Swahili na Waswahili

Swahili na Waswahili
Waswahili na Mswahili Rachel Siwa...Pamoja Daima!!

Tuesday 15 August 2017

Kikombe Cha Asubuhi;kitabu cha Hesabu..31




Shalom,Habari za Asubuhi,Hamjambo,Mmeamkaje?

Tumshukuru Mungu wetu kwa wema na fadhili zake kwetu..
Asante Mungu wetu,Baba yetu na mlinzi wetu..
Mungu wa Abrahamu,Isaka na Yakobo..
Muweza wa yote,Mfalme wa Amani..
Utukuzwe Baba wa Mbinguni,Uhimidiwe Mungu wetu..
Unastahili sifa Baba..Uabudiwe daima Mungu wetu..
Hakuna kama wewe,wewe ni Alfa na Omega..!!
Asante Mungu wetu kwa ulinzi wako wakati wote..
Asante kwakutuchagua tena na kutupa kibali cha kuendelea kuiona leo hii

Tazama jana imepita Mungu wetu Leo ni siku mpya Jehovah na kesho ni siku nyingine Yahweh..!
Tunashuka mbele zako Mungu wetu tunaomba utusamehe dhambi zetu tulizozifanya kwakuwaza,kwakunena,kwakutenda,kwakujua/kutojua..
Mfalme wa Amani tunaomba nasi utupe neema ya kuweza kuwasamehe wale wote waliotukosea..
Mungu wetu tunaomba utuepushe katika majaribu
 Baba wa mbinguni utuokoe na yule mwovu na kazi zake zote..
Yahweh maisha yetu yapo mikononi mwako..
Tunaomba utubariki na ukabariki kazi za mikono yetu na vyote tunavyoenda kufanya/kutenda tukatende sawasawa na mapenzi yako..
Ukabariki ridhiki zetu ziingiazo/zitokazo Mungu wetu nasi ukatupe neema ya kuweza kuwabariki wenye kuhitaji..
Tusipungukiwe katika mahitaji yetu Baba wa rehema ukatupe kama inavyokupendeza wewe..
Mungu wetu ukaonekane  popote tupitapo,tunenapo tukanene yaliyoyako..
ukatupe macho ya kuona na masikio ya kusikia sauti yako..
Ukatupe neema ya Hekima,Busara,Upendo,unyenyekevu na kuchukuliana..
Utuepushe na  Hasira,majivuno/kujisifu na kufuata mambo yetu yanayokwenda kinyume nawe..
Roho Mtakatifu akatuongoze katika yote na tukawe na kiasi..
Ukatufanye chombo chema Mungu wetu nasi tukatumike ipasavyo..

Tazama wenye shida/tabu,wote wanaopitia magumu/majaribu,walio katika vifungo mbalimbali Mungu Baba tunaomba ukawaguse na mkono wako wenye nguvu,wakapate uponyaji wa mwili na roho..
ukawape neema ya kusimamia Neno,Amri na sheria zako nazo zikawaweka huru ..

Baba wa Mbinguni tunawaweka viongozi wetu wote wa Kiroho mikononi mwako..
Mungu wetu ukawatendee na kuwaongoza katika huduma zao..
Ukawainua na pale walipojikwaa wakatambue na kukurudia Mungu,wakafuate matakwa yako Mungu wetu na si yao wenyewe,wakatuongoze katika roho na kweli,ukawaepushe katika roho za Tamaa,Majivuno,Dharau,masimango,masengenyo,ugombanishi na yote yanayokwenda kinyume nawe,wakatende sawasawa na mapenzi yako..
Nasi washarika/waumini ukatupe neema ya kutii na kuchukuliana,kupendana,kushirikiana,kuonyana kwa wema na upendo
tusimpe adui nafasi na kazi ya Mungu iende kama inavyopaswa kuenda..
 injili iende mbele na Neno lita simama..

Watumwa wote wanapaswa kuwaheshimu wakuu wao ili kusiwe na sababu ya watu kulitukana jina la Mungu na mafundisho yetu. Watumwa ambao wakuu wao ni Wakristo wasiwadharau kwani ni ndugu zao. Badala yake, wanapaswa kuwatumikia hata vizuri zaidi, maana hao wanaopata faida kutokana na kazi yao ni waumini ambao wanawapenda. Unapaswa kufundisha na kuhubiri mambo haya. Mtu yeyote anayefundisha kinyume cha mambo haya, na ambaye hakubaliani na maneno ya kweli ya Bwana wetu Yesu Kristo na mafundisho ya uchaji wa Mungu, huyo amejaa majivuno na wala hajui chochote. Ni mtu wa kupenda ubishi na magombano juu ya maneno matupu, na hiyo husababisha wivu, ugomvi, matusi, shuku mbaya, na ubishi usio na kikomo kutoka kwa watu ambao akili zao zimeharibika, na ambao hawana tena ukweli. Wanadhani dini ni njia ya kujipatia utajiri. Kweli kumcha Mungu humfanya mtu awe tajiri sana, ikiwa anatosheka na vitu alivyo navyo. Maana hatukuleta kitu chochote hapa duniani, wala hatutachukua chochote. Kwa hiyo basi, kama tunacho chakula na mavazi, tunapaswa kuridhika navyo. Lakini wale wanaotaka kutajirika huanguka katika majaribu, na kunaswa katika mtego wa tamaa nyingi mbaya za kipumbavu, ambazo huwavuta mpaka kwenye uharibifu na maangamizi. Kwa maana kupenda sana fedha ni chanzo cha uovu wote. Watu wengine wametamani sana kupata fedha hata wakatangatanga mbali na imani, na wameivunja mioyo yao kwa huzuni nyingi. Lakini wewe, mtu wa Mungu, jiepushe na mambo hayo. Zingatia uadilifu, uchaji wa Mungu, imani, upendo, subira na unyenyekevu. Piga mbio kadiri uwezavyo katika shindano la mbio za imani, ukajipatie tuzo la uhai wa milele uliloitiwa wakati ulipokiri imani yako mbele ya mashahidi wengi. Mbele ya Mungu anayevipa vitu vyote uhai, na mbele ya Yesu Kristo aliyetoa ushahidi na kukiri ukweli mbele ya Pontio Pilato, nakuamuru ushike maagizo yako na kuyatii kwa uaminifu mpaka siku ile atakapotokea Bwana wetu Yesu Kristo. Kutokea kwake kutafanyika wakati ufaao uliopangwa na Mungu mwenye heri na aliye Mtawala pekee, Mfalme wa wafalme, na Bwana wa mabwana. Yeye peke yake anaishi milele katika mwanga usioweza kukaribiwa na mtu. Hakuna mtu aliyepata kumwona au awezaye kumwona. Kwake iwe heshima na uwezo wa milele! Amina. Waamuru watu walio matajiri katika mambo ya maisha ya sasa, wasijivune, wasiweke tumaini lao katika mali isiyoweza kutegemewa; bali wamtegemee Mungu, ambaye kwa ukarimu hutupatia vitu vyote tuvifurahie. Waamuru watende mema, wawe matajiri katika matendo mema, na wawe wakarimu na walio tayari kuwashirikisha wengine mali zao. Kwa namna hiyo watajiwekea hazina ambayo itakuwa kwao msingi imara kwa wakati ujao. Hapo wataweza kujipatia uhai ambao ni uhai wa kweli. Timotheo, tunza salama yote yale uliyokabidhiwa. Jiepushe na majadiliano ya kidunia na ubishi wa kipumbavu juu ya kile wanachokiita watu wengine “Elimu.” Maana wengine wamejidai kuwa na hiyo elimu, na matokeo yake wamepoteza imani. Nawatakieni nyote neema!


Asante Mungu wetu katika yote..
tunayaweka haya mikononi mwako,tukiamini na kushukuru daima..
wewe ni Mungu wetu na kimbilio letu..
Sifa na utukufu tunakurudishia wewe...
Kwakuwa Ufalme ni wako Nguvu na Utukufu hata Milele..
Amina...!
Asanteni sana wapendwa/waungwana kwakuwa nami..
Mungu Baba aendelee kuwabariki na kuwatendea katika yote..
msipungukiwe katika mahitaji yenu,Mungu akawape kama itakavyompendeza yeye..
Nawapenda.


Vita vitakatifu dhidi ya Midiani


1Mwenyezi-Mungu aliongea na Mose, akamwambia, 2“Walipize kisasi Wamidiani mambo waliyowatenda Waisraeli; kisha wewe utafariki.”
3Basi Mose akazungumza na watu akawaambia, “Watayarisheni watu kwa vita waende kuwashambulia Wamidiani kumlipizia Mwenyezi-Mungu kisasi. 4Kutoka kila kabila la Israeli, mtapeleka watu 1.000 vitani.”
5Basi, watu 1,000 walitolewa kutoka kila kabila miongoni mwa maelfu ya Waisraeli, jumla wanaume 12,000 wenye silaha. 6Mose aliwapeleka vitani chini ya uongozi wa Finehasi mwana wa kuhani Eleazari, akiwa na vyombo vya mahali patakatifu na tarumbeta za kutoa ishara. 7Waliishambulia nchi ya Midiani, kama Mwenyezi-Mungu alivyomwamuru Mose, wakawaua wanaume wote. 8Miongoni mwa watu hao waliouawa, kulikuwako wafalme watano wa Midiani: Evi, Rekemu, Suri, Huri na Reba. Vilevile walimuua Balaamu mwana wa Beori.
9Waisraeli waliteka nyara: Ng'ombe, kondoo na mali yao yote. 10Miji yao yote, makazi yao na kambi zao zote waliziteketeza kwa moto. 11Walichukua nyara zote na mateka yote, ya watu na ya wanyama, 12wakampelekea Mose na Eleazari, na jumuiya yote ya Waisraeli iliyokuwa kambini katika nchi tambarare za Moabu, ngambo ya Yordani karibu na Yeriko.

Kurudi vitani

13Mose, kuhani Eleazari, na viongozi wote wa jumuiya ya Waisraeli walitoka kambini, wakaenda kuwalaki wanajeshi. 14Mose alikasirishwa na maofisa wa jeshi na makamanda waliosimamia makundi ya majeshi 1,000 na makundi ya wanajeshi mamia waliorudi kutoka vitani. 15Mose akawauliza, “Kwa nini mmewaacha wanawake hawa wote hai? 16Taz Hes 25:1-9 Kumbukeni kwamba wanawake ndio waliofuata shauri la Balaamu, wakasababisha Waisraeli wamwasi Mwenyezi-Mungu kule Peori hata maradhi mabaya yakawajia watu wake Mwenyezi-Mungu. 17Kwa hiyo basi, waueni watoto wote wa kiume na kila mwanamke aliyewahi kulala na mwanamume. 18Lakini msiwaue wasichana wote ambao hawajapata kulala na mwanamume; waacheni hai kwa ajili yenu wenyewe. 19Wote wale walio miongoni mwenu ambao wameua mtu au kugusa maiti ni lazima wakae nje ya kambi kwa muda wa siku saba; jitakaseni pamoja na mateka wenu katika siku ya tatu na ya saba. 20Ni lazima mtakase pia kila vazi, kila kitu kilichotengenezwa kwa ngozi, kwa manyoya ya kondoo au kwa mti.”
21Kuhani Eleazari akawaambia wanaume waliorudi vitani, “Hii ndiyo sheria ambayo Mwenyezi-Mungu amempa Mose. 22Dhahabu, fedha, shaba, chuma, bati na madini ya risasi, 23yaani vitu vyote ambavyo vinastahimili moto, vitatakaswa kwa kupitishwa motoni. Hata hivyo, ni lazima vitakaswe kwa maji ya utakaso. Vitu vingine vyote ambavyo haviwezi kustahimili moto vitatakaswa kwa maji ya utakaso. 24Siku ya saba ni lazima muyafue mavazi yenu; ndipo mtakapokuwa safi na kuruhusiwa kuingia kambini.”

Kugawa nyara na mateka

25Mwenyezi-Mungu akaongea na Mose, akamwambia, 26“Wewe na kuhani Eleazari, pamoja na viongozi wa koo za jumuiya ya Waisraeli, fanyeni hesabu ya nyara ya vitu, watu na wanyama. 27Gaweni nyara katika mafungu mawili, fungu moja la wanajeshi waliokwenda vitani na fungu lingine kwa ajili ya jumuiya nzima. 28Kisha kutokana na lile fungu la wanajeshi waliokwenda vitani, tenga zaka kwa ajili ya Mwenyezi-Mungu: Kitu kimoja kutoka kila vitu 500, iwe ni watu, ng'ombe, punda, kondoo au mbuzi, 29umpe kuhani Eleazari kuwa sadaka kwa Mwenyezi-Mungu. 30Kutoka lile fungu la jumuiya nzima, chukua sehemu moja ya kila hamsini, iwe ni watu, ng'ombe, punda, kondoo na mbuzi. Hivyo utawapa Walawi ambao wana wajibu wa kuhudumu katika hema la Mwenyezi-Mungu.” 31Mose na kuhani Eleazari walifanya kama Mwenyezi-Mungu alivyomwamuru Mose.
32Nyara walizoteka wanajeshi zilikuwa: Kondoo 675,000, 33ng'ombe 72,000, 34punda 61,000, 35na wasichana ambao hawakuwa wamelala na mwanamume 32,000. 36Nusu yake, sehemu ambayo iligawiwa wanajeshi waliokwenda vitani, ilikuwa kondoo 337,500, 37katika hao 675 walitolewa kwa Mwenyezi-Mungu. 38Ngombe wa wanajeshi walikuwa 36,000, na katika hao 72 walitolewa zaka kwa Mwenyezi-Mungu. 39Punda wao walikuwa 30,500, na katika hao 61 walitolewa zaka kwa Mwenyezi-Mungu. 40Watu walikuwa 16,000, na katika hao sehemu ya Mwenyezi-Mungu ilikuwa ni watu thelathini na wawili. 41Basi, Mose akampa kuhani Eleazari zaka hiyo iliyotolewa kwa Mwenyezi-Mungu, kama Mwenyezi-Mungu alivyomwamuru Mose.
42Ile nusu waliopewa Waisraeli, ambayo Mose aliitenga na ile nusu waliyopewa wanajeshi waliokwenda vitani, 43ilikuwa kondoo 337,500, 44ng'ombe 36,000, 45punda 30,500, 46na watu 16,000. 47Kutoka nusu hii waliyopewa Waisraeli, Mose alitwaa mmoja kati ya kila mateka hamsini na wanyama hamsini, kama alivyoamriwa na Mwenyezi-Mungu, akawapa Walawi ambao walihudumu katika hema la Mwenyezi-Mungu.
48Kisha maofisa wa majeshi, makapteni na makamanda wa askari wakamwendea Mose, 49wakamwambia “Watumishi wako tumewahesabu askari wote walio chini yetu na tumeona kwamba hakuna hata mmoja wao anayekosekana. 50Basi, tumeleta vyombo vya dhahabu, vikuku, bangili, pete za mhuri, vipuli na shanga ambavyo kila mtu alipata. Tumevitoa ili nafsi zetu zifanyiwe upatanisho mbele ya Mwenyezi-Mungu.” 51Mose na kuhani Eleazari wakapokea vitu vyote vilivyonakshiwa kwa dhahabu. 52Jumla ya dhahabu yote waliyomtolea Mwenyezi-Mungu ilikuwa karibu kilo 200. 53(Kila askari alijichukulia nyara zake binafsi). 54Basi, Mose na kuhani Eleazari wakaipokea dhahabu hiyo kutoka kwa makamanda wakaipeleka katika hema la mkutano, iwe ukumbusho wa Waisraeli mbele ya Mwenyezi-Mungu.



Hesabu31;1-54



Biblia Habari Njema kwa Watu Wote(BHN)

"Swahili Na Waswahili"Mbarikiwe.

No comments: