Swahili na Waswahili

Swahili na Waswahili
Waswahili na Mswahili Rachel Siwa...Pamoja Daima!!

Thursday 3 January 2013

Afya na Jamii;na Mswahili John Haule-Refusha maisha kwa MAJI!!!!!!!!


Refusha maisha kwa MAJI

Hivi karibuni kumetokea uhaba mkubwa wa maji duniani. Kwa wale tuliozaliwa miaka ya sabini na kurudi nyuma tulishuhudia watoto wakiogelea katika mabwawa yaliyokuwa yamezagaa nchi nzima, mito ilikuwa imejaa mpaka watoto walikuwa wakizama na kufa maji, mabomba yalikuwa yakitoa maji safi na yenye uhakika kila nyumba kwa vile huko yalikokuwa yakitoka kulikuwa kuna chemchem zenye uhakika wa kutoa neema ya maji safi pia kwa wakazi wa vijijini.

Maji yanauzwa:
Nyumba za vijijini kama kawaida zilikuwa na mitungi mikubwa ya kuwekea maji na juu yake kuliwekwa kata ya kuchotea na kunywea maji hayo ambayo yalikuwa na harufu na ladha nzuri ya ajabu isiyoelezeka labda msomaji wangu unisaidie kuielezea. Lakini maji hayo pia yalipatikana kwa gharama ya kupiga hodi, kusalimia na kuomba maji ya kunywa tosha! Vivyo hivyo mijini nako mambo yalikuwa si haba, hakika iliwezekana pia kupiga hodi nyumba yoyote ukasalimia vizuri na kuomba maji ya kunywa na wakakuletea galoni la maji lenye umande toka katika friji pamoja na glasi
ujisevie...
Lakini mambo leo hii yamebadilika. Ndiyo, maji yanauzwa! Si kiyama hiki jamani? Kiyama kwa maana maji ndio uhai wa binadamu sasa uhai unauzwa shilingi ngapi? Yanauzwa! kwenye chupa haya, kwenye mifuko ya plastiki ambayo bila adabu yamepewa jina "maji ya viroba" haya, ya kupimiana kwenye glasi tuambukizane maradhi haya. Yanauzwa...

Maji ya chupa:
Lakini, hebu tuyaangalie kwanza maji haya yanayoitwa ya chupa jinsi yanavyopewa urasmi katika matumizi kwa mipango ya "lifestyle..." Hapana, japo ninaweza nikagusa maslahi ya watengenezaji wa maji ya chupa nchini kwa hili nitawaomba waniwie radhi maana wanywaji ni sisi raia tusiojua kitu na kuwapa wao maisha yetu kirehani-rehani tu. Tabia imejengeka tena ya kukereketa kabisa rohoni kuona watu eti wananunua lundo la maji ya chupa na kuyaweka majumbani familia ipate maji ya kisasa zaidi. Wengine ndio imekuwa kawaida kuzunguka na maji hayo kutishia wenzao kuwa wao hunywa kilicho bora, mambo yao safi.
Maji yaliyofungiwa kitaalamu ni maji maiti. Maji maiti kwa maana maji ni kitiririka na hupoteza maana halisi au hufa mara tu yanapokatazwa kutiririka. Hii inajulikana dunia nzima. Kwa kutambua hilo ndio maana maji yaliyofungiwa huwa yanaharibika yakikaa muda fulani (Expire date) hii inahitaji macho tu kuisoma katika chupa ya maji yoyote. Hivyo kwa kuwa maji yakifungiwa hufa, ndio maana unashauriwa kuyarudishia uhai kiujanja kwa kuyaweka katika ubaridi kabla ya kuyanywa. Na kwa kuhakikisha hilo hebu kunywa maji ya chupa ya moto uisikie ladha yake ilivyokufa. Hapa sisemi kuwa maji ya chupa hayafai, ila najaribu kukufahamisha msomaji wangu kuwa maji ya chupa si rasmi kwa matumizi bali ni msaada tu pale maji rasmi yanapokosekana. Wewe unatakiwa unywe maji hai tena ikibidi ukinge mdomo katika chemchem....

Maji ya Madimbwi:
Binadamu akishikwa na pilika za kiu huwezi kumzuia. Akina mama watakuwa mashahidi wangu wazuri maana kesi za watoto kunywa mafuta ya taa wakidhani ni maji wameshazizoea. Eneo fulani wanaweza wakawa na shida ya maji salama. Hawa wanaweza kuwa wana madimbwi na mifereji ya maji lakini wanayaogopa kuyanywa kwa kuwa yameshawapeleka ahera wengi na wengi wao pale wameshalazwa kwa kuambukizwa maradhi na vimelea vya maradhi vilivyomo mle.
Niliposhiriki "Route Match" na jeshi fulani hapa duniani nakumbuka nilifundishwa kuweka "Iodine pellets" ndani ya mkoba wangu kama kinga ya kunywa maji yoyote mbele yangu kwa kuwa tulitembea siku nane usiku na mchana ndio kikaeleweka. Iodine pellets kwa kiswahili ni "shabu" tena zipo tele masokoni na pengine madukani. hutataabika kuzipata na kama itakusumbua nitafute nikusaidie. Chukua punje moja tu yenye ukubwa wa kunde, tia katika glasi yako yenye maji, acha ikae kwa dakika tano hadi kumi kisha kunywa maji hayo. Utakuwa salama salimini.
Lakini angalia kuwa kunywa maji ya aina hii kunataka upelelezi mdogo kwa kutumia akili ya kawaida kabisa. Inakubidi kwanza kabisa kabla hujafanya chochote chunguza vyanzo vya dimbwi ua mfereji huo kama unatoka kwenye viwanda au makazi ya binadamu? Siri yako msomaji wangu, viwanda na binadamu ni wazalishaji wakubwa wa sumu zisizojulikana hivyo ukigundua vyanzo ni hivyo USINYWE maji hayo.

Maji yenye chumvi:
Kwa wakazi wa Jiji la Dar Es Salaam hasa maeneo ya Mbagala wanayajua sana maji haya. Wao wanayapata toka katika visima vilivyozagaa maeneo hayo maana ndivyo vyanzo vyao vikubwa vya maji wanayotumia. Maji chumvi kitaalamu si maji salama japo unaweza ukayapata yakiwa safi. Usalama wake si wa kuaminika kwa kuwa ardhi ina utajiri wa madini ya aina nyingi zenye tija kwa binadamu lakini ardhi inabeba pia madini yenye sumu baridi (slow killer agents) ambayo unaweza kuyaonja katika maji na kusema ni "chumvi" bila kujua ni chumvi gani, na kama ni sumu au la.
Kisima kinachotoa maji yenye sumu baridi za aina hii hudhoofisha afya za wakazi wanaolizunguka eneo hilo kila wanapoyatumia maji hayo na siku moja sumu ikiwakolea ndipo mnakutana hospitali wakazi wa mtaa mzima bila kumjua mchawi wenu na huku dakitari akijikuta haujui ugonjwa wenu pia... Mtajikuta mmefanana na wakazi wa mji fulani waliokula nyama toka bucha moja ambalo bila kujua muuza bucha alikuwa anakatia nyama katika gogo la mti wenye asili ya sumu baridi. Ugonjwa wa ajabu mtaa mzima! Walijikuta mtaa mzima wamejaa hospitali, hawajulikani wanaumwa nini..... Tutaizungumza mungu akipenda.
Lakini msomaji wangu siwezi kukuacha yakukute. Unajua kuitenganisha chumvi na maji ya kunywa ni shughuli kubwa, yenye mipango mingi pengine kufungua kiwanda. Hapa ninayo mbinu ya kijeshi na ya kisayansi zaidi unayoweza kujichujia chumvi hiyo na ukapata maji japo kidogo ya kunywa. Fanya hivi: Chukua beseni tia maji hayo haramu yenye chumvi nenda kaweke juani.
Chukua jagi au kikombe kizito kisichoelea weka katikati ya beseni lako lakini angalia maji yasizidi yakaingia kwenye chombo chako na uhakikis ` he chombo hicho hakielei kimetuama kabisa. Chukua karatasi la nailoni ziba juu ya beseni lako kisha funga na kamba ikaze beseni lizibe kabisa. Chukua jiwe dogo saizi ya ndimu weka katikati ya karatasi pale juu ili lilete kauzito fulani.Pamoja na kauzito hako angalia karatasi lisikiguse chombo ulichoweka ndani.
Subiri maji yajichuje, baada ya masaa matatu nenda kafunue karatasi. Utakuta maji yenye chumvi ndani ya beseni yamekuwa ya moto yanatoa mvuke ambao unatengeneza umande kwenye karatasi la nailoni kwa ndani. Sasa, kwa kuwa nje umeweka jiwe katikati, basi umande ule pale ndani utatiririka kuja kati kwenye uzito na kisha ni kuangukia kwenye chombo kitupu ulichokitega kwa ndani. Utakapofungua lile karatasi utakuta chombo chako kina maji na ukiyanywa ni bariiidi kabisa hayana chumvi. Unaweza ukatengeneza chombo kikubwa zaidi kama matumizi yako ni makubwa ila utatakiwa kujua namna ya kupiga hesabu za kifundi. Ukishindwa niite nikusaidie.

Maji ni nini?
Maji ni neema ya kiuumbaji tuliyopewa na mola wetu bure! Shika hilo maana ukituuliza wanasayansi tutakuambia maji ni molekule yenye atomi mbili za haidrojeni na atomi moja ya oxygen. Molekule hizo ndizo zinazounda kitu kiitwacho maji. Hakuna kitu muhimu duniani kama kunywa maji. Lakini kunywa maji safi na salama ndio busara ya kawaida kwa kila mtu. Maji hupatikana toka katika chemchem, mvua na vyanzo vingine vingi tu kama vile maji madini ya visima virefu nk. Umuhimu wa maji kwa binadamu ni mkubwa kupita maelezo kiasi kwamba wataalamu wa afya wa aina zote duniani wamekiri kuwa maji ndio uhai. Unaweza ukanywa, ukaoga, ukapikia, ukaoshea, ukanyweshea n.k. lakini usisahau shughuli za kiroho kama kubatiza, kusilimisha, kutibu, kuapisha na hata ukija kwangu nitakutibu kwa maji tu! ndiyo, nina ibada ya kuomba chochote kiwe mwilini mwako kwa maji na ukapona.

Kwanini unywe maji?
Kuna tafiti mbalimbali zimeonyesha kuwa mtu aliyekunywa lita mbili za maji au glasi nane tu kwa siku alitupa dawa za maumivu ya viungo baada ya wiki mbili tu. Mwingine alitupa dawa za kizunguzungu na kuumwa kichwa. Wapo pia walioi
pona bila kujijua maradhi ya aina nyingi sana. Hebu tujiulize maji huwa yanaenda wapi mwilini?
Kwa ujumla binadamu yeyote ni maji kwa 55% hadi 78% kulingana na ukubwa wa umbo lako. Labda nikuambie kuwa maji ni theluthi mbili ya mwili wa binadamu yeyote yule aliye hai hivyo ndio maana watu wakiamua kukuua hukuchinja. wanakata mshipa mkubwa ubebao maji yote ya mwili pale shingoni na ukikauka maji umetuaga!
75% ya misuli ya binadamu ni maji
. Mtu asiyekunywa maji hana nguvu, amini kabisa. kama vipi jiulize mbona mtu akiwa mgonjwa taabani huomba maji na si kinginecho. Umewaona wauguzi wajanja? Kabla ya yote mgonjwa anapewa dripu za maji kwanza. Shangaa...
90% ya ubongo wa binadamu ni maji.
Maji katika ubongo humfanya mtu awe na uwanja mpana mno kifikra katika kufikiri, kutoa maamuzi, kukiri, kusamehe, kushauri na kila kitu kiitwacho fikra sahihi. Alama ya kwanza kwa mtu asiyekunywa maji ni ubishi. Ukiona mtu anakuwa mbishi bila msingi basi mthibitishe kwa kumwangalia sura yake utagundua ni mzee kuliko umri wake... Maji. Ukimsogelea usoni mdomo wake unanuka vyakula vimevunda tumboni, huyo hanywi maji. Jichunguze msomaji wangu. Wewe si kikwazo kwa ubishi kwa wenzio? Kama vipi, kunywa maji.
22% ya mifupa ya binadamu ni maji.
Wazee mliofikia umri wa miaka 50 na kuendelea hebu nawaomba msogee mbele huku. Hapa nawaomba mnisikilize maana nyinyi ndio walalamishi mno wa maradhi ya mifupa lakini kunywa maji hamjui kuwa ni dawa. Ukinywa glasi 8 za maji kila siku kwa wiki mbili tu utanipigia simu kuwa maumivu yameanza kupungua. na ukiendelea kunywa maji kwa miezi mitatu utakuwa umepona sio tu mgongo, miguu, nyayo, kiuno, kizunguzungu na mengineyo, bali hata ujana unarudi! Niamini kabisa uone maajabu.
83% ya damu ya binadamu ni maji.
Hili sina haja sana ya kulijadili tena maana nimelisema hapo mwanzo na nafikiri hata wewe msomaji wangu tutakubaliana tu katika hili hata uwe mtoto mdogo. Usipokunywa maji unauakaribia mstari wa kupungukiwa na damu. Utakaribisha pia maradhi ya moyo kwa vivunde vya unavyokula bila kuviyeyusha na maji vinakuwa sumu kali mwilini na mwisho utakufa

Kazi za maji mwilini:
Maji yana kazi nyingi mno mwilini, na hata hivyo nyingi bado hazijawekwa bayana bado mpaka leo lakini nakupa tu hizi chache ambazo zinatosha kabisa kukushawishi msomaji wangu kuwa mnywaji mzuri wa maji. Maji yanasafirisha virutubisho vyote tunavyokula pamoja na hewa ya oksijeni kwenda sehemu zote za mwili. Maji ndio yanayoirutubisha hewa ya oksijeni katika mapafu, huku yakiwa bado kama korokorokoni kulinda na kukarabati seli zote za mwili.
Ukisikia mtu anasema kichwa kinauma mara kwa mara basi huyo hanywi maji! sio kichwa tu kinachouma pale, hata ngozi ya midomo inabanduka kwa ukavu, ni mwoga, hajiamini n.k. Maji pia hurekebisha joto la mwili, na ndio maana wakati wa jua wauza maji baridi ni neema kwao na wakati wa baridi wauza kahawa nao si haba... Lakini ukinywa maji basi ujue hayataishia mwilini bali yataenda kuchukua nafasi ya yale yaliyotumika na ndio maana ukiuonja mkojo una ladha kali lakini maji ulikunywa yakiwa matamu.
Shangaa. Kabla ya maabara duniani kisukari kilipimwa kwa dokta kuuonja mkojo wa mgonjwa ili aubaini ugonjwa! Upo ushahidi wa kumtibu mgonjwa wa maleria kwa kumpa maji kwa masaa kadhaa tu na akapona. Wazee narudia tena, mgongo, kiuno, miguu, usingizi, na shida zote za uzee kunywa maji glasi nane kila siku kwa wiki mbili uone maajabu! Elewa kuwa, hakika hakuna kisichotegemea maji toka unywele hata kufika miguuni kwenye ukucha wako.

Faida za maji mwilini:
Ukinywa maji utajisikia mwepesi maana yanavunja lehemu na sumu na kuzitolea kwenye mkojo. Ukinywa maji vile vile utapunguza njaa. Wataalamu wa lishe wanasema maji ni kirekebisho cha hamu ya kula ambacho unatakiwa unywe kabla ya kula ili usije vimbiwa kwa kula zaidi. Hivyo utajikuta njaa imepungua. Maji hayo pia ni dawa kwa waliozidiwa na uzito mwili (overweight) maana yanayeyusha mafuta yaliyozidi na kuyatoa kwa mkojo na jasho na kukupunguzia uzito kila siku.
Maji ni tiba binafsi (pocket doctor) pale unapo banwa na mawazo labda umechacha, bosi mkali, biashara imedoda, mwandani anasumbua kichwa chako n.k. kunywa maji mengi kukupunguzia mzigo huo wa mawazo na hakika utaukubali mpango huu. Maji humfanya binadamu aonekane kama mmea ulioota kando ya mto na asiyekunywa huonekana kama mmea uliooteshwa juu ya kichuguu! Wazee, Hakika ujana unarudi. Akina mama, mtaungua sana na hayo madawa ya kemikali kwa kutojua tu. Maji yanafanya kazi kushinda krimu au losheni yoyote ile duniani! Hata mimi natafuta mchumba anayekunywa maji walau glasi sita kwa siku, na nikimtazama kwa macho ajae katika mizani. Anayetaka kuamini aanze kunywa glasi nane tu kwa siku halafu baada ya wiki mbili aone maajabu.
Maji kwa wafanyakazi. Wewe kama ni mfanyakazi bila kujali ni wa sekta gani, jenga tabia ya kunywa maji glasi moja kila baada ya saa moja halafu baada ya majuma mawili tu utanipigia ukikiri ulivyonufaika. Maji yanakufanya uwe mjanja. Kwa kuwa yanamiliki 90% ya ubongo basi mtu asiyekunywa maji ni rahisi kudanganywa, kutapeliwa, kuzubaa, kutoeleweka maamuzi yako n.k. Maji kwa kuwa yanajaa mwilini kukupa afya na nguvu, basi anayekunywa maji si mwoga! Ni mtu anayejiamini na ni mshindi kwa wasiokunywa maji popote: darasani, kazini, biashara, shambani, michezoni n.k. Lakini ukinywa maji, huumwi hovyo! Amini msomaji wangu, wakati nakupa simulizi hii tamu malaika wa heri mbinguni wanapiga vinanda kuisifia nguvu hii kuu ya uumbaji duniani ambako pia Wataalamu wa afya duniani kote wameshikana mikono wakiirusha juu na kusema "REFUSHA, FURAHIA MAISHA KWA MAJI"


John Haule ni mpelelezi binafsi (Private investigator) anayejihusisha na tafiti zenye suluhisho kwa matatizo ya kijamii. Unaweza kumpigia kwa miadi ya ushauri juu ya tatizo lolote linalokusumbua kibinadamu. Anapatikana Car Painters - Temeke Stereo, Sandawe Street, jirani na Dr. Massawe. Simu: 0768 215 956 au email rumoursafrica@gmail.com

"Swahili NA Waswahili" Pamoja Sana.

Wednesday 2 January 2013

Kitabu Kimojawapo cha Prof.Mbele-Africans and Americans: Embracing Cultural Differences








The book is available at http://www.lulu.com/shop/joseph-mbele/africans-and-americans-embracing-cultur... and other internet sites.
 

Here is a review on Amazon http://www.amazon.com/Africans-And-Americans-Embracing-Differences/dp/1411623...


"Mbele takes on the arduous task of comparing American and African cultural differences, focusing mostly on Tanzanian culture and customs - and he does this in less than 100 pages. Anyone interested in this topic will find mostly anecdotal comments and observations from someone who has spent time on both continents. In the end Mbele notes that people are different and that we should embrace and accommodate our differences as much as possible. This is a good book with good information to consider if you are traveling to Africa anytime soon or hosting an exchange student from Africa.


Kujua Mengi kuhusu Prof.Mbele ingia;Joseph Mbele na http://hapakwetu.blogspot.co.uk/


"Swahili NA Waswahili" Pamoja Sana

Poleni Sana; Familia,Wa-Tanzania na Mashabiki wa Sajuki!!!

Marehemu;Juma Kilowoko [Sajuki].

Pole sana Wastara,Familia,Ndugu,Jamaa na Marafiki, Wa-Tanzania na Mashabiki wa Sajuki.Sisi Tulikupenda lakini  Lipangwalo na MUNGU Bina Damu hawezi kulipangua.

  Ulale kwa Amani.

Mboni Yangu-Wimbo uliokuwa ukihamasisha Uchangiaji wa Matibabu ya Sajuki.
Yote hayo yalifanywa kwa Mapenzi mema ili kuokoa Maisha ya Mwenzetu.


Wimbo umeshirikisha mastaa wa kibongo kama Ali Kiba, Wema Sepetu, Mwana FA, Professor Jay, Mzee Yusuph, Chidi Beenz, Fid Q, Afande Sele, Amini, Ditto, Madee, Peter Msechu, Dina Marios na wengine wengi.


"Swahili NA Waswahili" MUNGU awatie Nguvu katika wakati huu Mgumu.
Pamoja Daima.

Jukwaa Jipya la Malumbano ya Hoja;Filosofa Forum!!!!!


Filosofa Forum Imevutia Wengi

Discussion forum mpya – Filosofa Forum ni jukwaa jipya la malumbano ya hoja. Tangu kuanzishwa rasmi siku chache zilizopita kumekuwa na mlolongo wa wapenda hoja kujiunga na kuchangia hoja mbalimbali.

Malengo ya timu inayoendesha jukwaa hili ni kuhakikisha inampa kila mtu nafasi ya kutoa mawazo, kuuliza maswali, kuchangia hoja, n.k, bila kujali jinsia, maumbile, uwezo, cheo, kabila, itikadi au dini. Jukwaa hili limeundwa kwa kuzingatia maadili ya mtanzania. Maneno ya matusi yananaswa (detected automatically). Ni rahisi kujiunga au kuchangia hoja. Huhitaji ujuzi wa kompyuta wa hali ya juu sana kutumia. Karibu ujiunge uelimike na kuelimisha wengine.

Tuesday 1 January 2013

Afya na Jamii; na MSwahili John Haule-Panda maua yafukuzayo Mbu!


Panda maua yafukuzayo Mbu!

Msimu wa mvua unakuja. Hauji kimya kimya. Ni lazima unakuja na maambukizi makubwa ya malaria yatokanayo na madimbwi yanayozalisha mbu kwa wingi zaidi na mbaya sana mbu jike wa anofelesi huzaliwa wengi pia. Mbu hawa ndio vinara wa kuwaambukiza watu malaria na habari mbaya zaidi nilizonazo mkononi nikuwa wanawake hasa wajawazito ndio waathirika wakuu wa maambukizi ya ugonjwa huu kwa vile huzalisha hewa ya karboni nyingi kuliko wanaume na hivyo kuwavutia mbu hawa ambao wanaambukiza malaria kuwafuata na kuwadunga. Hii ndio siri ya foleni ndefu za akina mama na watoto mahospitalini.
Mbu hawa wapoje?
·        Wana rangi ya kahawia. Akitua katika mwili wako hutega tumbo lake kubwa juu kwa nyuzi 45 na kuleta miguu yake ya nyuma kuwa stendi za kubeba uzito wa damu atakayo kudunga!
·        Huweza kunusa binadamu alipo toka umbali wa mita 50!

Ni kawaida ya msimu wa mvua kuja na hali ya joto inayowavutia watu wengi kutoka nje na kupunga upepo usiku ambao ndio muda muafaka mbu hao kundunga na kuambukiza watu malaria kwa mujibu wa wataalamu. Rumours Africa tumetafiti namna bora ya kuwafukuza mbu toka katika maeneo yote ya nyumba yako, ofisi, hoteli, shule, hospitali, kiwanda na sehemu zingine za kazi ambazo watu hukaa usiku hasa mabaa yanayokesha ambayo pia ni wazalishaji wakubwa wa wagonjwa wa malaria.

Maua yafukuzayo Mbu?
Njia hiyo kwa mujibu wa tafiti mbalimbali zilizotugharimu mno kuokoa maisha ya watanzania ni kupanda maua yenye harufu na rangi zinazofukuza mbu kama vile rosemary, cintronella, mchaichai n.k.
Tulitafiti pia ni jinsi gani watanzania watazipata mbegu hizi za maua kwa urahisi lakini tukagundua kuwa ni sehemu chache sana wanazoishi watu wenye uelewa hasa wazungu ndio hupanda maua haya bila kuwaambia wengine  na kuwaacha watanzania wengine wapande maua kama urembo tu badala ya dawa na vyakula, na hivyo kujikuta wakipata wakati mgumu kupambana na malaria.

Kwa sasa bado tunafanya mpango wa kutafuta wadau wa kuwekeza kuanzisha bustani ya maua hayo ili tupate mbegu kusaidia watu lakini kwa mwenye haraka zake kujikinga na malaria ni gharama kidogo maana itabidi kusafiri mpaka Peramiho Mission au Uwemba Mission ambako nimeyaona kwa macho mashamba yanayozalisha maua yakiwemo hayo na kusafirishwa ulaya. Pengine labda niliwahi sikia tu kuwa hata Arusha pia kuna mashamba ya maua pia lakini upatikanaji wake kwa kweli siujui.

Maua haya hatimaye yatasambaa. Kila mtu nahisi angependa kupanda maua yenye maana halisi katika maisha na hasa kumlinda yeye, familia, wafanyakazi na wateja pia. Hivyo yeyote ambaye amevutiwa na habari hii na angependa kushiriki kwa namna yoyote kuwekeza katika fursa hii muhimu na adimu kwa taifa letu basi angewasiliana na rumoursafrica kupitia simu namba 0768215956 au email rumoursafrica@gmail.com.

Ujumbe huu unaweza kuwa muhimu kwako, lakini unaweza kuwa muhimu kwa wengine pia hivyo ningekuomba msomaji wangu uufikishe ujumbe huu kwa wapendwa wako ukisisitiza umuhimu wa kujikinga na malaria.

Asanteni kwa kunisoma.

John Haule ni mpelelezi binafsi (Private investigator) anayejihusisha na tafiti zenye suluhisho kwa matatizo ya kijamii. Unaweza kumpigia kwa miadi ya ushauri juu ya tatizo lolote linalokusumbua kibinadamu. Anapatikana Car Painters - Temeke Stereo, Sandawe Street, jirani na Dr. Massawe. Simu: 0768 215 956 au email rumoursafrica@gmail.com


         "Swahili NA Waswahili" Pamoja Daima.

Karate: J.Kassam Ft Juma Jazz!!!!!



mwanamuziki chipukizi lakini mkongwe kwa umri Juma Kassam ,ambaye pamoja na Muziki pia ni muigizaji 
na mwanamichezo hususani mchezo wakujihami KARATE.
Usikilizewimbo wake unaojulikana kwa jina la "KARATE" future-ring Juma Jazz na uone jinsi alivyokuja na muelekeo mpya 
zaidi ya vile tulivyozoea ya nyimbo zenye ujumbe wa mapenzi.





"Swahili NA Waswahili" Pamoja Sana

Mtazamo wa John Kitime katika muziki 2012!!!!!!!


Mwaka 2012 ndio huoo umetokomea, ni vizuri kuangalia yaliyopita ili kujitayarisha na yajayo. Muziki wa nchi yetu ulitawaliwa na muziki wa Bongoflava, Taarab, muziki wa bendi, matarumbeta, muziki wa Enjili, na muziki wa kiasili. Si siri kuwa muziki wa Bongoflava ndio uliokuwa ukitawala katika vyombo vya habari na sehemu nyingi za maonyesho ukifuatiliwa na muziki wa Taarab na muziki wa enjili.  Katika muziki wote huu jambo lililokuwa wazi ni kuwa waimbaji ndio waliokuwa wakipewa kipaumbele katika tasnia hii.  Waimbaji katika aina zote za muziki uliotajwa hapo juu ndio waliotajwa na kupewa sifa kwa ubora wa muziki. Kumekuweko na mashindano kadhaa ambayo yote yamejikita katika kutafuta vipawa vya waimbaji japo mara nyingi yamejitambulisha kama mashindano ya kusaka vipaji mbalimbali. Hakuna ubishi muziki wa dansi na muziki wa asili ndio muziki uliopewa muda mchache sana katika vyombo vya habari. Na hata katika muziki huo, bendi ambazo zimejikita kufuata mipigo ya Kikongo vilipewa nafasi zaidi ya bendi ambazo zimejichagulia njia nyingine za muziki wao.
Kuna sababu kadhaa ambazo zimefanya muziki wa bongoflava kuchukua nafasi zaidi katika vyombo vya habari, la kwanza ni uwingi wa kazi za bongoflava zinazorekodiwa. Karibu kila mji una studio ya aina moja au nyingine, na katika studio hizo kazi nyingi zaidi zinazorekodiwa ni aina hiyo ya muziki, hivyo kutokana na uwingi wa kazi hizo ni wazi kabisa ndizo ambazo zitaendelea kutawala anga la vyombo vya habari, na pia ni kutokana na mfumo wa vyombo vyetu vyote kujikita katika mfumo wa aina fulani tu za muziki.
Kwa mtizamo wangu heka heka za muziki wa Enjili zilipungua 2012. Yale matamasha makubwa ya muziki huo yalipungua sana, na hata nyimbo za kushtua jamii hazikuwa nyingi  kama ilivyokuwa miaka ya nyuma.
Muziki wa Taarab haujaleta mabadiliko kimuziki, mengi yaliyofanywa katika 2012 ni marudio tu ya ubunifu uliofanyika nyuma. Kama vile uanzishwaji wa kucheza show katika taarab, upigaji wa gitaa na kuliachia pekee yake kama ilivyokuwa kwa bendi kuachia gitaa la rhythm miaka kabla ya tisini na zile video za kucheza mbele za viwanja vya hoteli. Kumekuweko tu ubunifu wa misemo na mipasho, jambo tena ambalo limesababisha kuenziwa zaidi kwa waimbaji tu katika fani hiyo pia.
Bendi ziko katika wakati mgumu, wakati wanamuziki wengi wa bendi wakilalamika kuwa muziki wa bendi haupigwi, kumekuweko na jitihada ndogo za bendi kurekodi nyimbo mpya, maelezo mengi yamekuwa ni kuhadithia enzi ambapo muziki wa bendi ulitawala na kuona kama hiyo ni sababu tosha ya muziki huo kurushwa hewani. Bendi chache zilizorekodi hazijaja na  nyimbo zilizoweza kuteka umma wa wa Tanzania na hivyo kusababisha muziki huu kukosekana katika anga za muziki. Matangazo mengi ya muziki wa dansi yamekuwa ni kutangaza rap mpya au kupatikana kwa msanii mpya, lakini kiujumla hakujakuwa na kitu kipya katika muziki wa bendi.
Muziki asili pia umekosekana kwenye vyombo vya habari kwa kuwa si vikundi vingi vya muziki huu vyenye uwezo wa kulipia gharama za studio ambao muziki huu unastahili kurekodiwa. Studio nyingi zimejengwa kwa ajili ya muziki wa aina ya Bongoflava tu, zile studio za kuweza kuruhusu kundi la muziki wa asili kurekodi gharama yake huwa ni kubwa sana. 
Kundi la Makirikiri lilitakiwa kuwa elimu tosha kwa wasanii wa muziki wa Kiasili, kuwa na muziki huo ukifuata taratibu nzuri ya kurekodiwa unauza vizuri sana, bahati mbaya kuna vikundi sasa vimeacha muziki na ngoma zao, vinaiga uchezaji wa  Makirikiri.
Pengine watu watasema nimesahau muziki wa kwaya, sijausahau, kwa kweli muziki huu umebaki  hasa kwenye muziki wa Enjili. Hapo zamani ulikuwa ukitumika sana kwenye siasa na kampeni , lakini kwa mwaka 2012 hali imekuwa mbaya kwa muziki huu.
Pamoja na kuwa wengine wangeweza kusema tunasonga mbele katika muziki, kwangu mimi naona tunarudi nyuma kitaaluma. Tasnia inaingiza pesa nyingi zaidi, na hata kuna wasanii walioingiza pesa nyingi sana, lakini  kwangu hilo si kipimo cha maendeleo katika tasnia hii.
Kama nilivyoanza kusema washika maikrofon wamekuwa ndio alama ya muziki wa Tanzania. Muziki ni zaidi ya kuimba. Katika kuimba sauti nzuri ya muimbaji ni muhimu, na ninashukuru kwa hilo tunao waimbaji wazuri wengi sana, lakini  ule muziki unaomsindikiza muimbaji ni muhimu sana kwani ule hauna mipaka wala lugha, na ndio unaoweza kutufungulia mlango wa soko la kimataifa. Wengi tunapenda sana muziki wa kutoka Kongo, Nigeria, South Africa, pamoja na kuwa hatujui hata moja wanaloliongelea tunaupenda muziki huo kutokana na mpangilio wa vyombo vyao. Kutokujali wapigaji katika mfumo wa nchi yetu ndio unatupelekea kuwa watu wa ‘copy and paste’ wa upigaji wa muziki wa nchi nyingine. Ukiorodhesha nyimbo zote zilizotikisa nchi hii kwa mwaka 2012 utagundua asilimia kubwa ya muziki uliotumika ulikuwa ni wa kunakili kutoka muziki wa nchi nyingine, Nigeria, Congo na Afrika Kusini ndio wamekuwa waalimu wetu wakuu. Ushauri kwa maproducer wa Bongoflava, kuangalia pia muziki wetu wa asili humu ndani ya nchi ili tuje tumalize 2013 na kitu chetu ambacho Wanaigeria, Wakongo nao pia waige toka kwetu. Inawezekana sana maana wimbo wa Weekend wa Afro70 uliwahi kuweko katika  kumi bora 1972, Nigeria.
Muziki wa Enjili pamoja na kuwa ndio unaotegemewa kutufundisha maadili, ulikuwa na kasoro moja kubwa nayo ni kukosa maadili kwa kucopy na kupaste. Nyimbo nyingi zilizokuwa maarufu na kuteka hisia za maelfu ya watu zilikuwa ni kuiga moja kwamoja kutoka Afrika ya kusini. Najiuliza je ndio kilichopunguza moto wa muziki huu 2012? Kulikuwa hakuna za kukopi? Wanamuziki wa Enjili kama ilivyo kwa ushauri kuhusu Bongoflava, ni muda wa kurudi nyuma na kutumia raslimali ya utamaduni iliyoko kuleta mabadiliko na kukuza soko la muziki huo.
Tasnia ya muuziki wa Tanzania katika tafiti moja wapo umeitwa ‘the radio-driven contemporary music industry’. Kwa maneno rahisi, tasnia ambayo imekuwa inaendeshwa na radio. Radio zimekuwa na uwezo wa kumpandisha na kumshusha mwanamuziki, kumtafutia soko, kumzibia soko na kadhalika. Hali hii ikisindikizwa na rushwa ambayo imetapakaa katika jamii yetu, unapata picha kuwa kungeweza kukawa na sura bora au tofauti ya muziki hali isingekuwa ilivyo. Kuna ripoti za watu kutoa hongo nyimbo za wenzao zisipigwe, hongo ili nyimbo zipigwe, visasi vya kuzuia nyimbo zisipigwe na kadhalika. Na katika jamii ambayo imekuwa na kawaida ya kutegemea vyombo vya habari kujua muziki gani mpya na mzuri, uwanja huu si uwanja ulio tambarare hata kidogo. Bahati mbaya inaonekana wenye vyombo hivi wako mbali na ukweli unaoendelea katika vyombo vyao au kwa kutokujua au kupuuza. Janga hili limevikumba hata vyombo ambavyo vinaendeshwa na taasisi za dini. Wanamuziki wa muziki wa Enjili nao pia wanalia kudaiwa rushwa na watangazaji wa radio za Enjili!.  Nakumbuka siku niliyopata nafasi kuongea na kiongozi mmoja wa dini ambaye Kanisa lake linaendesha kituo cha radio, nilipata mshangao baada mkuu huyo, kuanza kutetea watangazaji wake badala ya kuamua kufanya uchunguzi wa tuhuma.
Umefika muda wa radio kuanza kujigawa kimuziki. Ni kichekesho mji kuwa na vituo vya radio 30 halafu vyote vinapiga aina hiyohiyo ya muziki, wakati kuna aina mbalimbali za watu. Ajabu ni kuwa wenye radio wanajua kuwa katika nchi nyingine unaweza kukuta radio iliyoamua kupiga aina fulani tu ya muziki, Jazz Radio, Country music Radio, Classic Music Radio, lakini hilo limekuwa gumu kwao kutekeleza hapa. Kuwe na utofauti, Wasikilizaji tuko wa aina tofauti.
Vyombo vya habari viijitahidi kupata wataalamu husika wa aina tofauti za muziki, muziki unaviingizia vyombo hivyo mabilioni ya fedha, vyombo vya habari  viupe heshima yake. Bila muziki hakuna radio.
Magazeti yamekuwa mstari wa mbele katika kutangaza aina mbalimbali za wasanii na sanaa. Pamoja na hongera kwa kazi nzuri lakini bado kuna nafasi kubwa ipo tupu, hakuna wataalamu wa uandishi wa habari za muziki. Hivyo habari nyingi za muziki zinaandikwa na waandishi kama wapenzi wa muziki na si wataalam wa uandishi wa muziki, jambo ambalo liko tofauti na uandishi wa michezo kwa mfano soka. Unaweza ukasoma habari ya soka ambapo mwandish atakueleza nafasi za wachezaji, kama ni faulo, ni nini kilisababisha, na kama ni goli lilikuwa ni la kichwa au kona au penalty, hili haliko katika muziki. Utaambiwa tu  bendi ilipagawisha, au msanii fulani ateka nyoyo za wapenzi, na maelezo ya juu juu kama yale, kunahitajika kuanzishwa mafunzo ya elimu ya uandishi wa kazi za sanaa. Hili litapunguza hata vurugu kama zilizotawala  mwaka huu ya wapiga picha kufikia hata kulala chini ili tu wapate picha ya nguo za ndani za msanii na hayo ndio kuwa maelezo makuu ya onyesho zima la  muziki.
Ikiwa kulikuwa na mchango wa serikali katika muziki, basi ulikuwa mdogo au ulikuwa ni kwa shughuli maalumu lakini si kwa kutengeneza mazingira ya kuwezesha unafuu kwa wanamuziki kwa ujumla. Idara ya Utamaduni imeendelea kupata bajeti ndogo ambayo imefanya Baraza La Sanaa La Taifa kuendelea kubaki Dar es Salaam tu, likibangaiza kuweko kwa kutegemea kutoa vibali mbalimbali kwa wasanii, na nguvu zake kuonekana Dar es Salaam tu. Na kwa kuwa hakuna Maafisa Utamaduni Mkoa, na Maafisa Utamaduni Wilaya na Manispaa wako chini ya serikali za mitaa hivyo kuwa wizara tofauti na Waziri wa Utamaduni, nguvu za serikali katika utamaduni ni 0. COSOTA chombo ambacho shughuli yake ilikuwa ni kulinda hakimiliki za wasanii na ambacho kilikuwa chini ya wasanii, kwa kinyemela kabisa kimerudishwa katika mikono ya serikali, lakini bado kinakusanya mirabaha 'kwa niaba ya wasanii' huku kukiwa na bodi isiyo na uwakilishi wa wasanii kuanzia 2007. Swali utakusanyaje pesa kwa iaba yangu lakini huniruhusu kujua ni kiasi gani umekusanya, unazitumiaje na ukiulizwa unakuwa mkali!!!!!!? Kuna wasanii wamekuwa wakidai kurudishiwa COSOTA, ushauri wangu wasanii wakae wajipange  na kuelewa vizuri sheria ya Hakimiliki kabla ya kujitwishwa zigo hilo la miba.
Katika miezi 6 ya mwisho ya 2012 kumejitokeza spidi kali ya Mamlaka ya Ukusanyaji wa Mapato kutengeneza mazingira ya kukusanya mapato kutokana na mauzo ya kazi za muziki na filamu. Kimsingi kulipa kodi ni wajibu wa kila mwananchi na wasanii ni wananchi pia, lakini taratibu zake ndio zinanipa utata, hasa pale ambapo kwa muda mrefu imekuwa ikitangazwa kuwa njia hii itasaidia wasanii kwa kupunguza kuibiwa.  Sentensi hii inaonyesha wazi anaeiongelea aidha hajui mfumo wa biashara ya kazi muziki, au kwa makusudi anapotosha ili kuficha kitu. Wasanii wengi huwa wamekwishalipwa kwa kazi ambazo zimesambaa na ziko barabarani zinaibiwa, wanaoibiwa ni wasambazaji. Hivyo kulinda kazi hizo unamlinda msambazaji si msanii. Pia kuanza kukusanya kodi kwa kazi hizi kumepewa jina ‘kurasmishwa  kwa kazi ya usanii’, kuna mabilioni wasanii wanatakiwa walipwe na watumiaji wa kazi za sanaa, kama radio na TV, mapromota, waajiri na kadhalika  hakuna anaeliongelea hilo wala hakuna anaetamka takwimu hizo. Kuna kazi ya kurudisha mitaala ya masomo ya sanaa mashuleni, kurudisha vyuo vya walimu wa sanaa, kurudisha maafisa utamaduni kuwa chini ya Wizara ya Utamaduni kuwawezesha kufanya kazi zao kadri ya sera ya Utamaduni, na mengine mengi ya aina hiyo ndio ningeona kurasimisha kazi za sanaa, lakini kukusanya kodi tu kwa kazi ambazo hata hivyo mikataba yake mingi inautata na kuita urasimishaji si sahihi. 
Katika nchi nyingi critics au watu ninaoweza kuwaita kiswahili wakosoaji, huwa ni muhimu katika maendeleo ya sanaa, watu hawa hupata heshima kutokana na kuweza kuangalia mapungufu katika kazi za sanaa na kuyasema, jambo ambalo hupelekea wasanii kujirekibisha na kutengeneza kazi bora zaidi. Hapa kwetu kutoa ushauri ni kutafuta matusi, toka kwa wasanii wenye kazi husika, vyombo vya habari na hata sehemu ya jamii, umefika muda wahusika kuchukua uchambuzi kama changa moto za kuboresha kazi.
Niliyoyataja hapa yote yako wazi ninachotegemea ni kuona 2013, hatua zinaanza kupigwa kurekibisha, ili wanamuziki wa nchi hii nao wapate nafasi sawa na wengine wa nchi nyingine.

John Kitime
31.12.2012
Sinza, Dar es Salaam 


      "Swahili Na Waswahili" Pamoja Sana.