Swahili na Waswahili

Swahili na Waswahili
Waswahili na Mswahili Rachel Siwa...Pamoja Daima!!

Friday 18 August 2017

Kikombe Cha Asubuhi;kitabu cha Hesabu..34



Shalom,Habari za Asubuhi,Hamjambo,Mmeamkaje?

Tumshukuru Mungu wetu katika yote..
Asante Mungu wetu Baba yetu,Muumba wetu na Mlinzi wetu,
Baba wa upendo,Baba wa rehema,Kimbilio letu,
Mungu wa Abrahamu,Isaka na Yakobo..
Baba wa Yatima,Mume wa Wajane,Muumba wa Mbingu na Nchi..
Utukuzwe Baba wa Mbinguni,Unastahili sifa Mungu wetu..
Uhimidiwe Mungu wetu,Unatosha Mfalme wa Amani..
Matendo yako ni makuu mno,Matendo yako ni ya Ajabu..!
Hakuna kama wewe Mungu wetu..
Sifa na Utukufu ni wako..
Nakupenda, ee Mwenyezi-Mungu, nguvu yangu! Mwenyezi-Mungu ni mwamba wangu, ngome yangu na mkombozi wangu; Mungu wangu, mwamba wangu ninayemkimbilia usalama; ngao yangu, nguvu za wokovu wangu na ngome yangu.
Asante Baba wa Mbinguni kwa wema na fadhili zako kwetu..
Asante kwakutuchagua tena na kutupa kibali cha kuendelea kuiona leo hii..
Tazama jana imepita Baba wa Mbinguni Leo ni siku mpya na kesho ni siku nyingine Mfalme wa Amani..
Tunakuja mbele zako tukijinyenyekeza,tukijishusha na kujiachilia mikononi mwako Muumba wetu..
Tunaomba utusamehe dhambi zetu zote tulizo zifanya kwakuwaza,kwakunena,kwakutenda,kwakujua/kutojua..
Baba wa upendo tunaomba nasi ukatupe neema ya kuweza kuwasamehe wale waliotukosea..
Utuepushe katika majaribu Mungu wetu utuokoe na yule mwovu na kazi zake zote..
Ututakase Miili yetu na Akili zetu na utufunike kwa Damu ya Bwana wetu Yesu Kristo wa Nazareti..
Roho Mtakatifu akatuongoze katika yote ..
Tukapate kupendana kama Bwana alivyotupenda sisi..
Tukawe na upendo wa kweli na kuheshimiana,kuhurumiana,kusaidiana..
Tukaonyane kwa upendo na hekima..
Busara ikatawale na tukanene yaliyo yako Mungu wetu..

Mimi ni mzabibu wa kweli, na Baba yangu ndiye mkulima. Kila tawi ndani yangu lisilozaa matunda yeye huliondoa, na kila tawi lizaalo hulisafisha lipate kuzaa zaidi. Nyinyi mmekwisha kuwa safi kwa sababu ya ule ujumbe niliowaambieni. Kaeni ndani yangu, nami nikae ndani yenu. Kama vile tawi haliwezi peke yake kuzaa matunda lisipobaki katika mzabibu, hali kadhalika nanyi hamwezi kuzaa matunda msipokaa ndani yangu. “Mimi ni mzabibu, nanyi ni matawi. Akaaye ndani yangu, nami nikiwa ndani yake, huyo huzaa matunda mengi, maana bila mimi hamwezi kufanya chochote. Mtu yeyote asipokaa ndani yangu hutupwa nje kama tawi litupwalo nje hata likakauka. Watu huliokota tawi la namna hiyo na kulitupa motoni liungue. Mkikaa ndani yangu na maneno yangu yakikaa ndani yenu, basi, ombeni chochote mtakacho nanyi mtapewa. Baba yangu hutukuzwa kama mkizaa matunda mengi na kuwa wanafunzi wangu. Mimi nimewapenda nyinyi kama vile Baba alivyonipenda mimi. Kaeni katika pendo langu. Mkizishika amri zangu mtakaa katika pendo langu, kama vile nami nilivyozishika amri za Baba yangu na kukaa katika pendo lake. Nimewaambieni mambo haya ili furaha yangu ikae ndani yenu, na furaha yenu ikamilike. Hii ndiyo amri yangu: Pendaneni; pendaneni kama nilivyowapenda nyinyi. Hakuna upendo mkuu zaidi kuliko upendo wa mtu atoaye uhai wake kwa ajili ya rafiki zake. Nyinyi ni rafiki zangu mkifanya ninayowaamuru. Nyinyi siwaiti tena watumishi, maana mtumishi hajui anachofanya bwana wake. Lakini mimi nimewaita nyinyi rafiki, kwa sababu nimewajulisha yote ambayo nimeyasikia kutoka kwa Baba yangu. Nyinyi hamkunichagua mimi; mimi niliwachagueni na kuwatuma mwende mkazae matunda, matunda yadumuyo, naye Baba apate kuwapeni chochote mnachomwomba kwa jina langu. Basi, amri yangu kwenu ndiyo hii: Pendaneni.

Tukasimamie Neno lako,Amri na Sheria yako Mungu wetu..
Ukatuepushe na chuki,kiburi,majivuno na kufuata mambo yetu wenyewe ...
Ukatuepushe na mambo yote mabaya ya Dunia hii yaliyo kinyume nawe Mungu wetu..
Ukatupe macho ya kuona na masikio ya kusikia..
tukapate kutambua/kujitambu na tukawe na kiasi..

“Kama ulimwengu ukiwachukia nyinyi, kumbukeni kwamba umenichukia mimi kabla ya kuwachukia nyinyi. Kama mngalikuwa watu wa ulimwengu, ulimwengu ungaliwapenda nyinyi kama watu wake. Lakini kwa vile nyinyi si wa ulimwengu, ila mimi nimewachagueni kutoka ulimwenguni, kwa sababu hiyo ulimwengu unawachukieni. Kumbukeni niliyowaambieni: Mtumishi si mkuu kuliko bwana wake. Ikiwa wamenitesa mimi, watawatesa na nyinyi pia; kama wameshika neno langu, watalishika na lenu pia. Lakini hayo yote watawatendeeni nyinyi kwa sababu ya jina langu, kwani hawamjui yeye aliyenituma. Kama nisingalikuja na kusema nao wasingalikuwa na hatia; lakini sasa hawawezi kujitetea kwamba hawana dhambi. Anayenichukia mimi, anamchukia na Baba yangu pia. Kama nisingalifanya kwao mambo ambayo hakuna mtu mwingine amekwisha yafanya wasingalikuwa na hatia; lakini sasa wameona niliyoyafanya wakanichukia mimi, wakamchukia na Baba yangu pia. Ndiyo maana yale yaliyoandikwa katika sheria yao ni kweli: ‘Wamenichukia bure!’ “Atakapokuja huyo Msaidizi nitakayemtuma kwenu kutoka kwa Baba, huyo Roho wa ukweli, atokaye kwa Baba, yeye atanishuhudia mimi. Nanyi pia mtanishuhudia kwa kuwa mmekuwa nami tangu mwanzo.
Yahweh tunaomba ukatubariki na ukabariki ridhiki zetu ziingiazo/zitikazo..
Mungu wetu nasi ukatupe neema ya kuweza kuwabariki wenye kuhitaji..
Tusipungukiwe katika mahitaji yetu Jehovah ukatupe sawasawa na mapenzi yako..
Ukabariki kazi za mikono yetu na vyote tunavyoenda kufanya/kutenda tukatende kama inavyokupendeza wewe..
Ukatufanye chombo chema nasi tukatumike kama inavyokupendeza wewe..

Asante Baba wa Mbinguni..
Tuyaweka haya yote mikononi mwako..
Tuliyoyanena na tusiyoyanena Mungu Baba unayajua na kutujua sisi zaidi ya tujijuavyo..

Kwakuwa Ufalme ni wako Nguvu na Utukufu hata Milele..
Amina..!

Asanteni sana wapendwa kwa muda wenu na kunisoma..
Mungu wa Baraka aendelee kuwabariki na kuwatendea..
Nawapenda..



Mipaka ya nchi

1Mwenyezi-Mungu akamwambia Mose, 2“Waamuru Waisraeli ukisema: Mtakapoingia Kanaani, nchi ambayo ninawapa iwe nchi yenu, mipaka ya eneo lenu lote itakuwa kama ifuatavyo. 3Upande wa kusini mpaka wenu utakuwa kutoka jangwa la Sini kupitia upande wa Edomu. Utaanzia mashariki upande wa kusini mwisho wa Bahari ya Chumvi. 4Kisha utapinda kusini kuelekea pito la Akrabimu na kupitia Sini hadi Kadesh-barnea, upande wa kusini. Kutoka hapo, mpaka utapinda kuelekea kaskazini-magharibi hadi Hasar-adari na kupita hadi Azmoni. 5Kutoka Azmoni utapinda kuelekea kijito cha Misri kwenye mpaka wa Misri na kuishia bahari ya Mediteranea.
6“Mpaka wenu wa upande wa magharibi utakuwa bahari ya Mediteranea.
7“Mpaka wenu wa upande wa kaskazini utakuwa kama ifuatavyo: Kutoka bahari ya Mediteranea, mtatia alama hadi Mlima Hori. 8Kutoka Mlima Hori mtatia alama hadi pito la Hamathi, na kuendelea hadi Sedadi, 9na kupita hadi Zifroni na kuishia Hazar-enani; huo utakuwa mpaka wenu wa kaskazini.
10“Mpaka wenu wa upande wa mashariki mtauweka kutoka Hazar-enani hadi Shefamu. 11Kutoka Shefamu utaelekea kusini hadi Ribla, mashariki mwa Aini; kisha mpaka huo utakwenda chini hadi mteremko wa mashariki wa ziwa Kinerethi,34:11 Kinerethi: Ziwa Galilaya. 12halafu utateremka kufuata mto Yordani hadi Bahari ya Chumvi; hii ndiyo itakuwa nchi yako kama mpaka ulivyo.”
13 Taz Yosh 14:1-5 Basi, Mose akawaambia Waisraeli, “Hii ndiyo nchi mtakayoirithi kwa kupiga kura, nchi ambayo Mwenyezi-Mungu ameagiza yapewe makabila tisa na nusu. 14Kabila la Reubeni na la Gadi, na nusu ya kabila la Manase yamepata urithi wao kulingana na koo zao. 15Makabila hayo mawili na nusu yamepata urithi wao ngambo ya mto Yordani upande wa mashariki, mkabala wa Yeriko, mawioni.”

Viongozi watakaosimamia mgawanyo wa nchi

16Mwenyezi-Mungu akamwambia Mose, 17“Kuhani Eleazari na Yoshua mwana wa Nuni ndio watakaowagawia watu nchi kuwa mali yao. 18Utachukua pia kiongozi mmoja kutoka kila kabila kusaidia katika ugawaji wa nchi. 19Haya ndiyo majina yao:
Kabila la Yuda, Kalebu mwana wa Yefune.
20Kabila la Simeoni, Shemueli mwana wa Amihudi.
21Kabila la Benyamini, Elidadi mwana wa Kisloni.
22Kabila la Dani, Buki mwana wa Yogli.
23Kabila la Manase mwanawe Yosefu, Hanieli mwana wa Efodi.
24Kabila la Efraimu, mwanawe Yosefu, Kemueli mwana wa Shiftani.
25Kabila la Zebuluni, Elisafani mwana wa Parnaki.
26Kabila la Isakari, Paltieli mwana wa Azani.
27Kabila la Asheri, Ahihudi mwana wa Shelomi
28Kabila la Naftali, Pedaheli mwana wa Amihudi.
29Hawa ndio watu ambao Mwenyezi-Mungu aliwaamuru wawagawie Waisraeli nchi ya Kanaani kuwa mali yao.”



Hesabu34;1-29



Biblia Habari Njema kwa Watu Wote(BHN)

"Swahili Na Waswahili"Mbarikiwe.

No comments: