Swahili na Waswahili

Swahili na Waswahili
Waswahili na Mswahili Rachel Siwa...Pamoja Daima!!

Monday 20 November 2017

Kikombe Cha Asubuhi ;Waamuzi 6...



Shalom,Habari za Asubuhi,Hamjambo,Mmeamkaje?

Haleluyah Mungu wetu yu mwema sana..
Ni siku/wiki nyingine tena Mungu wetu ametuchagua na kutupa
kibali cha kuendelea kuiona siku hii...
Si kwamba tumetenda mema sana,wala si kwamba sisi ni wazuri mno
si kwa nguvu/utashi wetu,wala si kwa akili zetu sisi kuwa hivi
tulivyo leo hii....
Ni kwa neema/rehema zake,Ni kwa mapenzi yake  Mungu wetu..


Palitokea manabii wa uongo kati ya watu, na vivyo hivyo waalimu wa uongo watatokea kati yenu. Watu hao wataingiza mafundisho maharibifu na kumkana Bwana aliyewakomboa, na kwa njia hiyo watasababisha ghafla maangamizi yao wenyewe. Tena watu wengi watazifuata hizo njia zao mbaya, na kwa sababu yao wengine wataipuuza njia ya ukweli. Kwa tamaa yao mbaya watajipatia faida kwa kuwaambieni hadithi za uongo. Lakini kwa muda mrefu sasa Hakimu wao yuko tayari, na Mwangamizi wao yuko macho! Malaika walipotenda dhambi, Mungu hakuwahurumia, bali aliwatupa katika moto wa Jehanamu ambako wamefungwa wakingojea siku ile ya hukumu. Mungu hakuihurumia dunia ya hapo kale, bali alileta gharika kuu juu ya nchi ile ya watu wasiomcha Mungu; lakini Noa ambaye alihubiri uadilifu, Mungu alimwokoa pamoja na watu wengine saba. Mungu aliiadhibu miji ya Sodoma na Gomora, akaiteketeza kwa moto, akaifanya iwe mfano wa mambo yatakayowapata watu wasiomcha Mungu.
Tumshukuru Mungu wetu kwa wema na fadhili zake kwetu...
Asante Baba wa Mbinguni kwa ulinzi wako wakati wote..
Asante kwa uzima/pumzi,afya na kuwa tayari katika majukumu yetu..
Utukuzwe ee Mungu wetu,Usifiwe Baba wa Mbinguni,Uhimidiwe Jehovah,
Uabudiwe Yahweh,Matendo yako ni makuu mno,Matendo yako ni ya ajabu
Sifa na Utukufu tunakurudishia Mungu wetu..!!


Baba wa Mbinguni tunakuja mbele zako tukijinyenyekeza,tukijishusha
na kujiachilia mikononi mwako Yahweh...
Tunaomba utusamehe dhambi zetu zote tulizozifanya kwakuwaza,
kwakunena,kwakutenda,kwakujua/kutojua..
Mungu wetu nasi tunaomba utupe neema ya kuweza kuwasamehe wale
wote waliotukosea..
Yahweh tunaomba utuepushe katika majaribu Baba utuokoe na
yule mwovu na kazi zake zote..
Jehovah tunaomba ututakase miili yetu na akili zetu Yahweh utufunike
kwa Damu ya Mwanao Mpendwa Bwana na Mwokozi wetu Yesu Kristo
wa Nazareti maana yeye aliteseka kwanza ili sisi tupate kupona..



Alimwokoa Loti, mtu mwema, ambaye alisikitishwa sana na mwenendo mbaya wa watu hao waasi. Loti aliishi miongoni mwa watu hao, na kwa siku nyingi moyo wake ulikuwa katika wasiwasi mkuu aliposikia matendo yao maovu. Kwa hiyo, basi, Bwana anajua jinsi ya kuwaokoa katika majaribu watu wanaomcha Mungu, na jinsi ya kuwaweka waovu katika adhabu hadi siku ile ya hukumu, hasa wale wanaofuata tamaa mbaya za mwili na kupuuza mamlaka. Watu hao ni wakaidi na wenye majivuno, huvitukana na hawaviheshimu viumbe vitukufu vya juu. Lakini malaika ambao wana uwezo na nguvu kuliko hao waalimu wa uongo, hawawashtaki na kuwatukana hao mbele ya Bwana. Watu hao ambao hutukana chochote kile wasichoelewa, ni sawa na wanyama wasio na akili ambao huzaliwa na baadaye hukamatwa na kuchinjwa! Wataangamizwa kutokana na uharibifu wao wenyewe, na watalipwa mateso kwa mateso ambayo wameyasababisha. Furaha yao ni kufanya, tena mchana kabisa, chochote kinachotosheleza anasa zao za mwili. Hao ni fedheha na aibu tupu kwa jumuiya yenu wakati wanapojiunga nanyi katika karamu zenu, hali wakifurahia njia zao za udanganyifu. Macho yao yamejaa uzinzi na uwezo wao wa kutenda dhambi hauna kikomo. Huwaongoza watu walio dhaifu mpaka mitegoni. Mioyo yao imezoea kuwa na tamaa ya mali. Wapo chini ya laana ya Mungu! Wameiacha njia iliyonyoka, wakapotoka na kuifuata njia aliyofuata Balaamu, mwana wa Beori ambaye alipendelea kupata faida kwa kufanya udanganyifu, akakaripiwa kwa ajili ya uovu wake. Punda ambaye hasemi, alinena kwa sauti ya binadamu, akaukomesha wazimu wa huyo nabii.




Baba wa Mbinguni tunaomba ukabariki kazi za mikono yetu..
Yahweh tunaomba ukatupe ubunifu,maarifa katika ufanyaji/utendaji
Baba nasi tukatende sawasawa na mapenzi yako....
Mungu wetu tunaomba ukabariki ridhiki zetu ziingiazo/zitokazo
Jehovah nasi tunaomba utupe neema ya kuweza kuwabariki wenye kuhitaji


Mfalme wa amani tunaomba amani yako ikatawale katika maisha yetu
Jehovah ukabariki nyumba/ndoa zetu,watoto,wazazi wetu,familia/ndugu
na wote wanaotuzunguka,Baba wa Mbinguni tunaomba ulinzi wako kwetu
na kwa vyote tunavyovimiliki,Yahweh ukatamalaki na kutuatamia,Mungu wetu ukatupe neema ya kufuata njia zako,Kusimamia Neno lako amri
na sheria zako siku zote za maisha yetu..Baba wa Mbinguni ukatupe
amani moyoni, utu wema,fadhili,unyenyekevu,hekima,busara,upendo,
tukaonyane/kuelimishana kwa upole na amani,tuakchuliane na kusamehena,Mungu wetu ukaonekane katika maisha yetu,tupate kutambua/kujitambua,ukatufanye barua njema nasi tukasomeke kama
inavyokupendeza wewe..
Roho Mtakatifu akatuongoze katika yote na tukawe na kiasi..

Watu hao ni kama chemchemi zilizokauka, kama mawingu yanayopeperushwa na tufani; makao yao waliyowekewa ni mahali pa giza kuu. Husema maneno ya majivuno na yasiyo na maana, na kutumia tamaa zao mbaya za kimwili kuwatega wale ambao wamejitenga hivi karibuni na watu waishio katika udanganyifu. Huwaahidi watu wengine eti watakuwa huru, kumbe wao wenyewe ni watumwa wa upotovu – maana mtu ni mtumwa wa chochote kile kinachomtawala. Watu waliokwisha ponyoka katika upotovu wa ulimwengu kwa kupata kumjua Bwana na Mwokozi wetu Yesu Kristo, kisha wakakubali kunaswa na kutawaliwa tena na upotovu huo, hali yao itakuwa mbaya zaidi kuliko awali. Ingalikuwa afadhali kwao kama wasingalijua kamwe njia hiyo ya uadilifu kuliko kuijua na kisha kuiacha na kupoteza amri takatifu waliyopokea. Ipo methali isemayo: “Mbwa huyarudia matapishi yake mwenyewe,” na nyingine isemayo: “Nguruwe aliyekwisha oshwa hugaagaa tena katika matope!” Ndivyo ilivyo kwao sasa.


Tazama wenye shida/tabu Mungu wetu,wagonjwa,wenye njaa,wanaopitia
magumu/majaribu mbalimbali,walio katika vifungo vya yule mwovu,
waliokataliwa,waliokata tamaa,wenye hofu na mashaka,waliopotea/kuanguka na wote walio katika mapito mbalimbali
Mungu wetu tunaomba ukawaguse kwa mkono wako wenye nguvu,Yahweh tunaomba ukawaponye kiroho na kimwili pia,Baba ukawape neema ya
kujiombea,kufuata njia zako,Yahweh ukawape chakula na ukabariki mashamba yao,Mungu wetu tunaomba ukawarudishe na kuwasimamisha tena,Baba wa Mbinguni wakapate tumaini na Nuru yako ikaangaze
katika maisha yao,Baba wa Mbinguni ukaonekane katika shida zao
Mungu wetu ukawasamehe wale wote waliokwenda kinyume nawe
Baba ukasikie kulia kwao na ukawafute machozi ya watoto wako
wanaokutafuta,kukuomba kwa imani na bidii,Ee Baba tunaomba upokee
sala/maombi yetu na ukawatendee sawasawa na mapenzi yako..
Kwakuwa Ufalme ni wako Nguvu na Utukufu hata Milele....
Amina..!

Asanteni sana wapendwa katika Kristo Yesu kwa kuwa nami..
Mungu aendelee kuwabariki na kuwatendea sawasawa na mapenzi yake
Amani,upendo,furaha na baraka ziwe nanyi...
Nawapenda.

Gideoni

1Waisraeli walitenda uovu mbele ya Mwenyezi-Mungu; naye akawatia mikononi mwa Wamidiani kwa muda wa miaka saba. 2Wamidiani waliwakandamiza sana Waisraeli, mpaka wakajichimbia mashimo na mapango milimani kuwa ngome zao. 3Kila mara Waisraeli walipopanda mbegu mashambani, Wamidiani, Waamaleki na watu wengine wa huko mashariki walikuja kuwashambulia. 4Mataifa hayo yaliweka kambi nchini, yakawashambulia na kuharibu mazao yote nchini hadi mpakani mwa Gaza, wasiwaachie Waisraeli chochote, awe kondoo, ng'ombe au punda. 5Adui waliozoea kuja kwa wingi kama nzige, pamoja na ng'ombe na ngamia wao na kufanya makao yao nchini Israeli, waliharibu nchi ya Israeli kwa vile walikuwa wengi mno wasiohesabika. 6Waisraeli walidhoofishwa sana na Wamidiani hata wakamlilia Mwenyezi-Mungu awasaidie.
7Waisraeli walipomlilia Mwenyezi-Mungu awaondolee taabu walizopata kwa Wamidiani, 8Mwenyezi-Mungu aliwapelekea nabii, naye akawaambia, “Mwenyezi-Mungu, Mungu wa Israeli, asema hivi: ‘Niliwatoa nchini Misri ambako mlikuwa watumwa, 9nikawakomboa mikononi mwa Wamisri wote waliowakandamiza. Nikawafukuza watu mbele yenu na kuwapa nyinyi nchi yao. 10Kisha nikawakumbusheni kuwa mimi ndimi Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu; na kwamba msiiheshimu miungu ya Waamori, ambao nchi yao mmeichukua, lakini hamkuisikiliza sauti yangu.’”

Mungu anamwamuru Gideoni awaokoe Waisraeli

11Malaika wa Mwenyezi-Mungu akaenda, akaketi chini ya mwaloni wa Yoashi, Mwabiezeri, huko Ofra. Gideoni mwana wa Yoashi, alikuwa anapura ngano ndani ya shinikizo la kusindikia zabibu ili Wamidiani wasimwone. 12Malaika wa Mwenyezi-Mungu akamtokea, akamwambia, “Mwenyezi-Mungu yuko pamoja nawe, ewe shujaa.”
13Gideoni akamwambia, “Ee Bwana wangu, ikiwa Mwenyezi-Mungu yuko pamoja nasi, mbona mambo haya yote yametupata? Yako wapi matendo yake ya ajabu ambayo wazee wetu walitusimulia, wakisema: ‘Mwenyezi-Mungu ndiye aliyetutoa nchini Misri.’ Lakini sasa Mwenyezi-Mungu ametutupa na kututia mikononi mwa Wamidiani!”
14Mwenyezi-Mungu akamgeukia, akamwambia, “Nenda kwa uwezo ulio nao, ukaikomboe Israeli kutoka Wamidiani. Ni mimi ninayekutuma.”
15Gideoni akamjibu, “Tafadhali Bwana, nitawezaje kuikomboa Israeli? Ukoo wangu ndio dhaifu zaidi katika kabila la Manase, na mimi mwenyewe ni mdogo kabisa katika jamaa yetu!”
16Mwenyezi-Mungu akamwambia, “Nitakuwa pamoja nawe; nawe utawaangamiza Wamidiani kana kwamba wangekuwa mtu mmoja.”
17Gideoni akamwambia, “Basi, ikiwa nimepata fadhili kwako, nioneshe ishara ili nijue kuwa ni wewe kweli uliyezungumza nami. 18Nakuomba usiondoke hapa mpaka nitakaporudi na kukuletea zawadi yangu na kuiweka mbele yako.”
Naye akamjibu, “Nitakaa hapa mpaka utakaporudi.” 19Gideoni akaenda nyumbani mwake, akatayarisha mwanambuzi na mikate isiyotiwa chachu kutoka debe la unga; akatia nyama ndani ya kikapu na mchuzi ndani ya chungu, kisha akampelekea chini ya mwaloni, akampa. 20Malaika wa Mungu akamwambia, “Chukua nyama na mikate isiyotiwa chachu uviweke juu ya mwamba huu. Halafu tia mchuzi juu ya mikate na nyama.” Naye akafanya hivyo. 21Malaika wa Mwenyezi-Mungu akanyosha fimbo yake, akagusa nyama na mikate kwa ncha ya fimbo. Ghafla, moto ukatoka mwambani, ukateketeza nyama na mikate. Mara malaika wa Mwenyezi-Mungu akatoweka mbele yake.
22Ndipo Gideoni akatambua kwamba huyo alikuwa malaika wa Mwenyezi-Mungu; akasema, “Ole wangu, ee Bwana Mwenyezi-Mungu, maana nimemwona malaika wako uso kwa uso.”
23Lakini Mwenyezi-Mungu akamwambia, “Amani iwe nawe! Usiogope, hutakufa.” 24Gideoni akamjengea Mwenyezi-Mungu madhabahu huko na kuyaita, “Mwenyezi-Mungu ni Amani.” Madhabahu hiyo iko huko Ofra, mji wa Wabiezeri, mpaka leo.

Gideoni anaibomoa madhabahu ya Baali

25Usiku huo, Mwenyezi-Mungu akamwambia Gideoni, “Chukua fahali mmoja wa baba yako, fahali yule wa pili wa umri wa miaka saba. Bomoa madhabahu ya Baali aliyo nayo baba yako na kuvunja sanamu ya Ashera iliyo karibu nayo. 26Halafu, unijengee mimi Mwenyezi-Mungu, Mungu wako, madhabahu nzuri juu ya mwinuko huu. Kisha unitolee sadaka ya kuteketezwa ya yule fahali wa pili ukitumia kuni za ile sanamu ya Ashera uliyoivunja.” 27Basi, Gideoni akachukua watumishi wake kumi, akafanya kama alivyoagizwa na Mwenyezi-Mungu. Lakini kwa kuwa aliiogopa jamaa yake na watu wa mjini, badala ya kufanya hayo mchana, alifanya wakati wa usiku.
28Wakazi wa mji walipoamka asubuhi na mapema waliona madhabahu ya Baali na sanamu ya Ashera iliyokuwa karibu nayo vimeharibiwa. Yule fahali wa pili alikuwa ameteketezwa juu ya madhabahu iliyokuwa imejengwa mahali hapo. 29Wakaulizana, “Nani amefanya jambo hili?” Walipofanya uchunguzi wakagundua kwamba Gideoni mwana wa Yoashi ndiye aliyekuwa amefanya hayo. 30Wakazi wa mji wakamjia Yoashi, wakamwambia, “Mtoe mwanao tumuue, maana ameharibu madhabahu ya Baali na kuivunja sanamu ya Ashera iliyokuwa karibu nayo.”
31Yoashi akawaambia wale wote waliomkabili, “Je, mnamtetea Baali? Je, mtamwokoa? Yeyote atakayemtetea atauawa kabla ya mapambazuko. Kama Baali ni mungu, basi, na ajitetee mwenyewe maana madhabahu yake imebomolewa.” 32Siku hiyo wakamwita Gideoni “Yerubaali” maana yake, “Baali na ajitetee mbele yake”, maana aliibomoa madhabahu ya Baali.
33Wamidiani, Waamaleki na watu wote wanaokaa kando ya mto Yordani wakapiga kambi zao katika bonde la Yezreeli. 34Lakini roho ya Mwenyezi-Mungu ikamjia Gideoni. Gideoni akapiga tarumbeta kuwaita Wabiezeri waje kumfuata. 35Akatuma wajumbe katika nchi yote ya Manase waje kumfuata. Wajumbe wengine akawatuma kuwaita watu wa makabila ya Asheri, Zebuluni na Naftali, nao wakaja kujiunga naye.
36Gideoni akamwambia Mungu, “Ikiwa utaikomboa Israeli kwa mkono wangu kama ulivyosema, 37sasa naweka ngozi ya kondoo kwenye sakafu ya kupuria ngano. Ikiwa kutakuwa na umande juu ya ngozi tu, na sakafu inayoizunguka ikawa kavu, basi, nitajua kuwa utawaokoa Waisraeli kwa mkono wangu kama ulivyosema.” 38Ikawa hivyo, kwa maana alipoamka asubuhi kesho yake, alikamua umande uliokuwa juu ya ile ngozi, akajaza bakuli. 39Gideoni akamwambia Mungu, “Tafadhali usinikasirikie. Nakuomba niseme mara moja tena. Nakuomba uniruhusu nitumie ngozi hii kufanya jaribio lingine. Nakuomba juu ya ngozi kuwe kukavu, lakini kwenye sakafu kuwe na umande.” 40Mungu akafanya hivyo usiku huo, maana, juu ya ngozi kulikuwa kukavu na kwenye sakafu kulikuwa na umande.


Waamuzi 6;1-40

Biblia Habari Njema kwa Watu Wote(BHN)

"Swahili Na Waswahili"Mbarikiwe.

No comments: