetu
Mungu wetu ukatupe ubunifu,maarifa katika ufanyaji/utendeji
Yahweh nasi tukatende sawasawa na mapenzi yako..
Jehovah tunaomba ukabariki ridhiki zetu ziingiazo/zitokazo Yahweh
nasi tunaomba utupe neema ya kuweza kuwabariki wenye kuhitaji..
Baba wa Mbinguni tusipungukiwe katika mahitaji yetu Mungu wetu
ukatupe kama inavyokupendeza wewe..



Namngojea Mungu peke yake kwa utulivu; kwake naliweka tumaini langu. Yeye peke yake ndiye mwamba na wokovu wangu, yeye ni ngome yangu, sitatikisika. Wokovu na fahari yangu vyatoka kwa Mungu; mwamba wangu mkuu na kimbilio langu ni Mungu. Enyi watu, mtumainieni Mungu daima; mfungulieni Bwana yaliyo moyoni mwenu. Mungu ndiye kimbilio la usalama wetu. Binadamu wote ni kama pumzi tu; wote, wakubwa kwa wadogo, hawafai kitu. Tena ukiwapima uzito hawafikii kilo, wote pamoja ni wepesi kuliko pumzi. Msitegemee dhuluma, msijisifie mali ya wizi; kama mali zikiongezeka, msizitegemee. Mungu ametamka mara moja, nami nimesikia tena na tena: Kwamba enzi ni mali yake Mungu; naam, nazo fadhili ni zake Bwana; humlipa kila mtu kadiri ya matendo yake.

Mtalme wa amani tunayaweka maisha yetu mikononi mwako..
Baba wa Mbinguni tunaomba ukatawale,ukatamalaki na kutuatamia
Yahweh tunaomba ulinzi wako wakati wote kwetu na kwa vyote
tunavyovimiliki,Mungu wetu ukatupe neema ya kutambua/kujitambu,
kufuata njia zako,kusimamia Neno lako amri na sheria zako siku zote
za maisha yetu,Yahweh tukawe wanyenyekevu kwa watu wote,
wepesi wa kusamehe Baba ukatupe amani ya moyo,upendo wa kweli,
kusaidiana,kuchukuliana,kuonyana/kuelimishana kwa amani na upendo
Mungu wetu ukatufanye barua njema nasi tukasomeke kama
inavyokupendeza wewe..
Roho Mtakatifu akatuongoze katika yote na tukawe na kiasi..




Tunakushukuru, ee Mungu, tunakushukuru! Tunatangaza ukuu wa jina lako na kusimulia juu ya matendo yako makuu. Mungu asema: “Mimi nimeweka wakati maalumu! Wakati huo nitahukumu kwa haki. Nchi ikitetemeka na vyote vilivyomo, mimi ndiye ninayeitegemeza misingi yake. Nawaambia wenye kiburi: ‘Acheni kujigamba’; na waovu: ‘Msioteshe pembe za kiburi! Msijione kuwa watu wa maana sana, wala kusema maneno ya majivuno.’” Hukumu haitoki mashariki au magharibi; wala haitoki nyikani au mlimani. Mungu mwenyewe ndiye hakimu; humshusha mmoja na kumkweza mwingine. Mwenyezi-Mungu, anashika kikombe mkononi, kimejaa divai kali ya hasira yake; anaimimina na waovu wote wanainywa; naam, wanainywa mpaka tone la mwisho. Lakini mimi nitafurahi milele, nitamwimbia sifa Mungu wa Yakobo. Atavunja nguvu zote za watu waovu; lakini nguvu za waadilifu ataziimarisha.

Mungu wetu tunaomba ukawaguse kwa mkono wako wenye nguvu
wote wataabikao na kuelemewa na mizigo,Mungu wetu tunaomba ukawaponye wagonjwa ,wenye njaa ukawapatie chakula,waliokataliwa na kukata tamaa Mungu wetu ukawape tumaini,wanaopita katika magumu/majaribu
Mungu wetu ukawavushe salama,waliokatika vifungo vya yule mwovu
Baba wa Mbinguni ukawafungue na kuwaweka huru,Yahweh ukawape
neema ya kujiombea,kufuata njia zako,ukawape macho ya kuona
na masikio ya kusikia sauti yako na kutii,Baba tunaomba ukapokee
sala/maombi yetu na ukawafute machozi ya watoto wako
wanaokutafuta kwa bidii na imani,Ee Baba utusikie..
Kwakuwa Ufalme ni wako Nguvu na Utukufu hata Milele..
Amina..!

Asanteni sana wapendwa katika Bwana kwakuwa nami
Mungu awe nanyi daima na msipungukiwe katika mahitaji yenu
Baba wa Mbinguni akawape sawasawa na mapenzi yake..
Nawapenda.

1Mwenyezi-Mungu aliyaacha nchini mataifa yafuatayo ili kuwajaribu Waisraeli ambao walikuwa hawajapigana vita katika nchi ya Kanaani 2(alifanya hivyo ili awape watu wa vizazi hivyo ujuzi wa kupigana kwani hawakuwa wameona vita): 3Wakuu watano wa Wafilisti, Wakanaani wote, Wasidoni na Wahivi waliohamia katika milima ya Lebanoni kutoka mlima Baal-hermoni mpaka kufikia Hamathi. 4Mwenyezi-Mungu alikusudia kuwatumia hao ili awajaribu Waisraeli, aone kama watatii amri zake alizowaamuru wazee wao kwa njia ya Mose. 5Basi, Waisraeli waliishi pamoja na Wakanaani, Wahiti, Waamori, Waperizi, Wahivi na Wayebusi. 6Wakaoa binti zao na kuoza binti zao kwa vijana wa mataifa hayo na kuiabudu miungu yao.
Othnieli
7Waisraeli walitenda uovu mbele ya Mwenyezi-Mungu; wakamsahau Mwenyezi-Mungu, Mungu wao, wakaabudu Mabaali na Maashera. 8Basi, hasira ya Mwenyezi-Mungu ikawaka dhidi ya Israeli, naye akawatia mikononi mwa Kushan-rishathaimu mfalme wa Mesopotamia, nao wakamtumikia kwa muda wa miaka minane. 9Waisraeli wakamlilia Mwenyezi-Mungu, naye akawapelekea mtu wa kuwakomboa yaani, Othnieli mwana wa Kenazi, ndugu mdogo wa Kalebu. 10Basi, roho ya Mwenyezi-Mungu ikamjia Othnieli, naye akawa mwamuzi wa Waisraeli. Othnieli alikwenda vitani naye Mwenyezi-Mungu akamtia Kushan-rishathaimu mfalme wa Mesopotamia mikononi mwake. 11Hivyo nchi ikawa na amani kwa muda wa miaka arubaini. Kisha Othnieli mwana wa Kenazi, akafariki.
Ehudi
12Waisraeli walitenda tena uovu mbele ya Mwenyezi-Mungu. Mwenyezi-Mungu akampa nguvu mfalme Egloni wa Moabu awashambulie Waisraeli, kwa sababu walitenda uovu mbele ya Mwenyezi-Mungu. 13Egloni akawakusanya Waamoni na Waamaleki, akaenda kupigana na Waisraeli, akawashinda. Akauteka Mji wa Mitende yaani Yeriko. 14Waisraeli wakamtumikia Egloni mfalme wa Moabu, kwa muda wa miaka kumi na minane.
15Lakini Waisraeli walipomlilia Mwenyezi-Mungu, yeye aliwapelekea mtu wa kuwakomboa, yaani Ehudi mwana wa Gera, mwenye mkono wa shoto, wa kabila la Benyamini.
Waisraeli walimtuma apeleke zawadi zao kwa Egloni mfalme wa Moabu. 16Ehudi akajitengenezea upanga wenye makali kuwili; urefu wake sentimita hamsini. Akaufunga kiunoni mwake upande wa kulia ndani ya mavazi yake. 17Kisha akampelekea Egloni zile zawadi. Egloni alikuwa mtu mnene sana. 18Ehudi alipomaliza kutoa zawadi, akawaambia watu waliobeba zawadi, waondoke. 19Lakini yeye alipofika kwenye sanamu za mawe yaliyochongwa karibu na Gilgali, alimrudia Egloni akasema, “Nina ujumbe wa siri kwako, ee mfalme.” Mfalme akawaamuru watumishi wakae kimya, nao wakatoka nje. 20Naye Ehudi akamkaribia pale alipokaa katika chumba chake chenye baridi barazani, akamwambia “Nina ujumbe wako kutoka kwa Mungu.” Mfalme akainuka kitini mwake na kusimama. 21Ehudi akauchomoa upanga wake kwa mkono wake wa kushoto kutoka paja lake la kulia, akamchoma nao tumboni mwake. 22Upanga ukaingia ndani pamoja na mpini wake, mafuta yakaufunika upanga huo kwani Ehudi hakuutoa tena; ukawa umetokea kwa nyuma.3:22 ukawa umetokea kwa nyuma: Maana ya neno la Kiebrania si dhahiri. 23Kisha, Ehudi akatoka nje barazani baada ya kuifunga milango ya chumba hicho kwa ufunguo.
24Ehudi alipoondoka, watumishi wa mfalme wakarudi. Walipoona milango yote ya chumba imefungwa, walifikiri amekwenda kujisaidia chooni humo ndani ya nyumba. 25Wakangojea mpaka wakaanza kuwa na wasiwasi. Walipoona hafungui, wakachukua ufunguo na kufungua mlango. Wakamwona mfalme wao sakafuni, naye amekufa.
26Walipokuwa wanangoja, Ehudi alitoroka akipitia kwenye sanamu za mawe, akaenda Seira. 27Alipofika huko alipiga tarumbeta katika nchi ya milima ya Efraimu, nao Waisraeli wakateremka pamoja naye kutoka huko milimani naye akawatangulia. 28Akawaambia, “Mnifuate, maana Mwenyezi-Mungu amewatia adui zenu Wamoabu mikononi mwenu.” Wakamfuata mpaka kivuko cha Yordani na kukiteka toka mikononi mwa Wamoabu, wakazuia mtu yeyote kupita. 29Siku hiyo, wakawaua Wamoabu wapatao 10,000; watu wote wenye afya na nguvu, wala hakuna hata mmoja aliyenusurika. 30Siku hiyo Waisraeli wakawashinda Wamoabu. Nchi ikawa na amani kwa muda wa miaka themanini.
Shamgari
31Baada ya Ehudi mwana wa Anati, Shamgari alishika nafasi yake. Yeye aliwaua Wafilisti 600 kwa fimbo ya kuchungia ng'ombe. Naye pia aliwakomboa Waisraeli.


Waamuzi 3;1-31

Biblia Habari Njema kwa Watu Wote(BHN)

"Swahili Na Waswahili"Mbarikiwe.

Tuesday 14 November 2017

Kikombe Cha Asubuhi ;Waamuzi 2...



Shalom,Habari za Asubuhi,Hamjambo,Mmeamkaje?

Tumshukuru Mungu wetu katika yote..

Mtakatifu..!Mtakatifu..!Mtakatifu.!Baba wa Mbinguni..
Mungu wetu,Muumba wetu,Mungu wa Abrahamu,Isaka na Yakobo..
Mungu wa Wajane,Baba wa Yatima,Muweza wa yote,Mponyaji wetu,
Utukuzwe Yahweh,Usifiwe Baba wa Mbinguni,Uabudiwe Jehovah,
Uhimidiwe Mungu wetu,Unatosha Baba wa Mbinguni,Hakuna kama wewe
wewe ni alfa na Omega,wewe ni mwanzo na wewe ni mwisho..!

Ndugu zangu, ninataka na kutazamia kwa moyo wangu wote hao wananchi wenzangu wakombolewe. Tena nawaombea kwa Mungu daima. Maana naweza kuthibitisha kwa niaba yao kwamba wanayo bidii ya kumtafuta Mungu; lakini bidii hiyo haikujengwa juu ya ujuzi wa kweli. Maana hawakufahamu jinsi Mungu anavyowafanya watu wawe waadilifu, na wamejaribu kuanzisha mtindo wao wenyewe na hivyo hawakuikubali njia hiyo ya Mungu ya kuwafanya wawe waadilifu. Maana kwa kuja kwake Kristo, sheria imefikia kikomo chake, ili wote wanaoamini wafanywe waadilifu.
Baba wa Mbinguni tunakuja mbele zako tukijinyenyekeza,tukijishusha na
kujiachilia mikononi mwako Yahweh..
Tunaomba utusamehe makosa yetu yote tuliyoyafanya kwakuwaza,
kwakunena,kwakutenda,kwakujua/kutojua Mungu wetu..
Tunaomba nasi utupe neema ya kuweza kuwasamehe wale wote
waliotukosea..
Jehovah tunaomba utuepushe katika majaribu Baba utuokoe na yule
mwovu na kazi zake zote..
Mungu wetu tunaomba ututakase miili yetu na akili zetu
Yahweh utufunike kwa Damu ya Bwana na Mwokozi wetu
 Yesu Kristo wa Nazareti..
Yeye aliteseka kwanza ili sisi tupate kupona..



Kuhusu kuwa mwadilifu kwa kuitii sheria, Mose aliandika hivi: “Mtu yeyote anayetimiza matakwa ya sheria ataishi.” Lakini kuhusu kuwa mwadilifu kwa njia ya imani, yasemwa hivi: “Usiseme moyoni mwako: ‘Nani atapanda mpaka mbinguni?’ (yaani, kumleta Kristo chini); wala usiseme: ‘Nani atashuka mpaka kuzimu?’ (yaani, kumleta Kristo kutoka kwa wafu).” Maandiko Matakatifu yasema hivi: “Ujumbe huo wa Mungu uko karibu nawe, uko kinywani mwako na moyoni mwako” nao ndio ile imani tunayoihubiri. Kama ukikiri kwa kinywa chako kwamba Yesu ni Bwana na kuamini moyoni mwako kwamba Mungu alimfufua kutoka kwa wafu, utaokoka. Maana mtu huamini kwa moyo akafanywa mwadilifu; na hukiri kwa kinywa akaokolewa. Maandiko Matakatifu yasema: “Kila anayemwamini hataaibishwa.” Jambo hili ni kwa wote, kwani hakuna tofauti kati ya Wayahudi na wasio Wayahudi; Bwana wa wote ni mmoja, naye ni mkarimu sana kwao wote wamwombao. Maana Maandiko Matakatifu yasema: “Kila mtu atakayeomba kwa jina la Bwana, ataokolewa.”

Mungu wetu tunaomba ukabariki kazi za mikono yetu,Jehovah
ukatupe ubunifu,maarifa katika ufanyaji/utendaji Yahweh
nasi tukatende sawasawa na mapenzi yako..
Baba wa Mbinguni tunaomba ukabariki ridhiki zetu ziingiazo/zitokazo
Jehovah nasi tunaomba utupe neema ya kuweza kuwabariki
wenye kuhitaji,Mungu wetu tusipungukiwe katika mahitaji yetu
Yahweh ukatupe sawasawa na mapenzi yako...

Mfalme wa amani tunaomba amani yako ikatawale katika nyumba/ndoa
zetu,watoto/wazazi wetu,familia/ndugu na wote wanaotuzunguka..
Yahweh tunaomba ulinzi wako kwetu na kwa vyote tunavyovimiliki
Mungu wetu ukatubariki,ukatamalaki na kutuatamia,Jehovah ukatupe
neema ya kufuata njia zako,kusimamia Neno lako amri na sheria zako siku zote za maisha yetu,Nuru yako ikaangaze katika maisha yetu Baba ukatuepushe na roho za kiburi,kujiona kujisifu,Mungu wetu na vyote vinavyokwenda kinyume nawe..
Jehovah ukatufanye chombo chema nasi tukatumike kama inavyokupenda wewe..
Roho Mtakatifu akatuongoze katika yote na tukawe na kiasi..

Basi, watamwombaje yeye ambaye hawamwamini? Tena, watamwaminije kama hawajapata kusikia habari zake? Na watasikiaje habari zake kama hakuna mhubiri? Na watu watahubirije kama hawakutumwa? Kama yasemavyo Maandiko Matakatifu: “Ni jambo la kupendeza mno kuja kwa wale wanaohubiri Habari Njema!” Lakini wote hawakuipokea hiyo habari njema. Maana Isaya alisema: “Bwana, ni nani aliyeamini ujumbe wetu?” Hivyo basi, imani inatokana na kuusikia ujumbe, na huo ujumbe unatokana na neno la Kristo. Lakini nauliza: Je, hawakuusikia huo ujumbe? Naam, waliusikia; kama Maandiko Matakatifu yasemavyo: “Sauti yao imeenea duniani kote; maneno yao yamefika mpaka kingo za ulimwengu.” Tena nauliza: Je, yawezekana kwamba watu wa Israeli hawakufahamu? Mose mwenyewe ni wa kwanza kujibu: “Nitawafanyeni muwaonee wivu watu ambao si taifa; nitawafanyeni muwe na hasira juu ya taifa la watu wapumbavu.” Tena Isaya anathubutu hata kusema: “Wale ambao hawakunitafuta wamenipata; nimejionesha kwao wasiouliza habari zangu.” Lakini kuhusu Israeli anasema: “Mchana kutwa niliwanyoshea mikono yangu watu waasi na wasiotii.”


Tazama wenye shida/tabu Mungu wetu, Tunaomba ukawaguse na mkono wako wenye nguvu,wagonjwa wakapate uponyaji wako,wenye njaa ukawapatie chakula,wanaopitia magumu/majaribu ukawavushe Mungu wetu,walio katika vifungo vya yule mwovu ukawafungue Jehovah ukawape neema ya kujiombea,kufuata njia zako,Nuru ikaangaze katika
maisha yao,wakapate uponyaji wa mwili na roho pia...

Sifa na utukufu tunakurudishia Mungu wetu..
Kwakuwa Ufalme ni wako Nguvu na Utukufu hata Milele
Amina..!

Asanteni sana wapendwa/waungwana kwakunisoma
Mungu aendelee kuwatendea kama inavyompendeza yeye
Amani,Upendo na Baraka ziwe nanyi siku zote..
Nawapenda.

Mwenyezi-Mungu anawagombeza watu wake

1Malaika wa Mwenyezi-Mungu aliondoka Gilgali, akaenda Bokimu, akawaambia Waisraeli, “Niliwatoa nchini Misri na kuwaleta katika nchi ambayo niliwaahidi kwa kiapo babu zenu. Nilisema kwamba sitalivunja agano langu nanyi kamwe. 2Na kwa upande wenu niliwaamuru msifanye agano na wenyeji wa nchi hii na kwamba madhabahu zao mtazibomoa. Lakini nyinyi hamkuitii amri yangu. Kwa nini mambo haya? 3Kwa hiyo sasa nasema: Sitawafukuza tena wakazi wa nchi hii bali watawataabisha, nayo miungu yao itakuwa mtego kwenu.” 4Malaika wa Mwenyezi-Mungu alipowaambia watu wote wa Israeli maneno haya, walipaza sauti zao na kulia. 5Wakapaita mahali hapo Bokimu.2:5 Bokimu: Jina hili katika Kiebrania linamaanisha “Wanaolia”. Hapo wakamtolea sadaka Mwenyezi-Mungu.

Kifo cha Yoshua

6Baada ya Yoshua kuwaaga Waisraeli, kila mmoja alikwenda kwenye eneo lake alilogawiwa ili kuimiliki nchi. 7Waisraeli walimtumikia Mwenyezi-Mungu siku zote za maisha ya Yoshua na baada ya kifo chake muda wote walioishi wale wazee waliosalia ambao waliyaona matendo makuu ambayo Mwenyezi-Mungu aliwatendea Waisraeli. 8Yoshua mwana wa Nuni na mtumishi wa Mwenyezi-Mungu, alifariki akiwa na umri wa miaka 110. 9Wakamzika katika sehemu aliyogawiwa iwe yake huko Timnath-heresi, katika nchi ya milima ya Efraimu kaskazini ya mlima Gaashi. 10Kisha watu wote wa kizazi chake walifariki, kikafuata kizazi kingine ambacho hakikumjua Mwenyezi-Mungu wala matendo aliyowatendea watu wa Israeli.

Waisraeli wanamwasi Mwenyezi-Mungu

11Basi, Waisraeli walitenda uovu mbele ya Mwenyezi-Mungu na kuabudu Mabaali. 12Walimwacha Mwenyezi-Mungu, Mungu wa wazee wao, ambaye aliwatoa katika nchi ya Misri, wakaifuata miungu mingine, miungu iliyoabudiwa na watu walioishi kandokando yao. Waliisujudia miungu hiyo, wakamkasirisha sana Mwenyezi-Mungu. 13Walimwacha Mwenyezi-Mungu, wakatumikia Mabaali na Maashtarothi. 14Basi, hasira ya Mwenyezi-Mungu iliwaka dhidi ya Israeli, naye akawaacha wanyanganyi wapore mali zao. Aliwakabidhi kwa adui zao waliowazunguka hata wasiweze tena kuwapinga. 15Kila walipokwenda kupigana, mkono wa Mwenyezi-Mungu uliwakabili kuwaletea balaa, kama alivyokuwa amewaonya na kuapa. Nao wakawa katika huzuni kubwa.
16Ndipo Mwenyezi-Mungu akawapa waamuzi ambao waliwaokoa mikononi mwa watu waliopora mali zao. 17Hata hivyo, Waisraeli hawakuwasikiliza waamuzi wao, maana walifanya kama wazinzi kwa kufuata miungu mingine na kuisujudia. Waliacha upesi nyayo walizofuata babu zao ambao walitii amri za Mwenyezi-Mungu; bali wao hawakufanya hivyo. 18Kila mara Mwenyezi-Mungu alipowapelekea mwamuzi, yeye mwenyewe alikuwa pamoja na mwamuzi huyo, akawaokoa mikononi mwa adui zao muda wote wa uhai wa mwamuzi huyo. Aghalabu, Mwenyezi-Mungu aliwaonea huruma aliposikia kilio chao kutokana na mateso na dhuluma walizofanyiwa. 19Lakini kila mara mwamuzi alipofariki walirudia mienendo yao ya zamani, wakaishi vibaya kuliko babu zao. Waliifuata miungu mingine, wakaitumikia na kuisujudia, wala hawakuyaacha matendo yao wala ukaidi wao. 20Kwa hiyo Mwenyezi-Mungu akawaka hasira dhidi ya Waisraeli, akasema, “Kwa kuwa watu hawa wamevunja agano nililofanya na babu zao, wakakataa kutii sauti yangu, 21sitayafukuza tena mataifa ambayo Yoshua aliyabakiza, wakati alipofariki. 22Nitayatumia mataifa hayo kuwajaribu Waisraeli nione kama watairudia njia yangu kama babu zao au sivyo.” 23Basi, Mwenyezi-Mungu akayaacha mataifa hayo, wala hakuyafukuza mara moja, wala hakumpa Yoshua ushindi juu ya mataifa hayo!

Waamuzi 2;1-23

Biblia Habari Njema kwa Watu Wote(BHN)

"Swahili Na Waswahili"Mbarikiwe.

Monday 13 November 2017

Kikombe Cha Asubuhi ;Tumemaliza kitabu cha Yoshua na Leo Tunaanza Kitabu cha Waamuzi 1...




Shalom,Habari za Asubuhi,Hamjambo,Mmeamkaje?

Wapendwa/Waungwana tunamshukuru Mungu kwa kutuwezesha
kumaliza kupitia/kusoma kitabu cha "YOSHUA"
Natumaini tumejifunza na kuongeza kitu...
Leo tunaanza kitabu cha "WAAMUZI"Tunaomba Mungu akatuongoze
vyema katika kusoma na tukaelewe na kufuata yaliyomo na tukasimamie
Neno lake na likawe msaada kwetu na kwa  wengine..
Ee Mungu tusaidie tukawe na kiu/shauku ya kusoma zaidi na kuzingatia


Kama ukiwapa ndugu wote maagizo haya, utakuwa mtumishi mwema wa Kristo Yesu, ukijiendeleza kiroho kwa maneno ya imani na mafundisho ya kweli ambayo wewe umeyafuata. Lakini achana na hadithi zile zisizo za kidini na ambazo hazina maana. Jizoeshe kuishi maisha ya uchaji wa Mungu. Mazoezi ya mwili yana faida yake, lakini mazoezi ya kiroho yana faida za kila namna, maana yanatuahidia uhai katika maisha ya sasa, na pia hayo yanayokuja. Usemi huo ni wa kusadikika kabisa na unastahili kukubaliwa. Sisi tunajitahidi na kufanya kazi kwa bidii kwani tumemwekea tumaini letu Mungu aliye hai ambaye ni Mwokozi wa watu wote, na hasa wale wanaoamini. Wape maagizo hayo na mafundisho hayo. Usikubali mtu yeyote akudharau kwa sababu wewe ni kijana, lakini jitahidi uwe mfano kwa wanaoamini: Katika usemi wako, mwenendo wako, upendo, imani na maisha safi. Tumia wakati wako na juhudi yako katika kusoma hadharani Maandiko Matakatifu, kuhubiri na kufundisha, mpaka nitakapokuja. Usiache kukitumia kile kipaji cha Kristo ndani yako ulichopewa kwa maneno ya manabii na kwa kuwekewa mikono na wazee. Fikiri kwa makini juu ya hayo yote na kuyatekeleza kusudi maendeleo yako yaonekane na wote. Angalia sana mambo yako mwenyewe na mafundisho yako. Endelea kufanya hayo, maana ukifanya hivyo, utajiokoa mwenyewe na wale wanaokusikiliza.
Haleluyah Mungu wetu yu mwema sana tunamshukuru
katika yote...
Asante Mungu wetu Baba yetu,Muumba wetu,Muumba wa Mbingu
Nchi na vyote vilivyomo,vinavyoonekana na visivyoonekana..
Mungu wa Abrahamu,Isaka na Yakobo,Mungu wa wote walio hai..
Muweza wa yote,Baba wa upendo,Mungu wenye huruma,Mponyaji
Jehovah Jireh,Jehovah Nissi,Jehovah Rapha,Jehovah Raah,Jehovah Shammah,Jehovah Shalom,Emanueli-Mungu pamoja nasi..
Unastahili Sifa,Unastahili kutukuzwa,Unastahili kuabudiwa,
Unastahili kuhimidiwa,Unastahili ee Baba...!Unatosha Mungu wetu..



Basi, ikiwa mmefufuka pamoja na Kristo, panieni mambo ya juu, kule Kristo aliko, ameketi upande wa kulia wa Mungu. Muwe na hamu ya mambo ya huko juu, na siyo mambo ya hapa duniani. Maana nyinyi mmekufa na uhai wenu umefichwa pamoja na Kristo katika Mungu. Uhai wenu halisi ni Kristo, na wakati atakapotokea ndipo nanyi pia mtakapotokea pamoja naye katika utukufu.
Asante kwa kwa ulinzi wako wakati wote Mungu wetu..
Asante kwa kutuchagua na kutupa kibali cha kuendelea kuiona leo hii
Asante kwa pumzi/uzima,afya na kuwa tayari katika majukumu yetu..

Tunakuja mbele zako Mungu wetu tukijinyenyekeza,tukijishusha na kujiachilia mikononi mwako Mungu wetu..
Tunaomba utusamehe dhambi zetu zote tulizozifanya
kwakuwaza,kwakunena,kwakutenda,kwakujua/kutojua..
Mungu wetu nasi tunaomba utupe neema ya kuweza kuwasamehe wale wote waliotukosea..
Mungu wetu tunaomba utuepushe katika majaribu Baba utuokoe na
yule mwovu na kazi zake zote..
Yahweh tunaomba ututakase miili yetu na akili zetu Mungu wetu
tunaomba utufunike kwa Damu ya Bwana na Mwokozi wetu
Yesu Kristo wa Nazareti,Yeye aliteseka kwanza ili sisi tupate kupona..
Mungu wetu tunaomba ukabariki kazi za mikono yetu,Baba ukatupe
ubunifu,maarifa katika kufanya/kutenda nasi tukatende sawasawa
na mapenzi yako,Yahweh tunaomba ukabariki ridhiki zetu
ziingiazo/zitokazo,Mungu wetu nasi tunaomba utupe neema ya
kuweza kuwabariki wenye kuhitaji..
Tusipungukiwe katika mahitaji yetu,Jehovah ukatupe
sawasawa na mapenzi yako...



Basi, ueni chochote kilicho ndani yenu ambacho ni cha kidunia: Uasherati, uchafu, shauku, tamaa mbaya na uchu (ambao ni sawa na kuabudu sanamu). Kwa sababu ya mambo hayo hasira ya Mungu huwajia wote wanaomwasi. Wakati mmoja nyinyi pia mliishi kufuatana na mambo hayo, mlipotawaliwa nayo. Lakini sasa mnapaswa kuachana na mambo haya yote: Hasira, tamaa na uovu; kufuru au maneno yasiyofaa yasitoke kamwe vinywani mwenu. Msiambiane uongo, kwani nyinyi mmekwisha vua ule utu wa kale pamoja na matendo yake yote, mkavaa utu mpya. Huu unaendelea kurekebishwa na Mungu, Muumba wake, kadiri ya mfano wake, ili mpate kumjua Mungu kwa ukamilifu. Katika hali hii, hakuna tena tofauti kati ya Mgiriki na Myahudi, aliyetahiriwa na asiyetahiriwa, msomi na asiye msomi, mtumwa na mtu aliye huru. Kristo ni kila kitu, na yumo katika yote. Nyinyi ni watu wake Mungu; yeye aliwapenda na kuwateua. Kwa hiyo, basi, vaeni moyo wa huruma, wema, unyenyekevu, upole na uvumilivu. Vumilianeni na kusameheana iwapo mmoja wenu analo jambo lolote dhidi ya mwenzake. Mnapaswa kusameheana kama Bwana alivyowasamehe nyinyi. Zaidi ya hayo yote, zingatieni upendo, kwani upendo huunganisha kila kitu katika umoja ulio kamili. Nayo amani ya Kristo itawale mioyoni mwenu; maana kwa ajili hiyo nyinyi mmeitwa katika mwili huo mmoja. Tena muwe na shukrani! Ujumbe wa Kristo na ukae ndani yenu pamoja na utajiri wake wote. Fundishaneni na kushauriana kwa hekima yote. Imbeni Zaburi, nyimbo na tenzi za kiroho; mwimbieni Mungu mioyoni mwenu kwa shukrani. Na, kila mfanyacho kwa neno au tendo, fanyeni vyote kwa jina la Bwana Yesu na kumshukuru Mungu Baba kwa njia yake.
Mfalme wa amani tunaomba amani yako ikatawale katika
nyumba/ndoa zetu,watoto,wazazi wetu,familia/ndugu na wote
wanaotuzunguka,Mungu wetu ukaonekane katika maisha yetu
Yahweh tunaomba ulinzi wako kwetu na kwa vyote tunavyo vimiliki
Baba tunaomba ukatubariki na ukatupe neema ya kusimamia
Neno lako,amri na sheria zako siku zote za maisha yetu..
Ukatufanye chombo chema Mungu wetu nasi tukatumike kama
inavyokupendeza wewe..
Roho Mtakatifu akatuongoze katika yote na tukawe na kiasi..


Lakini wewe, mtu wa Mungu, jiepushe na mambo hayo. Zingatia uadilifu, uchaji wa Mungu, imani, upendo, subira na unyenyekevu. Piga mbio kadiri uwezavyo katika shindano la mbio za imani, ukajipatie tuzo la uhai wa milele uliloitiwa wakati ulipokiri imani yako mbele ya mashahidi wengi. Mbele ya Mungu anayevipa vitu vyote uhai, na mbele ya Yesu Kristo aliyetoa ushahidi na kukiri ukweli mbele ya Pontio Pilato, nakuamuru ushike maagizo yako na kuyatii kwa uaminifu mpaka siku ile atakapotokea Bwana wetu Yesu Kristo. Kutokea kwake kutafanyika wakati ufaao uliopangwa na Mungu mwenye heri na aliye Mtawala pekee, Mfalme wa wafalme, na Bwana wa mabwana. Yeye peke yake anaishi milele katika mwanga usioweza kukaribiwa na mtu. Hakuna mtu aliyepata kumwona au awezaye kumwona. Kwake iwe heshima na uwezo wa milele! Amina. Waamuru watu walio matajiri katika mambo ya maisha ya sasa, wasijivune, wasiweke tumaini lao katika mali isiyoweza kutegemewa; bali wamtegemee Mungu, ambaye kwa ukarimu hutupatia vitu vyote tuvifurahie. Waamuru watende mema, wawe matajiri katika matendo mema, na wawe wakarimu na walio tayari kuwashirikisha wengine mali zao. Kwa namna hiyo watajiwekea hazina ambayo itakuwa kwao msingi imara kwa wakati ujao. Hapo wataweza kujipatia uhai ambao ni uhai wa kweli. Timotheo, tunza salama yote yale uliyokabidhiwa. Jiepushe na majadiliano ya kidunia na ubishi wa kipumbavu juu ya kile wanachokiita watu wengine “Elimu.” Maana wengine wamejidai kuwa na hiyo elimu, na matokeo yake wamepoteza imani. Nawatakieni nyote neema!

Mungu wetu ukawaguse kwa mkono wako wenye nguvu
wagonjwa,ukawape uponyaji,wenye njaa ukawape chakula
na ukabariki mashamba yao wakapate mavuno mengi na
wakawe na akiba,waliokatika magumu/majaribu Baba wa
Mbinguni tunaomba ukawavushe salama,waliokatika vifungo
mbalimbali Mungu wetu tunaomba ukawafungue na ukawape
wote neema ya kujiombea,kufuata njia zako ukawaweke huru
na Nuru yako ikaangaze katika maisha yao..
Wafiwa ukawe mfariji wao..
Kwa imani tunayaweka haya yote mikononi mwako
Kwakuwa Ufalme ni wako Nguvu na Utukufu Hata Milele..
Amina..!

Asanteni sana wapendwa katika Bwana kwa kuwa nami
Mungu aendelee kuwabariki na Upendo wa Kristo
Amani na furaha iwe nanyi Daima..
Nawapenda.



Waisraeli baada ya kifo cha Yoshua

1Baada ya kifo cha Yoshua, Waisraeli walimwuliza Mwenyezi-Mungu: “Mwenyezi-Mungu, ni kabila gani litakwenda kupigana kwanza na Wakanaani?” 2Mwenyezi-Mungu akawajibu, “Kabila la Yuda litakwenda kupigana nao kwanza, maana nimeitia nchi hiyo mikononi mwao.” 3Watu wa kabila la Yuda wakawaambia ndugu zao, watu wa kabila la Simeoni, “Shirikianeni nasi tunapokwenda kuitwaa nchi hiyo ambayo tumepewa. Nasi, pia tutashirikiana nanyi kwenda kuitwaa nchi mtakayopewa.” Hivyo kabila la Simeoni likakubali kushirikiana nao. 4Basi, watu wa kabila la Yuda wakaenda kufanya mashambulio, naye Mwenyezi-Mungu akawatia Wakanaani na Waperizi mikononi mwao, wakawaua watu 10,000 katika vita huko Bezeki. 5Katika mji huo walimkuta mfalme Adoni-bezeki, wakapigana naye na kuwashinda Wakanaani na Waperizi. 6Adoni-bezeki akakimbia, lakini walimfuatia, wakamkamata, wakamkata vidole gumba vya mikono na miguu. 7Adoni-bezeki akasema, “Wafalme sabini waliokatwa vidole gumba vya mikono na miguu waliokota makombo chini ya meza yangu. Sasa Mungu amenilipa kama nilivyotenda.” Wakampeleka Yerusalemu, akafia huko.
8Watu wa kabila la Yuda waliushambulia mji wa Yerusalemu na kuuteka. Waliwaua wakazi wake kwa mapanga na kuuteketeza mji kwa moto. 9Baadaye, watu wa kabila la Yuda walikwenda kupigana na Wakanaani walioishi kwenye nchi ya milima, Negebu na kwenye nchi tambarare. 10Waliwashambulia pia Wakanaani walioishi katika mji wa Hebroni ambao hapo awali uliitwa Kiriath-arba, wakashinda makabila ya Sheshai, Himani na Talmai.
11Kutoka huko watu wa kabila la Yuda walikwenda kuushambulia mji wa Debiri; ambao hapo awali uliitwa Kiriath-seferi. 12Kalebu akatangaza: “Mtu yeyote atakayefaulu kuuteka mji wa Kiriath-seferi, nitamwoza binti yangu Aksa.” 13Basi, Othnieli, mwana wa Kenazi na mdogo wake Kalebu, akauteka, naye Kalebu akamtoa bintiye Aksa aolewe na Othnieli. 14Aksa alipowasili kwa Othnieli, akamwambia Othnieli amwombe Kalebu baba yake shamba. Aksa alikuwa amepanda punda na aliposhuka chini baba yake alimwuliza, “Ungependa nikupe nini?” 15Akamjibu, “Nipe zawadi! Naomba unipe chemchemi za maji kwani eneo ulilonipa huko Negebu ni kavu.” Kalebu akampa chemchemi za juu na za chini.
16Wazawa wa Keni ambaye alikuwa baba mkwe wa Mose, walifuatana na watu wa kabila la Yuda kutoka Mji wa Mitende yaani mji wa Yeriko, mpaka jangwa la Yuda karibu na Aradi, wakafanya makao yao huko pamoja na watu wa Yuda.1:16 watu wa Yuda: Pengine Waamaleki. 17Watu wa kabila la Yuda walishirikiana na ndugu zao, watu wa kabila la Simeoni, wakawashinda Wakanaani waliokaa Sefathi. Waliuangamiza kabisa mji huo na kugeuza jina lake kuwa Horma.1:17 Horma: Jina hili katika Kiebrania linamaanisha “maangamizi”. 18Watu wa kabila la Yuda pia waliteka miji ya Gaza na eneo lake, Ashkeloni na eneo lake, na Ekroni na eneo lake. 19Mwenyezi-Mungu alikuwa pamoja na watu wa kabila la Yuda, nao wakaiteka nchi ya milima. Lakini hawakuweza kuwashinda wenyeji wa nchi tambarare kwa sababu magari yao ya vita yalikuwa ya chuma. 20Mji wa Hebroni ukakabidhiwa kwa Kalebu kufuatana na maagizo ya Mose. Kalebu akazifukuza kutoka huko koo tatu za Anaki. 21Lakini watu wa kabila la Benyamini hawakuwafukuza Wayebusi waliokaa mjini Yerusalemu; ndiyo maana Wayebusi wanakaa pamoja na watu wa kabila la Benyamini mjini Yerusalemu mpaka leo.
22Watu wa makabila ya Yosefu waliushambulia mji wa Betheli, naye Mwenyezi-Mungu alikuwa pamoja nao. 23Kwanza walikuwa wamewatuma wapelelezi kwenda kuupeleleza mji wa Betheli. Mji huo hapo awali uliitwa Luzu. 24Wapelelezi hao walimwona mtu mmoja akitoka mjini, wakamwambia, “Tafadhali, tuoneshe njia inayoingia mjini, nasi tutakutendea kwa wema.” 25Akawaonesha njia ya kuingia mjini. Basi, wakaingia na kuangamiza kila mtu aliyekuwamo. Lakini wakamwacha salama mtu huyo na jamaa yake. 26Mtu huyo akahamia nchi ya Wahiti, huko akajenga mji ambao aliuita Luzu; na mji huo unaitwa hivyo mpaka leo.
27Watu wa kabila la Manase hawakuwafukuza wakazi wa miji ya Beth-sheani na vijiji vyake, Taanaki na vijiji vyake, Dori na vijiji vyake, Ibleamu na vijiji vyake, na Megido pamoja na vijiji vyake. Wakanaani waliendelea kukaa huko. 28Hata Waisraeli walipokuwa na nguvu hawakuwafukuza Wakanaani bali waliwapa kazi za kulazimishwa.
29Watu wa kabila la Efraimu hawakuwafukuza Wakanaani walioishi huko Gezeri, na hawa waliishi huko pamoja na watu wa Efraimu.
30Watu wa kabila la Zebuluni hawakuwafukuza wakazi wa mji wa Kitroni, wala wale wa mji wa Nahalali, waliendelea kukaa pamoja nao wakiwafanyiza kazi za kulazimishwa.
31Watu wa kabila la Asheri hawakuwafukuza wakazi wa miji ya Ako, Sidoni, Alabu, Akzibu, Helba, Afeka na Rehobu. 32Watu wa kabila la Asheri walikaa pamoja na Wakanaani wenyeji wa nchi hiyo kwani hawakuwafukuza.
33Watu wa kabila la Naftali hawakuwafukuza wakazi wa mji wa Beth-shemeshi au wakazi wa Beth-anathi, lakini walikaa pamoja nao. Hata hivyo wenyeji wa miji hiyo, walilazimishwa kuwafanyia Waisraeli kazi za kulazimishwa.
34Waamori waliwafukuzia watu wa kabila la Dani milimani. Hawakuwaruhusu kuja kuishi katika nchi tambarare. 35Waamori waliendelea kuishi katika miji iliyokuwa katika kilima cha Heresi, Aiyaloni na Shaalbimu. Lakini watu wa makabila ya Manase na Efraimu waliwatawala Waamori na kuwafanya wafanye kazi za kulazimishwa. 36Mpaka wa Waamori ulikuwa kaskazini ya Sela, kupitia pitio la Akarimu.


Waamuzi 1;1-36

Biblia Habari Njema kwa Watu Wote(BHN)

"Swahili Na Waswahili"Mbarikiwe.