Swahili na Waswahili

Swahili na Waswahili
Waswahili na Mswahili Rachel Siwa...Pamoja Daima!!

Friday 28 July 2017

Kikombe Cha Asubuhi;kitabu cha Hesabu..19




Shalom,Habari za Asubuhi,Hamjambo,Mmeamkaje?

Tumshukuru Mungu wetu katika yote..

Msifuni Mwenyezi-Mungu! Nitamshukuru Mwenyezi-Mungu kwa moyo wangu wote, nikijumuika na jamii ya watu waadilifu. Matendo ya Mwenyezi-Mungu ni makuu mno! Wote wanaoyafurahia huyatafakari. Kila afanyacho kimejaa utukufu na fahari; uadilifu wake wadumu milele. Amesababisha matendo yake ya ajabu yakumbukwe; Mwenyezi-Mungu ni mwema na mwenye huruma. Huwapa chakula wenye kumcha; hasahau kamwe agano lake. Amewaonesha watu wake nguvu ya matendo yake, amewapa nchi za mataifa mengine ziwe mali yao. Matendo yake ni ya haki na ya kuaminika; kanuni zake zote ni za kutegemewa. Amri zake zadumu daima na milele; zimetolewa kwa haki na uadilifu. Aliwakomboa watu wake na kufanya nao agano la milele. Yeye ni mtakatifu na wa kutisha mno! Kumcha Mwenyezi-Mungu ni msingi wa hekima; wote wanaozitii amri zake hujaliwa busara. Sifa zake zadumu milele.

Asante Mungu wetu Sifa na utukufu tunakurudishia wewe
Wewe ni Mungu wetu Baba yetu na mlinzi wetu..
Asante kwa wema na fadhili zako kwetu..
Wewe ni Mungu wa Upendo,Mponyaji,Mfariji,Mwenye enzi
Baba wa Rehema,Baba wa Baraka,Utukuzwe daima Mungu wetu..
Asante kwa ulinzi wako wakati wote..
Asante kwa kutuchagua na kutupa kibali cha kuendelea kuiona leo hii..
Tunaomba utusamehe pale tulipokwenda kinyume nawe Mungu wetu
kwakuwaza,kwakunena,kwakutenda,kwakujua/kutojua..
Mfalme wa Amani nasi tunaomba utupe neema ya kuwasamehe wale waliotukosea..

Ee Mungu, ni nani aliye kama wewe? Wewe wasamehe dhambi za watu wako waliobaki, wala huyaangalii makosa yao. Hasira yako haidumu milele, ila wapendelea zaidi kutuonesha fadhili zako. Utatuhurumia tena, ee Mwenyezi-Mungu; utafutilia mbali dhambi zetu, utazitupa zote katika vilindi vya bahari.
Utuepushe katika majaribu Mungu wetu,Utuokoe na yule mwovu na kazi zake zote..
Ututakase Miili yetu na Akili zetu kwa Damu ya Mwanao Mpendwa Bwana na Mwokozi wetu Yesu Kristo..
Yeye aliteseka kwanza ili sisi tupate kupona..

Daima tunamshukuru Mungu, Baba wa Bwana wetu Yesu Kristo, wakati tunapowaombea. Maana tumesikia juu ya imani yenu kwa Kristo Yesu na juu ya mapendo yenu kwa watu wote wa Mungu. Imani yenu na mapendo yenu vina msingi katika tumaini mlilowekewa mbinguni. Mlipata kusikia juu ya hilo tumaini mara ya kwanza wakati mlipohubiriwa ule ujumbe wa ukweli wa Habari Njema. Injili inazidi kuzaa matunda na kuenea ulimwenguni kote kama vile ilivyofanya kwenu nyinyi tangu siku ile mliposikia juu ya neema ya Mungu na kuitambua ilivyo kweli. Mlijifunza juu ya neema ya Mungu kutoka kwa Epafra, mtumishi mwenzetu, ambaye ni mfanyakazi mwaminifu wa Kristo kwa niaba yetu. Yeye alitupa habari za upendo wenu mliojaliwa na Roho. Kwa sababu hiyo tumekuwa tukiwaombeeni daima tangu wakati tulipopata habari zenu. Tunamwomba Mungu awajazeni ujuzi kamili wa matakwa yake, pamoja na hekima yote na ujuzi wa kiroho. Hapo mtaweza kuishi kama anavyotaka Bwana na kutenda daima yanayompendeza. Maisha yenu yatakuwa yenye matunda ya kila namna ya matendo mema na mtazidi kukua katika kumjua Mungu. Mungu awajalieni nguvu kwa uwezo wake mtukufu ili muweze kustahimili kila kitu kwa uvumilivu. Na kwa furaha mshukuruni Baba, aliyewawezesha nyinyi kuwa na sehemu yenu katika mambo yale aliyowawekea watu wake katika ufalme wa mwanga. Yeye alituokoa katika nguvu ya giza, akatuleta salama katika ufalme wa Mwanae mpenzi. Kwake yeye tunakombolewa, yaani dhambi zetu zinaondolewa.
Roho Mtakatifu akatuongoze katika yote tupate kutambua/kujiambua
tukasimamie Neno lako Mungu wetu Sheria na Amri zako..
Ukatufanye chombo chema na tukatumike sawasawa na mapenzi yako..
Jehovah ukatubariki na kubariki Kazi zetu,Biashara,Masomo na vyote tunavyoenda kufanya/kutenda Mungu wetu tukatende kulingana na mapenzi yako..
Asante Mungu Baba katika yote..
Tunakushukuru na kukusifu daima..
Kwakuwa Ufalme ni wako Nguvu na Utukufu hata Milele..
Amina..!
Asanteni sana wapendwa wote mnaonitembea/kunisoma
Mungu akaonekane katika maisha yenu..
Baraka na Amani ziwafuate..
Nawapenda.

Majivu ya ng'ombe mwekundu

1Mwenyezi-Mungu aliendelea kuwaambia Mose na Aroni, 2“Haya ni masharti ya sheria ambayo mimi Mwenyezi-Mungu ninatoa. Waambieni Waisraeli wawaletee ng'ombe jike mwekundu asiye na dosari wala kasoro yoyote, na ambaye hajapata kufungwa nira. 3Nyinyi mtampa kuhani Eleazari ng'ombe huyo. Atatolewa nje ya kambi na kuchinjwa mbele ya kuhani huyo.
4“Kisha kuhani Eleazari atachukua kiasi cha damu na kuinyunyiza kwa kidole mara saba, kuelekea upande wa mbele wa hema la mkutano. 5Ngombe huyo mzima atateketezwa kwa moto mbele ya kuhani. Kila kitu chake kitateketezwa; ngozi, nyama, damu na utumbo wake. 6Halafu kuhani atachukua mti wa mwerezi, husopo na sufu nyekundu na kuvitia katika moto huo. 7Baada ya hayo, kuhani atazifua nguo zake na kuoga mwili kwa maji, halafu anaweza kuingia kambini; atakuwa najisi hadi jioni. 8Mtu atakayemteketeza ng'ombe huyo pia atazifua nguo zake kwa maji na kuoga mwili kwa maji, lakini naye pia atakuwa najisi hadi jioni. 9#Taz Ebr 9:13 Mtu aliye safi atayazoa majivu ya ng'ombe huyo na kuyapeleka mahali safi nje ya kambi. Yatahifadhiwa na kutumiwa na jumuiya nzima ya Israeli kutengeneza maji ya kuondoa najisi, ili kuondoa dhambi. 10Mtu atakayeyazoa majivu ya ng'ombe huyo lazima azifue nguo zake, lakini atakuwa najisi hadi jioni. Sharti hili ni la kudumu, na litawahusu Waisraeli na watu wengine watakaoishi pamoja nao.

Sheria kuhusu kutakaswa

11“Mtu akigusa maiti ya mtu yeyote, atakuwa najisi kwa siku saba. 12Siku ya tatu na ya saba mtu huyo atajiosha kwa yale maji ya utakaso, naye atakuwa safi. Lakini akiacha kujitakasa katika siku ya tatu na ya saba, mtu huyo atabaki kuwa najisi. 13Agusaye maiti, yaani mwili wa mtu aliyekufa, asipojitakasa, analitia najisi hema la Mwenyezi-Mungu, naye atatengwa na wana wa Israeli. Mtu huyo atabaki najisi kwa sababu hakunyunyiziwa yale maji ya utakaso.
14“Na hii ndiyo sheria ya kufuatwa kama mtu akifia hemani: Kila mtu atakayeingia ndani ya hema hilo, au aliye ndani ya hema hilo, atakuwa najisi kwa siku saba. 15Kila chombo kilicho wazi ambacho hakina kifuniko juu yake kitakuwa najisi. 16Mtu yeyote akigusa mwili wa mtu aliyeuawa au aliyekufa kifo cha kawaida nje ya nyumba, au akigusa mfupa wa mtu au kaburi, atakuwa najisi kwa siku saba.
17“Kwa ajili ya wale waliojitia najisi watachukua majivu ya sadaka ya kuondoa dhambi iliyoteketezwa, majivu hayo yatachanganywa na maji ya mtoni katika chungu. 18Mtu aliye safi atachukua husopo, halafu ataichovya katika maji hayo, kisha atainyunyizia hema, vyombo vyote vilivyomo ndani ya hema na watu waliokuwamo ndani. Atamnyunyizia pia mtu aliyegusa mfupa wa mtu, au mwili wa mtu aliyeuawa au aliyekufa kifo cha kawaida, au aliyegusa kaburi. 19Katika siku ya tatu na ya saba, mtu aliye safi atamnyunyizia mtu aliye najisi maji hayo; hivyo katika siku ya saba, atamtakasa mtu huyo aliye najisi, naye atazifua nguo zake na kuoga, na jioni atakuwa safi.
20“Lakini mtu akiwa najisi asipojitakasa, mtu huyo atakataliwa mbali na jumuiya, kwa kuwa analitia najisi hema la Mwenyezi-Mungu. Kwa vile hakunyunyiziwa maji ya utakaso, yu unajisi. 21Watu watalishika sharti hili daima. Mtu atakayenyunyiza maji ya kutakasia ataosha nguo zake; naye anayegusa maji hayo ya najisi atakuwa najisi hadi jioni. 22Chochote atakachogusa mtu najisi kitakuwa najisi, na yeyote atakayekigusa kitu hicho atakuwa najisi mpaka jioni.”

Hesabu19;1-22


Biblia Habari Njema kwa Watu Wote(BHN)

"Swahili Na Waswahili"Mbarikiwe.

No comments: