Swahili na Waswahili

Swahili na Waswahili
Waswahili na Mswahili Rachel Siwa...Pamoja Daima!!

Thursday 28 December 2017

Kikombe Cha Asubuhi ;1Samueli9...



Shalom,Habari za Asubuhi,Hamjambo,Mmeamkaje?
Tumshukuru Mungu wetu katika yote..
Mungu wetu Baba yetu,Mungu wa Abrahamu,Isaka na yakobo
Muumba wetu,Muumba wa Mbingu,nchi na vyote vilivyomo
Vinavyoonekana na visivyoonekana..
Mungu mwenye nguvu,Mungu wa walio hai,Mungu wa Yatima,
Mungu wa Wajane,Mungu mwenye huruma,Mungu wa haki,Mungu wa
Amani si Mungu wa fujo..


Yesu alipoyaona makundi ya watu, alipanda mlimani, akaketi. Wanafunzi wake wakamwendea, naye akaanza kuwafundisha: “Heri walio maskini rohoni, maana ufalme wa mbinguni ni wao. Heri walio na huzuni, maana watafarijiwa. Heri walio wapole, maana watairithi nchi. Heri wenye njaa na kiu ya kufanya atakavyo Mungu, maana watashibishwa. Heri walio na huruma, maana watahurumiwa. Heri wenye moyo safi, maana watamwona Mungu. Heri wenye kuleta amani, maana wataitwa watoto wa Mungu. Heri wanaoteswa kwa sababu ya kufanya atakavyo Mungu, maana ufalme wa mbinguni ni wao. “Heri yenu nyinyi watu wakiwatukana, wakiwadhulumu na kuwasingizia kila aina ya uovu kwa ajili yangu. Furahini na kushangilia maana tuzo lenu ni kubwa mbinguni. Hivyo ndivyo walivyowadhulumu manabii waliokuwako kabla yenu.


Asante Baba wa Mbinguni kwa wema na fadhili zako kwetu
Asante kwa ulinzi wako wakati wote..
Asante kwa pumzi/uzima,afya na kuwa tayari kwa majukumu yetu..
Asante kwa kutuchagua tena na kutupa kibali cha kuendelea kuiona leo hii..
Si kwamba sisi tumetenda mema sana,wala si nguvu zetu,si kwa utashi wetu,si kwa akili zetu sisi kuwa hivi tulivyo leo hii..
Mungu wetu ni kwa neema na rehema zako..
Yahweh ni kwa mapenzi yako kwwetu sisi kuwa hivi tulivyo..
Sifa na utukufu tunakurudishia ee Mungu wetu..



“Nyinyi ni chumvi ya dunia. Lakini chumvi ikipoteza ladha yake itakolezwa na nini? Haifai kitu tena, ila hutupwa nje na kukanyagwa na watu. “Nyinyi ni mwanga wa ulimwengu! Mji uliojengwa juu ya mlima hauwezi kufichika. Wala watu hawawashi taa na kuifunika kwa debe, ila huiweka juu ya kinara ili iwaangazie wote waliomo nyumbani. Vivyo hivyo, ni lazima mwanga wenu uangaze mbele ya watu, ili wayaone matendo yenu mema, wamtukuze Baba yenu aliye mbinguni.
Baba wa Mbinguni tunakuja mbele zako tukijinyenyekeza,tukijishusha na 
kujiachilia mikononi mwako..
Mungu wetu tunaomba utusamehe makosa yetu yote tuliyoyafanya
kwakuwaza,kwakunena,kwakutenda,kwakujua/kutojua..
Mfalme wa Amani nasi tunaomba utupe neema  ya kuweza kuwasamehe wale wote waliyotukosea..
Yahweh tunaomba utuepushe Katika majaribu Baba wa mbinguni
tunaomba utuokoe na yule mwovu na Kazi zake zote..
Mungu wetu tunaomba ututakase miili yetu na akili zetu Jehovah
tunaomba utufunike kwa Damu ya Bwana na Mwokozi wetu Yesu Kristo
wa Nazareti,Yeye aliseka kwanza ili sisi tupate kupona..


“Msidhani kuwa nimekuja kutangua sheria na mafundisho ya manabii. Sikuja kutangua bali kukamilisha. Kweli nawaambieni, mpaka hapo mbingu na dunia zitakapopita, hakuna hata nukta moja au sehemu ndogo kabisa ya sheria itakayoondolewa, mpaka yote yametimia. Basi, yeyote atakayevunja hata amri moja ndogo kuliko zote, na kuwafundisha wengine wafanye hivyo, huyo atakuwa mdogo kabisa katika ufalme wa mbinguni. Lakini yule atakayezishika na kuwafundisha wengine, huyo atakuwa mkubwa katika ufalme wa mbinguni. Ndio maana nawaambieni, wema wenu usipozidi ule wa waalimu wa sheria na wa Mafarisayo, hamtaingia kamwe katika ufalme wa mbinguni.

Yahweh tunaomba ukabariki Kazi za mikono yetu..
Jehovah tunaomba utupe ubunifu na marifa Katika ufanyaji/utendaji
Mungu wetu nasi tukatende sawasawa na mapenzi yako..
Baba wa Mbinguni tunaomba ukabariki ridhiki zetu ziingiazo/zitokazo
Jehovah nasi tunaomba utupe neema ya kuweza kuwabariki wenye kuhitaji..
Mungu wetu tunaomba tusipungukiwe katika mahitaji yetu
Yahweh ukatupe sawasawa na mapenzi yako..


“Mmekwisha sikia ya kuwa watu wa kale waliambiwa: ‘Usiue! Atakayeua lazima ahukumiwe.’ Lakini mimi nawaambieni, yeyote anayemkasirikia ndugu yake, lazima ahukumiwe. Anayemdharau ndugu yake atapelekwa mahakamani. Anayemwita ndugu yake: ‘Pumbavu’ atastahili kuingia katika moto wa Jehanamu. “Basi, ukipeleka sadaka yako mbele ya madhabahu na hapo ukakumbuka kwamba ndugu yako ana ugomvi nawe, iache sadaka yako mbele ya madhabahu, nenda kwanza ukapatane na ndugu yako, ndipo urudi utoe sadaka yako. “Patana na mshtaki wako upesi mkiwa bado njiani kwenda mahakamani. La sivyo, mshtaki wako atakukabidhi kwa hakimu, naye hakimu atakukabidhi kwa askari, nawe utafungwa gerezani. Kweli nakuambia, hutatoka humo mpaka umelipa senti ya mwisho.
Mfalme wa amani tunaomba amani yako ikatawale katika nyumba/ndoa
zetu..


“Mmesikia kwamba watu waliambiwa: ‘Usizini!’ Lakini mimi nawaambieni, atakayemtazama mwanamke kwa kumtamani, amekwisha zini naye moyoni mwake. Basi, kama jicho lako la kulia linakukosesha, lingoe ukalitupe mbali. Afadhali zaidi kwako kupoteza kiungo kimoja cha mwili wako, kuliko mwili wako wote kutupwa katika moto wa Jehanamu. Na kama mkono wako wa kulia unakukosesha, ukate ukautupe mbali. Afadhali kwako kupoteza kiungo kimoja cha mwili wako, kuliko mwili wako wote uende katika moto wa Jehanamu. “Ilikwisha semwa pia: ‘Anayemwacha mke wake, yampasa ampe hati ya talaka’. Lakini mimi nawaambieni, anayempa mkewe talaka, isipokuwa kwa sababu ya uzinzi, anamfanya azini; na mwanamume akimwoa mwanamke aliyepewa talaka, anazini.
Baba tunaomba ukabariki watoto,wazazi wetu,familia/ndugu
na wote wanaotuzunguka..
Mungu wetu tunaomba ulinzi wako kwetu na kwa vyote tunavyovimiliki
Yahweh tunaomba ukatuguse kwa mkono wako wenye nguvu..
Mungu wetu ukatamalaki na kutuatamia,yahweh ukatupe neema ya kufuata njia zako,Mungu wetu ukatupe neema ya kusimamia Neno lako
Amri na Sheria zako siku zote za maisha yetu..
Mungu wetu ukaonekane popote tupitapo..
Yahweh na ijulikane kwamba upo Baba wa mbinguni..
Tukanene yaliyo yako,ukatupe macho ya rohoni,ukatupe masikio na tukasikie sauti yako na kuitii..
Yahweh tukawe salama moyoni na Amani ya Kristo Yesu ikatawale,Nuru yako ikaangaze katika maisha yetu...



“Tena mmesikia kwamba watu wa kale waliambiwa: ‘Usivunje kiapo chako, bali ni lazima utimize kiapo chako kwa Bwana.’ Lakini mimi nawaambieni, msiape kamwe; wala kwa mbingu, maana ni kiti cha enzi cha Mungu; wala kwa dunia, maana ni kiti chake cha kuwekea miguu; wala kwa Yerusalemu, maana ni mji wa Mfalme mkuu. Wala usiape kwa kichwa chako, maana huwezi kuufanya hata unywele mmoja kuwa mweupe au mweusi. Ukisema, ‘Ndiyo’, basi iwe ‘Ndiyo’; ukisema, ‘Siyo’, basi iwe kweli ‘Siyo’. Chochote kinachozidi hayo hutoka kwa yule Mwovu.
Ukatufanye chombo Chema Mungu wetu nasi tukatumike kama inavyokupendeza wewe..
Roho Mtakatifu akatuongoze katika yote na tukawe na kiasi..


“Mmesikia kwamba ilisemwa: ‘Jicho kwa jicho, jino kwa jino.’ Lakini mimi nawaambieni, usimlipize kisasi mtu mbaya. Mtu akikupiga kofi shavu la kulia, mgeuzie pia la pili. Mtu akikupeleka mahakamani kutaka kukuchukulia shati lako, mwache achukue pia koti lako. Mtu akikulazimisha kubeba mzigo wake kilomita moja, ubebe kilomita mbili. Akuombaye mpe, wala usimpe kisogo anayetaka kukukopa kitu. “Mmesikia kwamba ilisemwa: ‘Mpende jirani yako, na kumchukia adui yako.’ Lakini mimi nawaambieni, wapendeni maadui zenu na kuwaombea wale wanaowadhulumu nyinyi, ili mpate kuwa watoto wa Baba yenu aliye mbinguni. Kwa maana yeye huwaangazia jua lake watu wabaya na wema, na kuwanyeshea mvua watu wanyofu na waovu. Je, mtapata tuzo gani kwa kuwapenda tu wale wanaowapenda nyinyi? Hakuna! Kwa maana, hata watozaushuru hufanya hivyo! Kama mkiwasalimu ndugu zenu tu, je, mmefanya kitu kisicho cha kawaida? Hata watu wasiomjua Mungu nao hufanya vivyo hivyo. Basi, muwe wakamilifu kama Baba yenu wa mbinguni alivyo mkamilifu.
Mfalme wa amani tunaomba amani yako ikawe na ndugu zetu
waliokufa moyo,Yahweh wakawe salama moyoni,Mungu wetu ukawe 
tumaini kwa vote waliokata tamaa,waliokataliwa,wenye hofu na mashaka
Mungu wetu ukawaguse kwa mkono wako wenye nguvu na ukawaponye wagonjwa na ukawape nguvu/uvumilivu wale wanaowaguza..
Yahaweh tunaomba ukabariki mashamba/kazi na wakapate chakula chakutosha,kuweka akiba na kuwasaidia wenyengine wale wote wenye njaa..
Mungu wetu tunaomba ukawavushe salama wanaopitia magumu/majaribu mbalimbali..
Yahweh tunaomba ukawaguse masikini/wenye dhiki,shida/tabu Baba wa mbinguni ukaonekane katika maisha yao..
Mungu wetu ukawape ubunifu na maarifa ..
Yahweh tunaomba ukawaokoe na kuwaweka huru wale walio Katika vifungo vya yule mwovu,Mungu wetu ukawatendee walio magerezani
pasipo na hätiä haki ikatendeke..
Mfalme wa amani tunaomba ukawape neema ya kujiombea,shauku ya kusoma na kusimamia Neno lako nalo lika waweke huru..
Jehovah ukawatendee sawasawa na mapenzi yako..
Kwakuwa Ufalme ni wako Nguvu na Utukufu hata Milele..
Amina..!
Wapendwa/waungwana asanteni sana kwakuwa nami
Baba wa Upendo aendelee kuwabariki na kuwatendea
kama inavyompendeza yeye..
Amani ya Bwana wetu Yesu Kristo iwe nanyi daima..
Nawapenda.

Shauli anakutana na Samueli

1Katika kabila la Benyamini, kulikuwa na mtu mmoja tajiri aliyeitwa Kishi. Yeye alikuwa mtoto wa Abieli, mwana wa Zero, mwana wa Bekorathi, mwana wa Afia Mbenyamini. 2Kishi alikuwa na mtoto wa kiume aliyeitwa Shauli. Shauli alikuwa kijana mzuri, na hakuna mtu katika Israeli aliyelingana na Shauli kwa uzuri. Shauli alikuwa mrefu zaidi kuliko mtu yeyote katika nchi ya Israeli; watu wote walimfikia mabegani.
3Siku moja, punda wa Kishi, baba yake Shauli, walipotea. Hivyo, Kishi akamwambia Shauli, “Mchukue mmoja wa watumishi, uende kuwatafuta punda.” 4Wakawatafuta kwenye nchi ya milima ya Efraimu na eneo la Shalisha, lakini hawakuwaona huko. Halafu wakafika Shalimu, na huko hawakuwaona. Wakawatafuta katika nchi ya Benyamini, hata hivyo hawakuwapata. 5Walipofika kwenye nchi ya Sufu, Shauli alimwambia mtumishi wake, “Turudi nyumbani, la sivyo baba yangu ataacha kufikiria juu ya punda, na badala yake atakuwa na wasiwasi juu yetu.”
6Yule mtumishi akamwambia, “Ngoja kidogo; katika mji huu kuna mtu wa Mungu ambaye anaheshimiwa sana; kila asemalo huwa kweli. Sasa tumwendee, labda anaweza kutuambia jinsi safari yetu itakavyokuwa.” 7Shauli akamwuliza, “Lakini tukimwendea, tutampa nini? Tazama, mikate katika mifuko yetu imekwisha na hatuna chochote cha kumpa huyo mtu wa Mungu. Tuna nini?”
8Yule mtumishi akamjibu Shauli, “Ona, mimi nina fedha robo shekeli. Nitampa huyo mtu wa Mungu ili atuambie juu ya safari yetu.” 9(Hapo awali katika Israeli kama mtu akitaka kumwomba Mungu shauri, alisema, “Haya, njoo, twende kwa mwonaji.” Kwani mtu anayeitwa nabii siku hizi hapo awali aliitwa mwonaji). 10Shauli akamjibu, “Hilo ni jambo jema; haya, twende.” Hivyo, wakaenda kwenye mji alimokuwa anakaa yule mtu wa Mungu. 11Walipokuwa wanapanda mlima kuelekea mjini, wakakutana na wasichana waliokuwa wakienda kuteka maji. Wakawauliza wasichana hao, “Je, mwonaji yuko mjini?” 12Wale wasichana wakawajibu, “Ndiyo, yuko. Tena yuko mbele yenu; mkifanya haraka mtamkuta. Ameingia tu mjini leo, kwa sababu leo watu watatambika huko mlimani. 13Mara mtakapoingia mjini, mtamkuta kabla hajaenda mahali pa ibada mlimani ili kula. Maana watu hawatakula mpaka kwanza yeye abariki tambiko. Baadaye wale walioalikwa watakula. Hivyo nendeni haraka; mtakutana naye mara.” 14Hivyo Shauli na mtumishi wake walikwenda mjini. Walipokuwa wanaingia mjini, walimwona Samueli akitoka mjini, na anaelekea mahali pa juu.
15Jana yake, kabla Shauli hajafika mjini hapo, Mwenyezi-Mungu alikuwa amemwambia hivi Samueli: 16“Kesho, wakati kama huu, nitakuletea mtu kutoka nchi ya kabila la Benyamini, nawe utampaka mafuta kuwa mtawala wa watu wangu Israeli. Yeye atawaokoa watu wangu kutoka kwa Wafilisti, kwani nimeyaona mateso ya watu wangu na kilio chao kimenifikia.” 17Samueli alipomwona tu Shauli, Mwenyezi-Mungu alimwambia, “Huyu ndiye yule mtu niliyekuambia. Yeye ndiye atakayewatawala watu wangu.” 18Hapo Shauli alimwendea Samueli aliyekuwa karibu na lango la mji na kumwuliza, “Nakuomba unioneshe nyumba ya mwonaji.”
19Samueli akamjibu; “Mimi ndiye mwonaji. Nitangulieni kwenda mahali pa juu kwani leo mtakula pamoja nami. Kesho asubuhi maswali yote uliyo nayo nitayajibu. 20Kuhusu wale punda waliopotea siku tatu zilizopita, msiwe na wasiwasi juu yao; wamekwisha patikana. Lakini ni nani yule ambaye Waisraeli wanamtaka sana? Je, si wewe na jamaa yote ya baba yako?”
21Shauli akajibu: “Mimi ni wa kabila la Benyamini, kabila dogo kuliko makabila yote ya Israeli. Na katika kabila lote la Benyamini jamaa yangu ndiyo ndogo kabisa. Lakini, kwa nini unanizungumzia namna hiyo?”
22Kisha Samueli akampeleka Shauli na mtumishi wake sebuleni, akawapa mahali pa heshima, ambako wageni walioalikwa walikuwa wamekaa. Kulikuwa na wageni wapatao thelathini. 23Samueli akamwambia mpishi, “Lete ile sehemu niliyokupatia, nikakuambia uiweke kando.” 24Yule mpishi akaenda akaleta paja na sehemu ya nyama iliyokuwa upande wa juu9:24 Paja … juu: Makala ya Kiebrania si dhahiri. wa paja hilo na kuviweka mbele ya Shauli. Ndipo Samueli akamwambia Shauli, “Tazama kile ulichowekewa; sasa kimewekwa mbele yako. Sasa ule kwa sababu kimewekwa kwa ajili yako ili upate kula pamoja na wageni.”9:24 Tazama … wageni: Makala ya Kiebrania si dhahiri.
Hivyo, Shauli akala pamoja na Samueli siku hiyo. 25Waliporudi mjini kutoka mahali pa juu pa ibada, Shauli alitandikiwa kitanda kwenye paa la nyumba, akalala huko.

Samueli anampaka mafuta Shauli

26Alfajiri na mapema, Samueli alimwita Shauli kutoka darini: “Amka, ili nikusindikize urudi nyumbani.” Shauli aliamka, na wote wawili, yeye na Samueli, wakatoka na kwenda barabarani. 27Walipofika mwisho wa mji, Samueli akamwambia Shauli, “Mwambie huyo kijana atangulie mbele yetu.” Kijana alipokwisha ondoka, Samueli akaendelea kusema, “Ngoja kidogo, nami nitakufunulia yale aliyosema Mungu.”


1Samweli9;1-27

Biblia Habari Njema kwa Watu Wote(BHN)

"Swahili Na Waswahili"Mbarikiwe.

No comments: