Swahili na Waswahili

Swahili na Waswahili
Waswahili na Mswahili Rachel Siwa...Pamoja Daima!!

Friday 3 November 2017

Kikombe Cha Asubuhi ;Yoshua 19...



Shalom,Habari za Asubuhi,Hamjambo,Mmeamkaje?

Tumshukuru Mungu wetu katika yote..

Mtakatifu..!Mtakatifu.!Mtakatifu..!Baba wa Mbinguni..
Mungu wetu,Baba yetu,Muumba wetu,Mungu wa wote walio hai..
Mungu wa Abrahamu,Isaka na Yakobo...
Muweza wa yote,kimbilio letu,Mungu mwenye huruma,Mponyaji wetu
Baba wa upendo,Baba wa yatima,Baba wa baraka na amani..
Jehovah Jireh..!Jehovah Rapha..!Jehovah Nissi..!Jehovah Raah..!
Jehovah Shammah,Jehovah Shalom..!Emanueli-Mungu pamoja nasi..!!

Asante Baba wa Mbinguni kwa wema na fadhili zako kwetu..
Asante kwa kutuchagua tena na kutupa kibali cha kuendelea
kuiona leo hii..
Asante kwa pumzi/uzima,afya na kuwa tayari katika majukumu yetu..

Tunakuja mbele zako Mungu wetu tukijinyenyekeza,tukijishusha
na kujiachilia mikononi mwako Baba wa Mbinguni..
Tunaomba utusamehe makosa yetu yote tuliyoyafanya
kwakuwaza,kwakunena,kwakutenda,kwakujua/kutojua Jehovah..
Yahweh nasi tunaomba utupe neema ya kuweza kuwasamehe
wale wote waliotukosea..
Mungu wetu tunaomba utuepushe katika majaribu Yahweh utuokoe
na yule mwovu na kazi zake zote..
Baba wa Mbinguni tunaomba ututakase miili yetu na akili zetu
Mungu wetu utufunike kwa damu ya Bwana wetu Yesu Kristo wa Nazareti
Yeye aliteseka kwanza ili sisi tupate kupona..


Hatimaye, ndugu, tuombeeni ili ujumbe wa Bwana uzidi kuenea upesi na kupokelewa kwa heshima kama vile ulivyo kati yenu. Ombeni pia ili Mungu atuokoe na watu wapotovu na waovu, maana si wote wanauamini ujumbe huu. Lakini Bwana ni mwaminifu. Yeye atawaimarisheni na kuwalinda salama na yule Mwovu. Naye Bwana anatupatia tumaini kubwa juu yenu, na hatuna shaka kwamba mnafanya na mtaendelea kufanya yale tuliyowaambieni. Bwana aiongoze mioyo yenu katika upendo wa Mungu na katika uvumilivu tunaopewa na Kristo.

Jehovah tunaomba ukabariki kazi za mikono yetu Yahweh
ukatupe ubunifu,maarifa katika yote tunayoenda kufanya
Baba wa Mbinguni tukafanye/kutenda sawasawa na mapenzi yako..
Mungu wetu ukabariki ridhiki zetu ziingiazo/zitokazo...
 Yahweh nasi tunaomba utupe neema ya kuweza kuwabariki wenye kuhitaji..
Jehovah tunaomba tusipungukiwe katika mahitaji yetu
Yahweh ukatupe sawasawa na mapenzi yako..


Ndugu, tunawaamuru kwa jina la Bwana wetu Yesu Kristo, mjiepushe na ndugu wote walio wavivu na ambao hawafuati maagizo tuliyowapa. Nyinyi wenyewe mnajua kwamba mnapaswa kufuata mfano wetu. Sisi tulipokuwa nanyi hatukuwa wavivu; hatukula chakula kwa mtu yeyote bila ya kumlipa. Tulifanya kazi kwa bidii na taabu mchana na usiku ili tusiwe mzigo kwa mtu yeyote kati yenu. Tulifanya hivyo si kwa kuwa hatuna haki ya kutaka msaada wenu, ila kwa sababu tunataka kuwapeni mfano. Tulipokuwa pamoja nanyi tulikuwa tukiwaambieni, “Mtu yeyote asiyependa kufanya kazi, asile chakula.” Tunasema mambo hayo kwa sababu tumesikia kwamba wako baadhi yenu ambao ni wavivu na ambao hawafanyi chochote, isipokuwa tu kujiingiza katika mambo ya watu wengine. Kwa jina la Bwana wetu Yesu Kristo tunawaamuru na kuwaonya watu hao wawe na nidhamu na kufanya kazi ili wajipatie maslahi yao wenyewe. Lakini nyinyi ndugu, msichoke kutenda mema. Huenda kwamba huko kuna mtu ambaye hatautii huu ujumbe tunaowapelekeeni katika barua hii. Ikiwa hivyo, basi, mfichueni mtu huyo na msiwe na uhusiano wowote naye, kusudi aone aibu. Lakini msimtendee mtu huyo kama adui, bali mwonyeni kama ndugu.

Mfalme wa amani tunaomba amani yako ikatawale katika
nyumba/ndoa zetu,watoto,wazazi wetu,familia/ndugu na wote
wanaotuzunguka,Mungu wetu tunaomba ulinzi wako kwetu
na kwa vyote tunavyo vimiliki..Baba wa Mbinguni ukatamalaki na
kutuatamia,Ukatubariki na kututendea kama inavyokupendeza wewe
Yahweh ukatupe neema ya kusimamia Neno lako amri na sheria zako
siku zote za maisha yetu,Ukatuokoe na majivuno,ubinafsi,fitina,
kiburi,unafiki,usengenyaji,uchoyo,makwazo na ukatupe neema
ya kuombeana/kujiombea,kufuata njia zako na kuelimishana/kuonyana
kwa upole na amani,Upendo kati yetu na ukadumu..
Tukawe barua njema popote tupitapo na tukasome vyema..
Roho Mtakatifu akatuongoze katika yote na tukawe na kiasi..


Bwana mwenyewe ambaye ndiye chanzo cha amani, awajalieni amani siku zote kwa kila namna. Bwana awe nanyi nyote. Kwa mkono wangu mwenyewe naandika hivi: Salamu kutoka kwa Paulo! Hivi ndivyo ninavyotia sahihi kila barua; ndivyo ninavyoandika. Tunawatakieni nyote neema ya Bwana wetu Yesu Kristo.

Mungu wetu ukawaguse kwa mkono wako na ukawape neema
ya kujiombea wagonjwa ukawape uponyaji wa mwili na roho
wenye njaa ukawape chakula na kubariki mashamba yao..
wanaopitia magumu/majaribu baba ukawape njia ya kuvuka..
waliokatika vifungo mbali mbali vya yule mwovu Mungu wetu
ukawafungue na kuwaweka huru,ukawape amani moyoni na
ukawape neema ya kujua njia zako na kufuata ili wawe huru..
ee Mungu wetu ukasikie kilio cha watoto wako Baba ukawafute
machozi na ukawatendee kama inavyo kupendeza wewe..


Lakini nyinyi wapenzi wangu, kumbukeni yale mliyoambiwa hapo awali na mitume wa Bwana wetu Yesu Kristo. Waliwaambieni: “Siku za mwisho, watatokea watu watakaowadhihaki nyinyi, watu wafuatao tamaa zao mbaya.” Hao ndio wanaosababisha mafarakano, watu wa fikira za kidunia, wasio na Roho wa Mungu. Lakini nyinyi, wapenzi wangu, jijengeni wenyewe juu ya imani yenu takatifu kabisa. Salini kwa nguvu ya Roho Mtakatifu, na kudumu katika upendo wa Mungu, mkimngojea Bwana wetu Yesu Kristo ambaye, kwa huruma yake, atawajalieni uhai wa milele. Muwe na huruma kwa watu walio na mashaka; waokoeni kwa kuwanyakua kutoka motoni. Lakini kwa wengine muwe na huruma pamoja na tahadhari, mkichukia hata mavazi yao yenye madoa ya tamaa zao mbaya.

Sifa na Utukufu tunakurudishia Mungu wetu..
Kwakuwa Ufalme ni wako Nguvu na Utukufu hata Milele..
Amina...!

Asanteni sana wapendwa katika Bwana kwakuwa nami
Baba wa upendo aendelee kuwabariki na kuwatendea
sawasawa na mapenzi yake..
Nawapenda.


Nchi waliyopewa kabila la Simeoni

1Kura ya pili ilizipata koo za kabila la Simeoni na sehemu yao ya nchi ilikuwa imezungukwa na ile ya kabila la Yuda. 2Kabila la Simeoni lilipata miji ya Beer-sheba, Sheba, Molada 3Hasar-shuali, Bala, Esemu, 4Eltoladi, Bethuli, Horma, 5Siklagi, Beth-markabothi, Hasar-susa, 6Beth-lebaothi na Sharuheni. Jumla ya miji waliyopewa ni kumi na mitatu pamoja na vijiji vyake. 7Pia kulikuwa na miji ya En-rimoni, Etheri, na Ashani. Jumla ya miji waliyopewa ni minne pamoja na vijiji vyake. 8Taz 1Nya 4:28-33 Pamoja na vijiji vyote vilivyoizunguka miji hiyo hadi Baalath-beeri, (au Rama) ya Negebu. Hizo zote ni sehemu zilizopewa koo za kabila la Simeoni. 9Kwa vile eneo lililopewa kabila la Yuda lilikuwa kubwa kuliko kabila hilo lilivyohitaji, sehemu ya eneo lake lilipewa kabila la Simeoni.

Nchi waliyopewa kabila la Zebuluni

10Kura ya tatu ilizipata koo za kabila la Zebuluni. Eneo lao lilienea hadi Saridi. 11Kutoka huko mpaka wake ulikwenda magharibi hadi Mareali, ukapitia pembeni mwa Dabeshethi na kwenda kwenye kijito kilichoko mashariki ya Yokneamu. 12Kutoka Saridi, mpaka huo ulielekea mashariki hadi kwenye mpaka wa Kisloth-tabori, na kutoka huko ukapita Daberathi hadi Yafia. 13Kutoka Yafia uliendelea mashariki hadi Gath-heferi, Eth-kasini, na kuendelea hadi Rimoni ambako ulipanda kuelekea Nea. 14Upande wa kaskazini mpaka uligeuka kuelekea Hanathoni na kuishia kwenye bonde la Yiftaheli. 15Ukajumuisha miji ya Katathi, Nahalali, Shimroni, Yidala na Bethlehemu. Jumla ya miji waliyopewa ni kumi na miwili pamoja na vijiji vyake. 16Hiyo ndiyo sehemu zilizopewa koo za kabila la Zebuluni miji hiyo pamoja na vijiji vyake.

Nchi ya kabila la Isakari

17Kura ya nne ilizipata koo za kabila la Isakari. 18Eneo lenyewe lilikuwa na miji ya Yezreeli, Kesulothi, Shunemu, 19Hafaraimu, Shioni, Anaharathi, 20Rabithi, Kishioni, Ebesi, 21Remethi, En-ganimu, En-hada na Beth-pasesi. 22Kadhalika, mpaka wao ulifika Tabori, Shahasuma, Beth-shemeshi na kuishia kwenye mto Yordani. Jumla ya miji waliyopewa ni kumi na sita pamoja na vijiji vyake. 23Hizo ndizo sehemu zilizopewa koo za kabila la Isakari; miji hiyo pamoja na vijiji vyake.

Nchi ya kabila la Asheri

24Kura ya tano ilizipata koo za kabila la Asheri. 25Eneo la nchi yao lilikuwa na miji ya Helkathi, Hali, Beteni, Akshafi, 26Alameleki, Amadi na Mishali. Kwa upande wa magharibi mpaka uligusana na Karmeli na Shihor-libnathi. 27Kisha ukageuka kuelekea mashariki kwenda Beth-dagoni ambako unagusana na Zebuluni na bonde la Iftaheli. Halafu ukaendelea kaskazini hadi Beth-emeki, Neieli na kuzidi kuelekea kaskazini hadi Kabuli, 28Ebroni, Rehobu, Hamoni, Kana hadi Sidoni Kuu. 29Hapo, mpaka uligeuka kuelekea Rama na kufikia kwenye mji wa Tiro uliokuwa na ngome. Kisha ukageuka kuelekea Hosa na kuishia kwenye bahari ya Mediteranea. Miji mingine iliyokuwamo ni Maharabu, Akzibu, 30Uma, Afeka na Rehobu. Jumla ya miji waliyopewa ni ishirini na miwili pamoja na vijiji vyake. 31Sehemu hizo ndizo zilizopewa koo za kabila la Asheri; miji hiyo pamoja na vijiji vyake.

Nchi ya kabila la Naftali

32Kura ya sita ilizipata koo za kabila la Naftali. 33Mpaka wake ulianzia Helefu na mwaloni mwa Zaananimu, ukapita Adami-nekebu na Yabneeli hadi Lakumu na kuishia kwenye mto Yordani. 34Kutoka hapo mpaka ulikwenda magharibi kuelekea Aznoth-tabori; toka huko ukaenda Hukoki na kugusana na pembe ya kusini ya eneo la kabila la Zebuluni; kisha kugusana na eneo la kabila la Asheri upande wa magharibi, na kugusana na eneo la kabila la Yuda. Kwa upande wa mashariki mpaka ukiingilia kwenye mto Yordani.19:34 Yordani: Makala ya Kiebrania: Yuda mtoni Yordani. 35Miji yao iliyokuwa na ngome ni Zidimu, Zeri, Hamathi, Rakathi, Kinerethi, 36Adama, Rama, Hazori, 37Kedeshi, Edrei, En-hazori, 38Yironi, Migdaleli, Horemu, Beth-anathi na Beth-shemeshi. Jumla ya miji waliyopewa ni kumi na tisa pamoja na vijiji vyake. 39Hizo ndizo sehemu zilizopewa koo za kabila la Naftali; miji hiyo pamoja na vijiji vyake.

Nchi ya kabila la Dani

40Kura ya saba ilizipata koo za kabila la Dani. 41Eneo la nchi yao lilikuwa na miji ya Sora, Eshtaoli, Ir-shemeshi 42Shaalabini, Aiyaloni, Yithla, 43Eloni, Timna, Ekroni 44Elteke, Gibethoni, Baalathi, 45Yehudi, Bene-beraki, Gath-rimoni, 46Me-yarkoni na Rakoni na nchi iliyokuwa karibu na Yopa. 47Taz Amu 18:27-29 Watu wa kabila la Dani walipopoteza nchi yao, walikwenda na kuushambulia mji wa Leshemu. Waliushinda na kuuteka, na baada ya kuwaua wakazi wake wote, waliumiliki halafu wakabadili jina la mji huo kuwa Dani; jina ambalo lilikuwa ni la babu yao. 48Hizo ndizo sehemu zilizopewa koo za kabila la Dani; miji hiyo pamoja na vijiji vyake.

Ugawanyaji wa mwisho

49Walipomaliza kugawiana sehemu zote za nchi, Waisraeli walimpa Yoshua, mwana wa Nuni, sehemu yake katikati yao. 50Kulingana na amri ya Mwenyezi-Mungu walimpa mji ambao aliuchagua yeye mwenyewe, yaani Timnath-sera, ambao ulikuwa katika nchi ya milima ya Efraimu. Naye Yoshua akaujenga upya mji huo na kukaa humo.
51Basi, kuhani Eleazari na Yoshua, mwana wa Nuni, pamoja na viongozi wa makabila ya Waisraeli waligawa sehemu hizo kwa kura mbele ya Mwenyezi-Mungu mlangoni mwa hema la mkutano huko Shilo. Basi, wakakamilisha kuigawa nchi.

Yoshua 19;1-51

Biblia Habari Njema kwa Watu Wote(BHN)

"Swahili Na Waswahili"Mbarikiwe.

No comments: