Swahili na Waswahili

Swahili na Waswahili
Waswahili na Mswahili Rachel Siwa...Pamoja Daima!!

Wednesday 1 November 2017

Kikombe Cha Asubuhi ;Yoshua 17...



Shalom,Habari za Asubuhi,Hamjambo,Mmeamkaje?
Ni siku/mwezi Mwingine tena Mungu wetu ametuchagua na kutupa
kibali cha kuendelea kuiona leo hii...
Tumempa nini Mungu?Tumetenda wema gani?Tumekuwa wazuri sana?
Tumekuwa wenye nguvu/utashi ndiyo maana ametutendea haya?
Tumetenda yote yanayompendeza Mungu?Tumekuwa kiroho?
Hapana si kwamba sisi si wakosaji au wema sana zaidi ya wengine
ambao leo hii hawakuweza kuiona siku hii,na wengine wapo hoi
vitandani hawawezi hata kujigeuza,wengine hawana kauli ya hata kumuita
Mungu na kutubu,Mimi na wewe ni nani na jee tumechukuliaje Neema/rehema hii? kwa maana ni kwa mapenzi yake sisi kuwa hivi
tulivyo leo,Kwake yeye yote yanawezekana,tuwe tayari hatujui
muda wala siku Mwana wa Mungu yuaja...

“Muwe tayari mmejifunga mkanda kiunoni, na taa zenu ziwe zinawaka; muwe kama watumishi wanaomngojea bwana wao arudi kutoka harusini, ili wamfungulie mara atakapobisha. Heri yao watumishi wale ambao bwana wao atakaporudi atawakuta wanakesha! Nawaambieni hakika, huyo bwana atajifunga mkanda kiunoni, atawaketisha mezani na kuwahudumia. Hata kama atarudi usiku wa manane au alfajiri na kuwakuta wanakesha, heri yao watumishi hao! Jueni kwamba, kama mwenye nyumba angejua saa ambayo mwizi atakuja, angekesha, wala hangeiacha nyumba yake ivunjwe. Nanyi, kadhalika muwe tayari, maana Mwana wa Mtu atakuja saa msiyoitazamia.”


Asante Baba wa Mbinguni kwa  wema na fadhili zako kwetu
Asante kwa ulinzi wako kwetu wakati wote..
Utukuzwe ee Mungu wetu,Usifiwe ee Baba wa Mbinguni,Unastahili
kuabudiwa Jehovah,Unastahili kuheshimiwa Yahweh,Unastahili
kuhimidiwa Mungu wetu,Unatosha Baba wa Mbinguni,Matendo yako
ni makuu mno,Matendo yako ni ya ajabu...!!

Haleluya! Msifuni Mwenyezi-Mungu! Mshukuruni Mwenyezi-Mungu kwa kuwa ni mwema; kwa maana fadhili zake zadumu milele! Ni nani awezaye kutaja matendo ya Mwenyezi-Mungu? Ni nani awezaye kumsifu kama anavyostahili? Heri wale wanaotekeleza haki, wanaotenda daima mambo yaliyo sawa. Unikumbuke ee Mwenyezi-Mungu unapowafadhili watu wako; unisaidie wakati unapowaokoa; ili niweze kuona fanaka ya wateule wako, nipate kufurahia furaha ya taifa lako, na kuona fahari pamoja na watu wako.

Tazama jana imepita Mungu wetu leo ni siku mpya na kesho ni
siku nyingine Baba wa Mbinguni tunakuja mbele zako tukijinyenyekeza,
tukijishusha,tujiachilia mikononi mwako Jehovah..
Tunaomba utusamehe dhambi zetu zote tulizo zifanya kwakuwaza,
kwakunena,kwakutenda,kwakujua/kutojua...
Baba wa Mbinguni tunaomba nasi utupe neema ya kuweza
kuwasamehe wale wote waliotukosea..
Mungu wetu tunaomba utuepushe  katika majaribu Baba na utuokoe na yule mwovu na kazi zake zote...
Yahweh tunaomba ututakase miili yetu na akili zetu Jehovah
tunaomba
  utufunike kwa damu ya Bwana wetu Yesu Kristo wa Nazareti..
Yeye aliteseka kwanza ili sisi tupate kupona..

Sisi tunayo madhabahu ambayo wale wanaotumikia bado katika hema la Wayahudi hawana haki ya kula vitu vyake. Kuhani mkuu wa Kiyahudi huleta damu ya wanyama katika Mahali Patakatifu na kuitoa tambiko kwa ajili ya dhambi; lakini nyama za hao wanyama huteketezwa nje ya kambi. Ndiyo maana Yesu pia, kusudi apate kuwatakasa watu kwa damu yake mwenyewe, aliteswa na kufa nje ya mji. Basi, tumwendee huko nje ya kambi tukajitwike laana yake. Maana hapa duniani hatuna mji wa kudumu; lakini tunautafuta ule unaokuja. Basi, kwa njia ya Yesu, tumtolee Mungu tambiko ya sifa daima, yaani sifa zinazotolewa kwa midomo inayoliungama jina lake.

Mungu wetu tunaomba ukabariki kazi za mikono yetu,Biashara,
mashamba,masomo na yote tunayoenda kufanya/kutenda
Mungu wetu tukatende sawasawa na mapenzi yako..
Yahweh tunaomba ukabariki ridhiki zetu ziingiazo/zitokazo
Jehova nasi tunaomba utupe neema ya kuweza kuwabariki
wenye kuhitaji..

Jishughulishe na biashara hata kama kwa kubahatisha; yawezekana baadaye ukapata chochote kile. Wagawie watu saba hata wanane sehemu yako, maana, hujui balaa litakalofika duniani. Mawingu yakijaa maji, mvua hunyesha; mti ukiangukia kusini au kaskazini, hapo uangukiapo ndipo ulalapo. Anayengoja upepo hatapanda mbegu, anayesubiri mawingu yatoweke, hatavuna kitu. Usivyojua jinsi uhai unavyoingia katika mifupa ya mtoto tumboni mwa mamake, kadhalika huwezi kuelewa matendo ya Mungu, ambayo hufanya kila kitu. Panda mbegu asubuhi na jioni usiache kupanda, maana, hujui zipi zitaota; za asubuhi, za jioni, au zote zitakuwa nzuri. Mwanga wafaa, na kuliona jua kwapendeza macho. Mtu akiishi miaka mingi, na aifurahie miaka hiyo yote; lakini akumbuke kuwa siku za giza zitakuwa nyingi, na kwamba yote yatakayofuata ni bure.


Baba wa Mbinguni tusipungukiwe katika mahitaji yetu
Yahweh ukatupe kama inavyo kupendeza wewe..
Mfalme wa amani tunaomba amani yako ikatawale katika
nyumba zetu,watoto,wazazi wetu,familia/ndugu na
wote wanaotuzunguka,Baba wa Mbinguni tunaomba ulinzi
wako kwetu na vyote tunavyovimiliki,Yahweh ukatamalaki na kutuatamia
Jehovah ukatupe neema ya kusimamia Neno lako,amri na sheria zako
siku zote za maisha yetu,Baba wa mbinguni tukawe na shauku/kiu
ya kusoma Neno lako,kufuata njia zako na ukatupe neema
ya kukumbushana/kuelimishana kwa upendo,amani katika mioyo yetu,
tuka nene yaliyo yako,tukapate kutambua/kujitambua..

Kisha, nilitoa maagizo kuwa sote tufike karibu na mto Ahava ili tufunge na kujinyenyekeza mbele za Mungu wetu na kumwomba atulinde na kutuongoza katika safari yetu pamoja na watoto wetu. Ingekuwa aibu kubwa kwangu kumwomba mfalme kikosi cha askari na wapandafarasi wa kutulinda na adui njiani maana nilikuwa nimekwisha mwambia kuwa Mungu wetu huwabariki wote wanaomtafuta, lakini huwachukia na kuwaadhibu wote wanaomwacha. Kwa hiyo tulifunga na kumwomba Mungu atulinde, naye aliyasikia maombi yetu.

Ee Baba tunaomba upokee sala/maombi yetu..
Baba wa Mbinguni tunaomba ukawaguse kwa mkono wako
wenye nguvu na uponyaji,Yahweh tunaomba ukawaponye wagonjwa,
Baba wa Mbinguni ukawatendee na kuwapa maarifa wenye njaa
Jehovah tunaomba ukawafungue walio katika vifungo mbalimbali
vya yule mwovu,Yahweh ukwape tunaini wale wote walikata tamaa..
Baba wa Mbinguni ukawaponye kiro/mwili na ukasikie kulia kwao
Yahweh ukawafute machozi ya watoto wako ukapokee sala/maombi
yao na ukawape neema ya kujiombea,wakasimamie njia zako
Nuru ikaangaze katika maisha yao..
Kwa imani tunayaweka haya yote mikononi mwako Jehovah..
Sifa na utukufu tunakurudishia Mungu wetu..
Kwakuwa Ufalme ni wako Nguvu na utukufu hata Milele..
Amina..!!

Asanteni sana wapendwa katika Bwana kwa kuwa nami
Amani ikatawale katika maisha yenu,Baraka na upendo,
Na Mungu aendelee kuwatendea katika yote yampendezayo yeye
Nawapenda..

1Watu wa kabila la Manase ambaye alikuwa mzaliwa wa kwanza wa Yosefu, pia walipewa eneo lao kwa kura. Makiri, mzaliwa wa kwanza wa Manase na baba yake Gileadi, alikwishapewa kwa kura miji ya Gileadi na Bashani, maana alikuwa hodari vitani. 2Wengine waliobaki wa kabila la Manase walipewa sehemu yao kwa kura kulingana na koo zao. Koo hizo zilikuwa zile za Abiezeri, Heleki, Asrieli, Shekemu, Heferi na Shemida ambao wote walikuwa wazawa wa kiume wa Manase mwana wa Yosefu.
3Lakini Selofehadi mwana wa Heferi, mwana wa Gileadi, mwana wa Makiri, mwana wa Manase, hakuwa na watoto wa kiume, bali alikuwa na watoto wa kike tu, nao walikuwa: Mahla, Noa, Hogla, Milka na Tirza. 4Taz Hes 27:1-7 Mabinti hao wakamjia kuhani Eleazari na Yoshua, mwana wa Nuni, na viongozi wengine wakawaambia, “Mwenyezi-Mungu alimwamuru Mose atugawie na sisi sote nchi kama wagawiwavyo wanaume wa kabila letu.” Basi kufuatana na amri ya Mwenyezi-Mungu, Yoshua akawapatia sehemu yao kama alivyowapa wanaume wa kabila lao. 5Kwa hiyo kabila la Manase liliongezewa sehemu mbili zaidi yaani nchi ya Gileadi na Bashani iliyoko upande mwingine wa mto Yordani, 6kwa sababu binti za Manase waligawiwa sehemu zao kama walivyogawiwa wanaume wa kabila lao. (Nchi ya Gileadi walipewa wazawa wengine wa Manase).
7Eneo la kabila la Manase lilianzia Asheri na kwenda hadi Mikmethathi mashariki ya Shekemu; halafu mpaka wao ukaendelea kusini hadi kwenye nchi ya wakazi wa En-tapua. 8Nchi ya Tapua ilikuwa mali yake Manase, lakini mji wa Tapua, ambao ulikuwa mpakani, ulikuwa mali ya wazawa wa Efraimu. 9Mpaka huo uliendelea hadi kijito cha Kana. Miji iliyokuwa kusini ya Kana ilikuwa ya Waefraimu hata ingawa ilikuwa katika nchi ya kabila la Manase. Halafu mpaka ukapita kaskazini ya kijito Kana na kuishia bahari ya Mediteranea. 10Eneo la kusini lilikuwa la kabila la Efraimu na eneo la kaskazini lilikuwa la kabila la Manase, mpaka wake ukiwa bahari ya Mediteranea kwa upande wa magharibi. Kabila la Asheri lilikuwa kaskazini-magharibi ya eneo la Manase na kaskazini-mashariki lilikuwa kabila la Isakari. 11Vilevile katika nchi ya kabila la Isakari na kabila la Asheri, kabila la Manase lilipatiwa miji ya Beth-sheani na Ibleamu pamoja na vijiji vyake, na miji ya Dori, En-dori, Taanaki na Megido pamoja na wakazi na vijiji vyake; na pia theluthi ya Nafathi.17:11 makala ya Kiebrania si dhahiri. 12Taz Amu 1:27-28 Lakini wazawa wa Manase hawakuweza kuwafukuza wakazi wa miji hiyo, Wakanaani wakaendelea kuishi humo, 13ingawa hata baada ya Waisraeli kuwa na nguvu zaidi, hawakuweza kuwafukuza ila tu waliwafanyisha kazi za kulazimishwa.
14Watu wa kabila la Yosefu walimwendea Yoshua, wakamwambia, “Kwa nini umetugawia sehemu moja tu ya nchi sisi ambao Mwenyezi-Mungu ametubariki hata akatufanya tuwe wengi sana?” 15Yoshua akawajibu, “Kama mmekuwa wengi hivyo, hata nchi ya milima ya Efraimu haiwatoshi tena, basi nendeni msituni katika nchi ya Waperizi na ya Warefai, mkaufyeke msitu huo na kufanya makao yenu huko.” 16Nao wakamjibu, “Ni kweli kwamba nchi hii ya milima haitutoshi; hata hivyo wale Wakanaani wote wanaokaa kwenye tambarare wana magari ya chuma, vilevile wale wote wanaokaa Beth-sheani pamoja na vijiji vyake, na wale wanaoishi katika Bonde la Yezreeli.”
17Basi, Yoshua akawaambia wazawa wa Yosefu, yaani kabila la Efraimu na Manase, “Kweli nyinyi mmekuwa wengi na wenye uwezo mkubwa. Haifai mpate sehemu moja tu, 18bali pia nchi ya milima itakuwa yenu. Ingawa sasa ni msitu, mtaifyeka na kuimiliki yote toka upande huu hadi upande mwingine. Mtawaondoa Wakanaani, hata kama wana magari ya chuma na ni wenye nguvu.”


Yoshua 17;1-17

Biblia Habari Njema kwa Watu Wote(BHN)

"Swahili Na Waswahili"Mbarikiwe.

No comments: