Swahili na Waswahili

Swahili na Waswahili
Waswahili na Mswahili Rachel Siwa...Pamoja Daima!!

Tuesday 8 August 2017

Kikombe Cha Asubuhi;kitabu cha Hesabu..26



Shalom,Habari za Asubuhi,Hamjambo,Mmeamkaje?

Tumshukuru  Mungu wetu katika yote...
Asante Mungu  wetu Baba yetu,Muumba wa yote..
Mungu wa Abrahamu,Isaka na Yakobo..!
Utukuzwe ee Baba..Uinuliwe Yahweh..Usifiwe Mfalme wa Amani..Uabudiwe daima..!


Uponyaji unapatikana kwako,Upendo wa kweli upo ndani yako,Faraja inapatika nawe,Furaha ipo na wewe,wema na fadhili zipo kwako..

wewe ni Mungu wa Wajane,Wewe ni Baba wa Yatima,,
Wewe ni Alfa na Omega..!Hakuna lililogumu kwako Mungu..!
Sifa na Utukufu ni wako Jehovah...!

Ee Mwenyezi-Mungu, nitaimba fadhili zako milele; nitavitangazia vizazi vyote uaminifu wako. Natamka kuwa fadhili zako zadumu milele; uaminifu wako ni thabiti kama mbingu. Umesema: “Nimefanya agano na mteule wangu, nimemwapia mtumishi wangu Daudi: ‘Daima nitamweka mzawa wako kuwa mfalme, tena nitaudumisha ufalme wako milele.’” Mbingu na zisifu maajabu yako, ee Mwenyezi-Mungu; uaminifu wako usifiwe katika kusanyiko la watakatifu. Nani mbinguni awezaye kulinganishwa nawe ee Mwenyezi-Mungu? Nani aliye sawa nawe kati ya viumbe vya mbinguni? Wewe waogopwa katika baraza la watakatifu; wote wanaokuzunguka wanatiwa hofu kuu. Ee Mwenyezi-Mungu, Mungu wa majeshi, ni nani mwenye nguvu kama wewe, ee Mwenyezi-Mungu? Uaminifu umekuzunguka pande zote. Wewe watawala machafuko ya bahari; mawimbi yake yakiinuka, wayatuliza. Uliliponda joka Rahabu na kuliua; uliwatawanya adui zako kwa nguvu yako. Mbingu ni zako na dunia ni yako pia; ulimwengu na vitu vyote vilivyomo wewe uliviumba. Wewe uliumba kaskazini na kusini; milima Tabori na Hermoni inakusifu kwa furaha. Mkono wako una nguvu, mkono wako una nguvu na umeshinda! Uadilifu na haki ni msingi wa utawala wako; fadhili na uaminifu vyakutangulia! Heri watu wanaojua kukushangilia, wanaoishi katika mwanga wa wema wako, ee Mwenyezi-Mungu. Wanafurahi mchana kutwa kwa sababu yako, na kukusifu kwa ajili ya uadilifu wako. Wewe ndiwe fahari na nguvu yao; kwa wema wako twapata ushindi. Ee Mwenyezi-Mungu, mlinzi wetu ni wako, mfalme wetu ametoka kwako ewe Mtakatifu wa Israeli.

Tunakuja Mbele zako Mungu wetu tukijishusha,tukijinyenyekeza na kujiachilia mikononi mwako Mungu Baba..
Tunaomba utusamehe pale tulipokwenda kinyume nawe Mungu wetu..
kwakuwaza,kwakunena,kwakutenda,kwakujua/kutojua..
Baba wa Mbinguni nasi tunaomba utupe neema yakuweza kuwasamehe wale wote waliotukosea..
Utuepushe katika majaribu Yahweh  utuokoe na yule mwovu na kazi zake zote..


Jehovah tunaomba ukatubariki na ukabariki kazi za mikono yetu na vyote tunavyoenda kufanya/kutenda Mungu Baba tukatende sawasawa na mapenzi yako..
Ukabariki ridhiki zetu ziingiazo na zitokazo Mungu wetu nasi ukatupe neema ya kuweza kuwasaidia wenye kuhitaji..
Tusipungukiwe katika mahitaji yetu Mfalme wa Amani ukatupe kama inavyokupendeza wewe..

Yahweh tazama wenye shida/tabu na wote wanaopitia magumu/majaribu mbalimbali,wagonjwa na waliokata tamaa,wafiwa ukawe mfariji wao..
Jehovah tunaomba ukawaguse na mkono wako wenye nguvu,ukawaponye kimwili na kiroho pia..Ukawape neema ya kusimamia Neno lako nalo litawaweka huru..


Mwenyezi-Mungu, Mkombozi wenu, Mtakatifu wa Israeli, asema hivi: “Kwa ajili yenu nitatuma jeshi Babuloni. Nitayavunjilia mbali malango ya mji wake, na kelele za hao Wakaldayo zitageuka maombolezo. Mimi ni Mwenyezi-Mungu, Mtakatifu wenu; Mimi ndimi Muumba wa Israeli, Mfalme wenu.” Mwenyezi-Mungu asema hivi: “Wakati mmoja nilifanya barabara baharini nikaweka njia kati ya mawimbi makubwa. Nililipiga jeshi lenye nguvu, jeshi la magari na farasi wa vita, askari na mashujaa wa vita. Niliwaangusha chini wasiweze kuinuka tena, niliwakomesha na kuwazima kama utambi wa taa. Sasa nasema: ‘Msiyanganganie mambo yaliyopita, wala msifikirie vitu vya zamani. Tazameni, mimi ninafanya kitu kipya. Kinafanyika sasa hivi, nanyi mtaweza kukiona. Nitafanya njia nyikani, na kububujisha mito jangwani. Wanyama wa porini wataniheshimu, kina mbweha na kina mbuni, maana nitaweka maji nyikani, na kububujisha mito jangwani, ili kuwanywesha watu wangu wateule, watu niliowaumba kwa ajili yangu mwenyewe, ili wazitangaze sifa zangu!’

Roho Mtakatifu akatuongoze katika yote na tukawe na kiasi..
Ukatufanye chombo chema Mungu Baba popote tulipo tukatumike sawasawa na mapenzi yako..

Asante Mungu wetu..tunayaweka haya yote mikononi mwako..
Sifa na utukufu tunakurudishia wewe  Baba wa Yote..
Kwakuwa Ufalme ni wako Nguvu na Utukufu hata Milele..
Amina..!

Asanteni sana wapendwa katika yote..
Mungu aendelee kuonekana katika maisha yenu..
Msipungukiwe katikamahitaji  yenu Baba wa Mbinguni akawape kama itakavyompendeza yeye..

Nawapenda.


Sensa ya Pili

1 Taz Hes 1:1-46 Baada ya yale maradhi, Mwenyezi-Mungu akamwambia Mose na Eleazari mwana wa kuhani Aroni, 2“Hesabuni jumuiya yote ya Waisraeli, kila mtu kufuatana na jamaa yake. Wahesabuni watu wote wenye umri wa miaka ishirini na zaidi wanaofaa kwenda jeshini.” 3Mose na kuhani Eleazari wakazungumza na watu kwenye nchi tambarare za Moabu, ngambo ya mto Yordani, karibu na Yeriko, wakawaambia, 4“Hesabuni watu kuanzia na wenye umri wa miaka ishirini na zaidi, kama Mwenyezi-Mungu alivyomwamuru Mose.” Idadi ya Waisraeli waliotoka Misri ni hii:
5Kwanza ni kabila la Reubeni, mzaliwa wa kwanza wa Yakobo. Henoki, Palu, 6Hesroni na Karmi. 7Hizo ndizo koo za kabila la Reubeni. Idadi ya wanaume waliohesabiwa ni 43,730. 8Wazawa wa Palu walikuwa Eliabu, 9na wanawe Nemueli, Dathani na Abiramu. (Hawa wawili: Dathani na Abiramu, ndio waliokuwa wamechaguliwa miongoni mwa jumuiya, lakini wakampinga Mose na Aroni, na kujiunga na wafuasi wa Kora wakati walipomwasi Mwenyezi-Mungu. 10Wakati huo ardhi ilifunguka ikawameza, wakafa pamoja na Kora na wafuasi wake moto ulipoangamiza watu 250; wakawa onyo kwa watu. 11Pamoja na hayo wana wa Kora hawakufa.)
12Kabila la Simeoni. Nemueli, Yamini, Yakini, 13Zera na Shauli. 14Hizo ndizo koo za kabila la Simeoni, jumla yao wanaume 22,000.
15Kabila la Gadi lilikuwa na jamaa za Sefoni, Hagi, Shuni, 16Ozni, Eri, 17Arodi na Areli. 18Hizo ndizo koo za kabila la Gadi, jumla wanaume 40,500.
19Kabila la Yuda lilikuwa na wanawe wa Yuda Eri na Onani. Hawa walifia nchini Kanaani. 20Kabila la Yuda lilikuwa na jamaa za Shela, Peresi, na Zera. 21Kutoka kwa Peresi, familia ya Hesroni na Hamuli. 22Hizo ndizo koo za Yuda, jumla wanaume 76,500.
23Kabila la Isakari lilikuwa na jamaa za Tola, Puva, 24Yashubu na wa Shimroni. 25Hizo ndizo koo za Isakari, jumla wanaume 64,300.
26Kabila la Zebuluni lilikuwa na jamaa za Seredi, wa Eloni na wa Yaleeli. 27Hizo ndizo koo za Zebuluni, jumla wanaume 60,500.
28Kabila la Yosefu baba yao Manase na Efraimu.
29Kabila la Manase lilikuwa na jamaa ya: Makiri, Gileadi. 30Yezeri, Heleki, 31Asrieli, Shekemu, 32Shemida na Heferi. 33Selofehadi, mwana wa Heferi hakupata watoto wa kiume bali wa kike tu, nao ni Mala, Noa, Hogla, Milka na Tirza. 34Hizo ndizo koo za Manase, jumla wanaume 52,700.
35Kabila la Efraimu lilikuwa na jamaa za Shuthela, Bekeri na Tahani. 36Ukoo wa Erani ulikuwa na jamaa ya Shuthela. 37Hizo ndizo koo za Efraimu, jumla wanaume 32,500. Zote hizo zilitokana na Yosefu.
38Kabila la Benyamini lilikuwa na jamaa za Bela, Ashbeli, Ahiramu, 39Shufamu na Hufamu. 40Koo za Ardi na Naamani, zilitokana na Bela. 41Hizo ndizo koo za Benyamini, jumla wanaume 45,600.
42Kabila la Dani lilikuwa na jamaa ya Shuhamu; 43ukoo ulikuwa na wanaume 64,400.
44Kabila la Asheri lilikuwa na jamaa za Imna, Ishvi na Beria. 45Koo za Heberi na Malkieli zilitokana na Beria. 46Asheri alikuwa na binti aliyeitwa Sera. 47Hizo ndizo koo za kabila la Asheri, jumla wanaume 53,400.
48Kabila la Naftali lilikuwa na jamaa za Yaseeli, Guni, 49Yeseri na Shilemu. 50Hizi ndizo koo za kabila la Naftali, jumla wanaume 45,400.
51Idadi ya wanaume Waisraeli waliohesabiwa ilikuwa 601,730.
52 Taz Hes 34:13; Yosh 14:1-2 Kisha Mwenyezi-Mungu alimwambia Mose, 53“Makabila haya yatagawiwa nchi iwe urithi wao, kulingana na idadi ya majina yao. 54Kabila kubwa litapewa sehemu yao kubwa na dogo litapewa sehemu yao ndogo. Kila kabila litapewa urithi wake kulingana na idadi ya watu wake. 55Hata hivyo ugawaji wa nchi utafanywa kwa kura. Kila kabila litarithi kulingana na majina ya ukoo wao. 56Urithi wa kila kabila utagawanywa kwa kura, kila kabila litapata kulingana na ukubwa au udogo wake.”
57Hizi ndizo koo za Walawi zilizoorodheshwa na jamaa zao: Gershoni, Kohathi na Merari, 58Pamoja na jamaa za Libni, Hebroni, Mahli, Mushi na Kora. Kohathi alikuwa baba yake Amramu. 59Mkewe Amramu aliitwa Yokebedi binti yake Lawi, aliyezaliwa Misri. Huyu alimzalia Amramu watoto wawili wa kiume, Aroni na Mose, na binti mmoja, Miriamu. 60Taz Hes 3:2 Aroni alikuwa na watoto wa kiume wanne: Nadabu, Abihu, Eleazari na Ithamari. 61Taz Lawi 10:1-2; Hes 3:4 Nadabu na Abihu walikufa walipomtolea Mwenyezi-Mungu sadaka ya moto usiofaa. 62Idadi ya Walawi wanaume wenye umri wa mwezi mmoja na zaidi ilikuwa 23,000. Hawa hawakuhesabiwa pamoja na Waisraeli wengine kwa sababu wao hawakupewa urithi wowote miongoni mwao.
63Hao ndio wanaume Waisraeli walioorodheshwa na Mose na kuhani Eleazari katika nchi tambarare za Moabu, ngambo ya mto Yordani, karibu na Yeriko. 64Miongoni mwao hakuwamo hata mtu mmoja aliyesalia kati ya wale waliohesabiwa na Mose na kuhani Aroni ambao walifanya sensa ya kwanza jangwani Sinai. 65Taz Hes 14:26-35 Mwenyezi-Mungu alikuwa amesema kwamba wote watafia jangwani, na kweli hakuna hata mmoja wao aliyebaki hai, isipokuwa Kalebu mwana wa Yefune, na Yoshua mwana wa Nuni.


Hesabu26;1-65


Biblia Habari Njema kwa Watu Wote(BHN)

"Swahili Na Waswahili"Mbarikiwe.

No comments: